Augusto

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Kaisari Augusto)
Sanamu ya Kaisari Augusto.

Augusto alikuwa Kaisari wa kwanza wa Dola la Roma kuanzia mwaka 27 KK hadi 14 BK. Jina lake la kiraia lilikuwa Gaius Octavius. Alizaliwa Italia tarehe 23 Septemba 63 KK.

Octavius alikuwa mpwa wa Julius Caesar aliyempenda kijana huyo na kumteua kama mrithi katika wasia wake.

Historia ya Augusto ina vipindi viwili:

Majina[hariri | hariri chanzo]

Sanamu ya Kaisari Augusto aliyeabudiwa kama mungu; sadaka zilichomwa mbele yake.

Augusto anajulikana kwa majina mbalimbali.

  • alizaliwa kama Gaius Octavius
  • baada ya kuasiliwa na Caesar alitumia jina lake, hivyo aliitwa Gaius Iulius Caesar Octavianus yaani "Julius Caesar wa familia ya Octavius"
  • tangu mwaka 31 KK alitumia pia cheo "Imperator" (mwenye amri, "amiri") kama jina la kwanza
  • mwaka 27 KK alipewa jina la heshima la "Augustus" (anayestahili kuabudiwa) akaitwa "Imperator Caesar Augustus"

Mrithi wa Caesar[hariri | hariri chanzo]

Kifo cha Caesar (taswira ya 1867) - Tar. 15 Machi 44 KK Julius Caesar aliuawa na Marcus Junius Brutus na Gaius Cassius Longinus.

Alikuwa kijana wa miaka 19 aliyejiandaa kuwa afisa wa jeshi kwa mara ya kwanza katika maisha yake aliposikia habari za kuuawa kwa Julius Caesar. Alikimbilia Roma mara moja alipopata habari ya kuwa Caesar alimsiliki na kumtaja kama mrithi katika wasia. Hapo aliamua kulipiza kisasi juu ya wauaji wa Caesar, hivyo akaingia katika siasa ya Roma na kipindi cha vita vya wenyewe kwa wenyewe kilichofuata mauaji ya kiongozi wa dola.

Kushindana na kupatana na Marcus Antonius[hariri | hariri chanzo]

Rafiki yake marehemu, Marcus Antonius, hakukubali wasia akatwaa mali yote, lakini watu wengi na wanajeshi wa Caesar walisimama upande wa Octavius. Huyo aliajiri askari na kujenga jeshi na mwaka 43 KK alitwaa mji wa Roma kwa nguvu ya kijeshi wakati Marcus Antonius alikuwa mbali huko Gallia.

Senati ya Roma ilikubali hatua hii na kumchagua kuwa seneta. Aliendelea kuongoza jeshi la Senati na kumshinda Marcus Antonius kwenye mapigano huko Italia ya Kaskazini.

Konsuli wa Roma na mtawala katika ushirikiano[hariri | hariri chanzo]

Baada ya ushindi huo alikubaliwa kama konsuli wa Roma akaendelea kupatana na Marcus Antonius na kujenga ushirikiano naye. Pamoja walitawala Roma baada ya kupewa na senati madaraka ya kidikteta kwa muda wa miaka 5 na baadaye miaka 5 tena.

Mwaka 42 KK walifaulu kuwashinda wauaji wa Caesar waliokaa Ugiriki na baadaye waligawana eneo la dola kati yao: Octavianus alikuwa mkuu wa sehemu ya magharibi na Marcus Antonius mkuu wa sehemu za mashariki alipomwoa Kleopatra malkia wa Misri.

Mapigano ya baharini ya Aktium' ya 31 KK' (taswira ya 1672).
Dola la Roma baada ya Augusto.
kijani nyeusi: Majimbo chini ya Roma
kijani nyeupe: maeneo lindwa chini ya Roma yenye kiwango cha kujitawala;
kijani nyeupe nje ya mstari mweusi: Jimbo la Germania Magna lililopotea baada ya mwaka 9

Ushindi juu ya Marcus Antonius[hariri | hariri chanzo]

Maelewano kati yao yalizorota na mwaka 33 KK walitengana. Octavianus alimshinda Marcus katika mapigano ya baharini huko Aktium tarehe 2 Septemba 31 KK na huyo alijiua pamoja na Kleopatra.

Baada ya kuvamia na kuteka Misri Octavianus alirudi Roma mjini mwaka 29 KK akawa mtawala pekee.

Raia wa kwanza[hariri | hariri chanzo]

Huko Roma alishangaza watu wote akirudisha mamlaka yake ya kidikteta kwa senati. Aliombwa kuendelea kama mkuu wa jeshi akakubali.

Alikataa kupokea madaraka ya dikteta kwa muda wa maisha yake. Kwa njia hiyo alirudisha katiba ya jamhuri iliyotawaliwa na senati na maafisa yake.

Lakini hali halisi alishika mamlaka yote kama mtawala mkuu aliyeheshimu taasisi za jamhuri. Ni hekima hii iliyosifiwa na wengi ya kuwa hakuendelea kujipatia cheo cha mfalme au cha dikteta akaridhika kuitwa raia wa kwanza.

Utawala wake ulileta kipindi kirefu cha amani ya ndani. Wananchi walioteseka kwa miaka ya vita vya wenyewe kwa wenyewe waliweza kujenga maisha upya na uchumi ulistawi.

Milki kubwa ya Misri ilikuwa sehemu ya Dola la Roma. Hata sehemu nyingi za Germania ziliingizwa katika dola.

Vita vya pekee vilivyoenda vibaya vilikuwa jaribio la kupanua mipaka ya Roma katika Germania hadi mto Elbe. Wagermania waliangamiza legioni tatu na mpaka wa Kiroma ulirudishwa hadi mto Rhine.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu Kaizari fulani wa Roma bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Augusto kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.