Nyangao

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Nyangao ni kata iliyokuwa Wilaya ya Lindi Vijijini lakini sasa inajulikana kama Halmashauri ya Mtama katika Mkoa wa Lindi, Tanzania.

Katika sensa ya mwaka 2022 wakazi walihesabiwa 11,920 [1]. Wakati wa sensa iliyofanyika mwaka wa 2012, kata ilikuwa na wakazi wapatao 9,835. [2] walioishi humo.

Msimbo wa posta ni 65216.

Mazingira[hariri | hariri chanzo]

Nyangao imezungukwa na mito mikubwa miwili ambayo inatiririsha maji kwa vipindi vyote vya mwaka. Upande wa Kaskazini wa Nyangao unapendezeshwa na maji ya mto Lukuledi, maji ambayo yanatumika kwa shughuli za kilimo.

Kadhalika upande wa Kusini wa Nyangao upo mto mwingine uliobeba jina na ardhi mama ya Nyangao, mto Nyangao, mto murua kabisa unaopita chini ya miti iliyokuzwa vema na Uoto asilia mwingi.

Vijiji[hariri | hariri chanzo]

Kata ya Nyangao inaundwa na maeneo kama Nyangao A, Nyangao B, Mtakuja, Cheleweni, Kilimahewa, Chocholo, Mahiwa na Litingi.

Makao makuu ya kata hii yapo Nyangao B, sehemu ambayo kuna ofisi zote kwa ngazi ya kata.

Kata ya Nyangao, hususani makao makuu yake, ni kati ya sehemu inayokua kwa kasi kubwa katika halmashauri ya Mtama.

Ndipo mahali ilipo Hospitali kubwa ya Mtakatifu Walburga ambayo ilirithiwa toka kwa wamisionari wa Kanisa Katoliki, na sasa ipo chini ya Jimbo Katoliki la Lindi. Uwepo wa hospitali hiyo imekuwa msaada sana kwa wakazi wa Nyangao na maeneo mengine ya jirani kwenye upatikanaji wa huduma bora za afya. Nyangao ni sahihi kusema haina changamoto kubwa ya huduma ya afya.

Asili ya wakazi[hariri | hariri chanzo]

Kwa asili wenyeji wa Nyangao ni watu wa kabila la Wamwera ambalo ni kabila kubwa linalopatikana mkoani Lindi, lakini shughuli za kijamii mbalimbali zimepelekea kuwepo kwa watu wa kabila la Wamakonde ambao kijiografia ni majirani na jamii ya watu wa Nyangao.

Yapo pia karibu kila kabila linalopatikana katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hatua hii inafanya Nyangao kuwa kati ya sehemu chache katika mkoa wa Lindi ambazo zinakuwa kwa kasi kubwa.

Shughuli za wakazi[hariri | hariri chanzo]

Ni dhahiri kuwa asilimia kubwa ya wakazi wa Nyangao ni wakulima, zaidi wakitumia jembe la mkono na wachache sana wenye kuweza kutumia nyenzo nyingine za kisasa. Kilimo kama cha mpunga, mahindi na mtama hustawi vema kiasi maeneo hayo. Hiki kwao ni kilimo kwa jili ya chakula.

Kwa upande wa mazao ya biashara wakazi wa Nyangao wameweka nguvu zao nyingi kwenye kilimo cha zao la korosho, kilimo ambacho unaweza kukipatia jina la 'Southern Diamon': hakika ni almasi ya Kusini maana korosho imekuwa mwokozi wa maisha ya watu wengi kwenye mikoa ya Lindi na Mtwara.

Kati ya mazao makuu ya biashara ya eneo hilo kuna zao la ufuta pia. Kijiografia ya kilimo nchini ni dhahiri ufuta hulimwa kwa wingi katika eneo la mkoa wa Lindi, hivyo hakuna shaka kwa watu wa Nyangao kuwa sehemu ya jamii ya wakulima wa zao hilo ambalo ni la pili kwa ukubwa katika mikoa ya Tanzania Kusini.

Elimu[hariri | hariri chanzo]

Kata ya Nyangao inajumuisha shule za msingi nne, zote zikiwa ni za serikali, na shule mbili tu za sekondari, moja ni binafsi.

Shule za Msingi ni: Nyangao (Vigaeni), Ng'awa, Mahiwa na Litingi.

Shule za Sekondari ni: Mahiwa High school (Serikali) na Nyangao High school (Binafsi)

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. https://www.nbs.go.tz/
  2. Sensa ya 2012, Lindi - Lindi DC. Jalada kutoka ya awali juu ya 2016-03-03. Iliwekwa mnamo 2016-06-22.
Kata za Wilaya ya Mtama - Tanzania

Chiponda | Kiwalala | Longa | Majengo | Mandwanga | Mnara | Mnolela | Mtama | Mtua | Mtumbya | Nachunyu | Nahukahuka | Namangale | Namupa | Navanga | Nyangamara | Nyangao | Nyengedi | Pangatena | Sudi


Makala hii kuhusu maeneo ya Mkoa wa Lindi bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Nyangao kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.
Tafadhali usiingize majina ya maafisa au viongozi wa sasa maana wanabadilika mno.