Historia ya biolojia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
"Mti wa Uzima" wa Ernst Haeckel (1879).

Historia ya biolojia inapitia maendeleo ya somo hilo muhimu la sayansi. Ingawa biolojia katika mtindo wake wa kisasa ni hatua ya hivi karibuni, sayansi zinazohusiana na zinazojumuishwa ndani yake zimechunguzwa tangu kale.

Falsafa ya maumbile ilisomwa tangu siku za ustaarabu wa kale wa Mesopotamia, Misri, Bara Hindi na China.

Hata hivyo, asili ya biolojia ya kisasa na mtazamo wake kwa utafiti wa viumbe mara nyingi hupata asili yake kwa Ugiriki wa kale.[1] Huku mafunzo rasmi ya udaktari yakiwa yalianza wakati wa Hippokrates (460 KK hivi - 370 KK hivi), ni Aristotle (384 KK - 322 KK) ambaye alichangia sana ustawisho wa biolojia. Muhimu hasa ni "Historia ya Wanyama" na kazi zake nyingine ambazo alionyesha mwelekeo wa mwanaviumbe, na baadaye kazi za kijarabati zilizolenga usababisho wa kibiolojia na tofauti za uhai.

Theophrastus, mrithi wa Aristotle katika Lyceum, aliandika mfululizo wa vitabu juu ya botania ambavyo vilisalia kama mchango muhimu zaidi wa mambo ya kale kwa sayansi za mimea, hadi Karne za Kati.

Maendeleo muhimu katika utafiti na ustawisho wa biolojia yalikuzwa kwa juhudi za madaktari Waislamu kama vile msomi Mwafrika na Mwarabu al-Jahiz (781-869) katika zuolojia, [2]mwanabiolojia wa Kikurdi Al-Dinawari (828-896) katika botania,[3] na daktari wa Kiajemi Rhazes (865-925) katika anatomia na fiziolojia. Wanafalsafa hao walifafanua, kupanua, na kuboresha nadharia na utaratibu wa Kigiriki wa biolojia. Udaktari ulisomwa vizuri zaidi na wasomi wa Kiislamu waliofanya kazi katika mila za kifalsafa za Kigiriki, huku historia ya asili ikivutiwa sana na mawazo ya Aristotle, hasa katika kuunga mkono mfumo thabiti wa ngazi wa uhai.

Biolojia ilianza kuendelea na kukua haraka baada ya uboreshaji mkubwa wa darubini na Antony van Leeuwenhoek. Hapo ndipo wasomi waligundua manii bakteria, infusoria na ugeni tu na tofauti ya maisha ya hadubini. Uchunguzi wa Jan Swammerdam ulileta maslahi mapya katika entomolojia ikajenga mbinu za msingi za kuchangua na kutia madoa kwa hadubini.[4]

Maendeleo katika somo la hadubini pia yalikuwa na athari kubwa kwa kufikiri kibiolojia kwenyewe. Mapema katika karne ya 19, wanabiolojia kadhaa waliashiria umuhimu mkuu wa seli. miaka ya 1838 na 1839, Schleiden na Schwann walianza kuendeleza mawazo kuwa (1) kitengo muhimu cha viumbe ni seli na (2) seli za binafsi zina sifa zote bainifu za uhai, ingawa walipinga wazo kwamba (3) seli zote hutokana na mgawanyiko wa seli nyingine. Kwa msaada wa kazi ya Robert Remak na Rudolf Virchow, hata hivyo, katika miaka ya 1860 wanabiolojia wengi walikubali kanuni zote tatu za kile kilichojulikana kama nadharia ya seli.[5]

