Barabara ya hariri

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Njia za biashara ya kimataifa kati ya China na Ulaya wakati wa karne ya 1 BK (majina ya nchi kwa Kilatini: Sinae = China, Media Persis = Uajemi)

Barabara ya hariri (kwa Kiingereza: "Silk road") ilikuwa njia muhimu ya biashara kati ya China kwa upande mmoja na Afrika Mashariki, Mashariki ya Kati halafu Ulaya kwa upande mwingine. Biashara hiyo iliendelea tangu karne za kabla ya Kristo.

Jina la "barabara ya hariri" limetokana na hariri ambayo kwa muda mrefu ilitengenezwa katika China pekee ikawa kati ya bidhaa zilizotafutwa sana duniani kwa bei ya juu.

Mnamo Juni 2014, UNESCO imetangaza sehemu Chang'an-Tianshan ya barabara hiyo kuwa mahali pa Urithi wa Dunia.

Mtandao wa njia mbalimbali zilizopita Asia ya Kati[hariri | hariri chanzo]

Barabara ya hariri haikuwa njia moja tu bali jumla ya njia za misafara kati ya China na nchi za Magharibi zilizopita katika Asia ya Kati.

Kulikuwa na njia za kando, hasa baharini, kati ya China na Uhindi halafu kutoka Uhindi hadi Irak au Misri. Njia za bahari zilikuwa muhimu hasa kama njia ya nchi kavu ilikatika wakati wa vita au ukosefu wa usalama. Kuna vipindi vichache ambako eneo lote la barabara ya hariri lilikuwa na usalama, hasa wakati wa utawala wa Wamongolia. Vinginevyo safari zilikuwa za hatari zikachukua muda mrefu. Bidhaa zilipita mikononi mwa wanafanyabiashara mbalimbali zikaongezewa bei njiani.

Njia ya bidhaa, watu na mawazo[hariri | hariri chanzo]

Si bidhaa tu ndizo zilizosafiri kwenye barabara ya hariri. Wasafiri, sanaa, mawazo, mafundisho, dini na magonjwa walipita pia kwa njia hiyo.

Teknolojia kama za kutengenezwa kwa karatasi au kuchapishwa kwa vitabu zilipita njia hiyo kutoka China hadi Asia ya Magharibi na kutoka huko hadi Ulaya.

Uenezaji wa Ubuddha kwenda Mongolia na China katika karne ya 1 BK, wa Ukristo kufika China katika karne ya 3 na wa Uislamu kuelekea mashariki katika karne ya 8 ulifuata barabara hii.

Njia ya magonjwa[hariri | hariri chanzo]

Magonjwa yalipita njia hiyohiyo. Kwa mfano tauni ilianza katika miaka ya 1330 katika China kwenye jimbo la Yunnan. Ugonjwa huu unategemea viroboto kama kituo cha virusi vyake. Farasi za jeshi la Mongolia na biashara ya ngozi ilipeleka viroboto wale hadi Bahari Nyeusi. Mwaka 1348 wafanyabiashara Waitalia kutoka Bahari Nyeusi waliingiza ugonjwa Ulaya yenyewe ulikoua robo ya wakazi wote.

Barabara mpya ya hariri ("One Belt, One Road Initiative" au "Silk Road Economic Belt and the 21st-century Maritime Silk Road"); nyekundu: China; machungwa: nchi wanachama wa Benki ya Uwekezaji wa Miundombinu ya Asia (Asian Infrastructure Investment Bank)

Barabara mpya ya hariri[hariri | hariri chanzo]

Tangu mwaka 2013 serikali ya China imetangaza mpango wa "barabara mpya ya hariri" unaolenga kuimarisha na kupanua ushirikiano wa China, Asia ya Kati, Asia ya Magharibi na Ulaya, pamoja na sehemu za Afrika. Jina rasmi kwa Kiingereza ni "Belt and Road Initiative" au "Silk Road Economic Belt and the 21st-century Maritime Silk Road".

Kwa kushirikiana na nchi za maeneo hayo China imeanza kujenga au kupanua barabara na njia za reli. Kati ya miradi mingi iliyoanzishwa iko njia ya reli inayounganisha China ya magharibi na Kazakhstan na kuendelea hadi Urusi na Ulaya ya Magharibi kwa umbali wa takriban kilomita 12,000 ("New Eurasian Land Bridge"). Sehemu nyingine ni Ushoroba wa Kiuchumi wa China na Pakistan ("China–Pakistan Economic Corridor")[1] ambako barabara kuu na reli zinaunganisha China ya Magharibi na bandari mpya ya Gwadar kwenye Bahari Hindi. Bandari hii ilijengwa pia na makampuni ya China.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Kujisomea[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Barabara ya hariri kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.