Wolfgang Amadeus Mozart

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Wolfgang Amadeus Mozart

Wolfgang Amadeus Mozart (Salzburg, 27 Januari 1756Vienna, 5 Disemba 1791) alikuwa mtunzi mashuhuri wa opera na mpigaji wa ajabu sana wa piano kutoka nchini Austria.

Licha ya kuwa na maisha mafupi (alifariki akiwa na umri wa miaka 35 tu), alitunga zaidi ya nyimbo 800 za kila aina, zikiwemo opera (muziki wenye hadithi) Don Giovanni na Die Zauberflöte (Filimbi ya Ajabu). Watu wanaamini kwamba Mozart ni moja kati ya watunzi bora wa muda wote wa nyimbo za Ulaya, ikimpelekea mtunzi mwenzake Joseph Haydn kuandika kuwa: "kizazi kingine hakitaona talanta kama yake tena kwa karne moja".

Kazi zake alizianza na minuet (dansi) aliyoitunga akiwa na umri wa miaka minne, na alizimalizia kwa kipande chake cha mwisho, Requiem, ambacho alikiacha hajakimaliza.

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Familia na miaka ya mwanzoni[hariri | hariri chanzo]

Mahala alipozaliwa Mozart huko Getreidegasse 9, Salzburg, Austria

Mozart alizaliwa katika familia ya wanamuziki. Baba yake, Leopold Mozart, alikuwa mpiga zeze na mtunzi mashuhuri ambaye alifanya kazi na Askofu mkuu wa Salzburg. Alikuwa na dada mkubwa, Maria Anna, aliyeitwa kwa jina la utani "Nannerl" (kulikuwa na ndugu wengine ambao walifariki wakiwa watoto).

Mozart alibatizwa asubuhi baada ya kuzaliwa kwake kwenye kanisa kuu la mjini Salzburg. Jina lake kamili kwa Kilatini lilikuwa “Joannes Chrysostomus Wolfgangus Theophilus Mozart”. Kwa kawaida alikuwa akifahamika kama “Wolfgang Amadeus Mozart”, na jina lake la utani lilikuwa “Wolfi”.

Nyumba alipozaliwa katika mtaa unaoitwa Getreidegasse, sasa hivi ni sehemu ya maonyesho ya Mozart.

Mozart alikuwa mtoto wa ajabu: tangu akiwa mdogo alikuwa na kipaji cha muziki ambacho si cha kawaida. Baba yake alimpa ala kadhaa ili amfundishe mwanawe kutunga muziki.

Wolfgang alijifunza kupiga kinanda akiwa na umri wa miaka mitatu, na baada ya muda mfupi akajifunza pia kupiga zeze na organo vilevile.

Kuna vipande viwili vifupi vya noti za piano alizotunga akiwa na umri wa miaka mitano, lakini ziliandikwa kwa mwandiko wa baba yake, hivyo si rahisi kusema kiasi cha msaada alioweza kuupata.

Baadaye baba yake akaanza kumruhusu mtoto wake, na kumfanya aanze kupiga kazi kwenye kumbi huku kukiwa na watu muhimu kibao mbele yake. Siku hizi hili linaweza kuitwa “ukandamizaji” wa watoto wenye vipaji, lakini miaka hiyo watu walikuwa hawaoni tatizo kumwachia mtoto atumike kwa namna hii. Inaonekana kwamba hili halikumwathiri kabisa, na hivyo akajikuta anakua akiwa mtunzi mkubwa kama vile alivyostahili kuwa.

Mozart alianza kupiga kwenye umma mjini Salzburg alipokuwa na umri wa miaka mitano, halafu akachukuliwa na kuelekea jijini Vienna akiwa na umri wa miaka sita.

Pia aliwahi kupiga mjini Linz na Pressburg (leo hii inaitwa Bratislava). Aliwahi kupiga mara mbili mbele ya malkia Maria Theresa wa Austria. Katika konseti hili alipiga nyimbo ambazo hata watu wazima wanaweza kuzicheza, na muziki ambao watu hawakuwahi kuusikia. Alikuwa akibuni mitindo na kuicheza huku akiwa amevaa kinanda, au akiwa hatazami mikono yake inapiga wapi na akipitisha mikono huku na huku. Pia alitengeneza miziki ambayo inafuata milio ya vitu vingine na alikuwa akiziweka mbeleni kwake.