Wakati huohuo, taksonomia na uainishaji vikawa viini katika utafiti wa historia ya asili. Carolus Linnaeus alichapisha taksonomia ya msingi kwa ajili ya ulimwengu wa asili mwaka wa 1735 (mabadiliko yake yametumika tangu wakati huo), na miaka ya 1750 ilileta majina ya kisayansi ya spishi zake zote.[6] Georges-Louis Leclerc, Comte de Buffon, walielezea spishi kama vikundi bandia na viumbe hai kama vya kufulika - hata wakipendekeza uwezekano wa asili ya pamoja. Ingawa alikuwa anapinga mageuko, Buffon ni kielelezo muhimu katika historia ya mawazo ya mageuko; kazi yake ilishawishi nadharia za mageuko za Lamarck na Darwin.[7]

Mawazo makubwa ya mageuko yalitokana na kazi ya Jean-Baptiste Lamarck. Hata hivyo, ni mwanaviumbe Mwingereza Charles Darwin, akiunganisha mtazamo wa jiografia kama inavyoathiriwa na biolojia wa Humboldt, jiolojia ya kulingana ya Lyell, maandishi ya Thomas Malthus juu ya ukuaji wa idadi ya watu, na utaalamu wake mwenyewe wa kimofolojia, aliyeunda nadharia ya mageuko iliyokuwa na mafanikio zaidi iliyotokana na uteuzi asilia; mawazo sawa na ushahidi yalimfanya Alfred Russel Wallace kufikia uamuzi sawa.[8]

Ugunduzi wa uwakilishi wa kimwili wa urithi ulikuja pamoja na kanuni za mageuko na taaluma ya jenetikia inayohusu idadi ya watu. Katika miaka ya 1940 na mwanzoni mwa miaka ya 1950, majaribio yaliashiria kwa DNA kama sehemu ya kromosomu iliyoshikilia jeni. Kuzingatia viumbe vipya vya mfano kama vile virusi na bakteria, pamoja na ugunduzi muundo maradufu wa helikali wa DNA mwaka wa 1953, kuliashiria mpito kwa enzi ya jenetiki ya molekiuli.

Tangu miaka ya 1950 hadi sasa, biolojia imenyooshwa sana katika miliki ya molekiuli. Msimbo-jeni ulibanguliwa na Har Gobind Khorana, Robert W. Holley na Marshall Warren Nirenberg baada ya DNA kufahamika kuwa na kodoni.

Mwisho, Mradi wa Jenomu ya Binadamu ulianzishwa mwaka wa 1990 na lengo la kuwa na ramani ya jumla ya jenomu ya binadamu. Kimsingi, mradi huu ulikamilika mwaka wa 2003,[9] hata hivyo uchambuzi zaidi bado unachapishwa. Mradi wa Jenomu ya Binadamu ilikuwa hatua ya kwanza katika jitihada jumla za kushirikisha elimu iliyokusanywa ya biolojia katika fasili ya molekiuli ya kutenda ya mwili wa binadamu na miili ya viumbe vingine.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Magner, Historia ya Sayansi za Maisha
  2. Mehmet Bayrakdar, "Al-Jahiz And the Rise of Biological Evolutionism", The Islamic Quarterly, Third Quarter, 1983, London.
  3. Fahd, Toufic. uk. 815.  Missing or empty |title= (help); |chapter= ignored (help) , katika Morelon, Régis; Rashed, Roshdi (1996). Encyclopedia of the History of Arabic Science 3. Routledge. ISBN 0415124107. 
  4. Magner, Historia ya Sayansi za Maisha, pp 133-144
  5. Sapp, Mwanzo, sura ya 7, Coleman, Biolojia katika karne ya kumi na tisa, sura ya 2
  6. Mayr, Ukuaji wa Mawazo ya Kibiolojia, sura ya 4
  7. Mayr, Ukuaji wa Mawazo ya Kibiolojia, sura ya 7
  8. Mayr, Ukuaji wa Mawazo ya Kibiolojia, sura ya 10: "Ushahidi wa Darwin wa mageuko na asili ya pamoja", na sura ya 11: "Sababu ya mageuko: uteuzi asilia"; Larson, Mageuko, sura ya 3
  9. "BBC NEWS". 2003-04-14. Iliwekwa mnamo 2006-07-22.  Text " Science/Nature " ignored (help); Text " Human genome finally complete " ignored (help)