Saratani

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Kansa)

Kwa kundinyota yenye jina hili angalia Saratani (kundinyota)

Picha ya eksirei inayoonyesha kivuli cha kansa katika mapafu.

Saratani (kutoka Kiarabu سرطان, sartan) au kansa (kutoka Kiingereza cancer) ni aina za ugonjwa unaotokana na seli za mwili zinazoanza kujigawa yaani kukua bila utaratibu na bila mwisho.

Asili ya jina[hariri | hariri chanzo]

Jina la saratani linatokana na neno la Kiarabu sartan linalomaanisha pia "kaa". Sababu yake ni ya kwamba mtaalamu Galenos wa Ugiriki wa Kale aliona uvimbe uliofanana na miguu ya kaa. Jina hili lilitafsiriwa baadaye kwa lugha nyingi.

Hata kwa Kiingereza neno "cancer" linaweza kutaja pia jenasi moja ya kaa. Vivyo hivyo jina la kundinyota ya zodiaki ni "Cancer (constellation)" kwa Kilatini - Kiingereza na Saratani (kundinyota) kwa Kiswahili, yote kwa maana ya mnyama, si ya ugonjwa.

Matokeo ya ugawaji hovyo wa seli mwilini[hariri | hariri chanzo]

Ukuaji huu unaleta uvimbe mwilini unaozidi kuwa mkubwa hadi unabana viungo vya mwili kama neva, mishipa ya damu, ubongo, mapafu, maini, utumbo na kadhalika na hivyo kuzuia visifanye kazi. Hivyo inasababisha kifo, mara nyingi baada ya kipindi cha maumivu makali.

Pamoja na hayo kansa / saratani huwa na tabia za kujisambaza mwilini mahali pengi baada ya muda fulani na kusababisha kutokea kwa vimbe nyingi mwilini vinavyoendelea kukua hovyo. Kama uvimbe hauna uwezo wa kusambaza seli zake mwilini na kusababisha vimbe mpya si saratani.

Kansa inaweza kutokea kwa mtu yeyote lakini hutokea zaidi kwa watu wenye umri mkubwa na watu wanaoathiriwa na kemikali mbalimbali. Katika nchi zilizoendelea ambako wanachi hufikia umri mkubwa saratani iko kati ya sababu kuu za kifo.

Uchunguzi na matibabu ya kansa ni utaalamu wa onkolojia ndani ya somo la tiba.

Aina za saratani[hariri | hariri chanzo]

Zipo baadhi ya saratani zinazosababishwa na virusi kama vile saratani ya shingo ya kizazi. Saratani huweza kutokea kwenye sehemu mbalimbali za mwili kama vile mapafu, matiti[1], kibofu cha mkojo, shingo ya uzazi, ovari, utumbo, koo, mdomo, ngozi n.k.

Jinsi ya kuepuka saratani[hariri | hariri chanzo]

Hali nzuri ya lishe na mtindo bora wa maisha ni kigezo muhimu sana katika kuzuia saratani[2] na pia ni sehemu muhimu ya matibabu na kudumisha maisha bora baada ya matibabu ya saratani kumalizika.

Matumizi ya baadhi ya vyakula huweza kuongeza uwezekano wa kupata baadhi ya saratani na vyakula vingine huweza kupunguza uwezekano wa kupata saratani.

Uzito wa mwili unapozidi kiasi unaweza pia kuongeza uwezekano wa kupata baadhi ya saratani.

Pamoja na mtindo bora wa maisha unaodumisha ulaji bora, mazoezi ya mwili, uzazi na unyonyeshaji wa watoto wachanga, ni muhimu pia kupata na kufuata ushauri wa wataalamu wa afya kuhusu upimaji unaoweza kugundua mapema baadhi ya saratani na kuzidhibiti. Mfano wa upimaji huo ni pamoja na upimaji wa matiti na shingo ya kizazi kwa wanawake. Kuhusu vipimo au uchunguzi unaohitajika, pata maelezo zaidi kutoka kwa wataalamu wa afya.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. HANS, RAPHAEL, "Saratani ya matiti kwa wanaume ipo", A-Z 360 (in en-US), retrieved 2018-10-18 
  2. RAPHAEL HANS. A-Z 360: Matokeo ya utafutaji wa saratani (en-US). A-Z 360. Iliwekwa mnamo 2018-10-18.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya tiba bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Saratani kama sababu yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.