Watu wengi walimsikia kijana huyu mashuhuri na kuandika habari zake na ndiyo maana hadi leo hii tunajua mengi yaliyotokea. Pia inajulikana kwamba alikuwa anaweza kukumbuka noti za muziki aliotunga akizichungulia mara moja tu.

Safari za kwanza nchi za nje[hariri | hariri chanzo]

Kwa muda mfupi Mozart akawa anasafiri nchi za nje kwa shughuli za kimuziki. Aliwahi kutumbuiza Munich, Prague, Paris, The Hague na London. Huko mjini London, alipiga mbele ya mfalme George III na kubahatika kukutana na mtunzi mmoja aitwaye Johann Christian Bach, mmoja kati ya watoto wa Johann Sebastian Bach. Alipenda sana muziki wa Christian Bach na hata akaamua kufanya pamoja naye kazi ya muziki.

Mnamo mwaka 1767 alikuwa zake mjini Vienna tena ambapo alipata ugonjwa wa ndui, lakini alipona, na baba yake aliona hili kama ni dalili kutoka kwa Mungu kwamba mtoto wake atakuwa salama.

Baada ya hapo akaenda nchini Italia ambapo alipata kusikia miziki ya watunzi wengine wengi wa Kiitalia. Watunzi hao ni pamoja na Gregorio Allegri ambaye aliandika wimbo Miserere ambao uliandikwa kwa ajili ya Papa na kwa kuimbiwa na kwaya nzima ya Basilika la Mt. Petro (Vatikani).

Katika tungo hizo, hakuna mtu yeyote aliyeruhusiwa kuona kilichoandikwa kwenye muziki huo, hivyo hakukuwa na mtu mwingine aliyeweza kuziimba katika kwaya. Cha kushangaza Mozart alizisikia mara moja tu na kukaa chini na kuzichezea kwa kutumia kumbukumbu yake tu!

Alikutana na Papa na kupewa naye knighthood ya Order of the Golden Spur.

Mnamo mwaka 1777, alikwenda safari akiwa na mama yake.

Huko Mannheim akatokea kumpenda msichana mmoja aliyeitwa Aloysia Weber. Alikuwa na umri wa miaka 16 tu na alikuwa akisomea kuimba. Mozart akataka amchukue kisha aende naye Italia ili amfanye maarufu, lakini baba yake akamwandikia barua kali ya mkwara wa kumtaka aache kufikiria huo upuuzi.

Kunako 1778, Mozart na mama yake walikuwa mjini Paris, lakini wakiwa huko mama akafariki dunia.

Mozart mjini Vienna[hariri | hariri chanzo]

Mozart aliandika opera ndogondogo kadhaa akiwa bwana mdogo, lakini opera yake ya kwanza na muhimu ilikuwa Idomeneo, ambayo ilianza kutumbuizwa mjini Munich mnamo 1780.

Mwaka uliofuatia akaenda zake Vienna. Lakini muda huo alikuwa akifanya kazi, kama baba yake, kwa Askofu Mkuu wa Salzburg. Aliporudi tena Salzburg akalumbana na Askofu Mkuu, kitendo ambacho kilipelekea kumfanya atimuliwe mbali. Mozart akarudi tena mjini Vienna ambapo alitumia maisha yake yote yaliyombakia.

Mnamo mwaka 1782, alimwoa Constanze Weber, mmoja kati ya wadogo watatu wa Aloysia (ambaye kwa wakati huo alikuwa ameolewa na mtu mwingine). Walibarikiwa kupata watoto saba, lakini kwa bahati mbaya watano kati yao walikufa wakiwa bado wadogo. Baba yake Mozart hakupitisha ndoa hiyo. Constanze alikuwa mke mpendwa, lakini, kama Mozart, hakuwa mzuri sana katika suala la kutafuta fedha, hivyo mara nyingi walikuwa maskini.

Mwaka huohuo 1782, Mozart akatunga opera nyingine iliyompa mafanikio makubwa kabisa: Die Entführung aus dem Serail ("Kutekwa nyara kutoka Seraglio"). Ni hadithi moja maarufu inayoelezea kwamba, baada ya mtawala kusikia opera, akamwuliza Mozart kama kulikuwa na “noti nyingi?”. Mozart akamjibu yule mtawala: “Zipo kiasi cha zitakazotakikana, Mtukufu.”

Tangu hapo, Mozart akaanza kutumbuiza katika makonseti mfululizo akipiga piano yake mwenyewe, iliyokuwa ikielekezwa kutoka kwenye kinanda.

Katika safari zake akapata kukutana na mtunzi mwenzi Joseph Haydn na hao watu wawili wakawa marafiki wakubwa; mara nyingi walipiga pamoja kwenye string quartet. Siku moja Haydn aliyasema haya kwa Leopold Mozart: "Mbele ya Mungu na nikiwa msemakweli ni kwamba mtoto wako ni mtunzi mkubwa anayejulikana nami kibinafsi au kijina. Ana ladha, na cha zaidi ni kwamba, mtu mwenye uelewa mkubwa katika utunzi."

Mozart alikuwa mwanachama wa Masonic Lodge kama alivyokuwa Haydn, na alitengeneza kazi kadhaa kwa ajili yake.

Picha ya Mozart (ambayo haikumalizwa kuchorwa), 1782

.

Mozart huko Prague[hariri | hariri chanzo]

Baada ya muda fulani watazamaji wengi wa mjini Vienna hawakuwa wakimwunga mkono sana Mozart, hivyo mara nyingi alienda zake mjini Prague mahali ambapo washabiki wengi walikuwa wakimpenda. Opera yake Ndoa ya Figaro ilikuwa maarufu sana kule, na mwaka 1787 akatumbuiza kwa mara ya kwanza opera yake Don Giovanni.

Kuumwa na kufa kwake[hariri | hariri chanzo]

Kuna hadithi chungu nzima zinazohusu ugonjwa wa mwisho na kifo cha Mozart, na si rahisi kuwa na hakika ya kipi hasa kilitokea.

Alikuwa akifanya kazi kwenye opera The Magic Flute ambayo ni moja kati ya kazi zake kubwa na ni maarufu sana hadi leo hii. Opera hiyo iliandikwa kwa Kijerumani, na si kwa Kiitalia, kama ilivyo kwa opera zake nyingine nyingi. Katika hali nyingine ipo kama Kiingereza hivi pantomime.

Wakati huohuo aliokuwa akifanya kazi hii akaombwa na mtu mmoja atunge kwa siri requiem (maombi kwa ajili ya marehemu). Pia akaombwa atunge opera ya Kiitalia La Clemenza di Tito. Hii iliimbwa mjini Prague wakati wa Septemba mwaka 1791. Mwishoni kabisa mwa mwezi huo The Magic Flute ilipigwa kwa mara ya kwanza. Baada ya hapo Mozart akawa anashughulikia vilivyo Requiem.

Alipata kugundua kwamba tayari yu mgonjwa sana, na kwa maana hiyo ile requiem ilikuwa kwa ajili yake mwenyewe. Alikufa kabla hajaweza kuimaliza. Constanze akamwomba mtunzi mwingine, aliyeitwa Franz Xaver Süssmayr, kuimalizia kazi. Hadi leo hii hatuna hakika ni kipi kidogo alichoongezea Süssmayr, lakini yamkini karibu muziki wote ulikuwa kazi ya Mozart mwenyewe.

Mozart alizikwa kwenye kaburi lisilojulikana kwa sababu kulikuwa hakuna fedha za kutayarishia mazishi mazuri.

Muziki wa Mozart[hariri | hariri chanzo]

Muziki wa Mozart, kama ule wa Joseph Haydn, ni muziki mashuhuri sana unaojulikana kama Staili ya klasiki. Wakati huo alipoanza kutunga, kipindi cha muziki wa Baroque kilikuwa kinaelekea ukingoni. Ladha za muziki zilianza kupatikana katika muziki. Mozart alikuwa mtunzi wa kwanza kutunga muziki wa kutumia piano, kifaa pekee kilichokuwa kinakuja kuwa maarufu.

Alianza karibu kila aina ya muziki: symphonies, operas, solo concertos, chamber music, hasa string quartets na string quintets, na piano sonata. Pia, aliandika miziki kibao ya kidini, ikiwemo mass, na vilevile miziki mashuhuri kama vile dansi, divertimenti na serenade.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Kujisomea zaidi[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Wikiquote ina mkusanyiko wa dondoo kuhusu:
Digitized, scanned material (books, sheet music)
Muziki ya kuchapishwa