Mbawakawa-duma

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mbawakawa-duma
Mbawakawa-duma mfalme (Chaetodera regalis
Mbawakawa-duma mfalme (Chaetodera regalis
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Arthropoda (Wanyama wenye miguu yenye viungo)
Nusufaila: Hexapoda (Wanyama wenye miguu sita)
Ngeli: Insecta (Wadudu)
Ngeli ya chini: Pterygota (Wadudu wenye mabawa)
Oda: Coleoptera (Wadudu wenye mabawa magumu)
Nusuoda: Adephaga
Familia ya juu: Caraboidea
Familia: Cicindelidae
Latreille, 1802
Ngazi za chini

Makabila 6, 3 katika Afrika ya Mashariki:

Mbawakawa-duma ni mbawakawa wa familia Cicindelidae katika nusuoda Adephaga ya oda Coleoptera wanaowinda wadudu wengine wakikimbia kwa kasi, kama duma. Kinyume na ndugu wao, mbawakawa wakimbiaji, huwinda wakati wa mchana. Wengi wana rangi zinazotokea mwanga wa jua. Kuna karibu na spishi 2900 duniani na karibu na spishi kati ya 200 na 300 katika Afrika ya Mashariki.

Maelezo[hariri | hariri chanzo]

Ukubwa wa mbawakawa hao ni wa kati wenye mfikio wa mm 7-70. Sifa bainifu ni macho makubwa yaliyobenuka, miguu mirefu na myembamba na mandibulo kubwa zilizopindika. Pronoto ni nyembamba kuliko mabawa ya mbele (elitra) yasipotumika. Pande za mabawa hao ni sambamba au mapana zaidi kidogo upande wa nyuma. Rangi za wadudu hao ni nyeusi, kahawia au kijani, mara nyingi wenye mabaka ya rangi kali. Pia wanaweza kuwa na rangi za mng'ao wa kimetali.

Buu la umbo la S ndani ya chimbo lake.

Mbawakawa-duma wanaweza kukimbia sana ili kukamata wadudu wengine. Spishi iliyo na kasi kubwa kabisa inayojulikana, Rivacindela hudsoni, inapiga mbio za km/h 9 au m/s 2,5, yaani 125 mara urefu wa mwili wake kwa sekunde.

Lava ni kama mabuu lakini wana umbo la S. Hukaa katika machimbo ya urefu hadi m 1. Wana nundu juu ya pingili ya tano ya fumbatio inayobeba kulabu mbili ambazo zinaanga buu ndani ya chimbo lake. Kichwa ni kikubwa chenye mandibulo kubwa.

Biolojia na ekolojia[hariri | hariri chanzo]

Kinyume na mbawakawa wakimbiaji mbawakawa-duma hukiakia mchana. Kwa kawaida wanawinda ardhini lakini kuna spishi za kitropiki zinazoishi juu ya miti. Wanapenda mahali za mchanga kama matuta ya mchanga, kingo za bahari na maziwa, na njia za mchanga. Hao ni mbuai kali wanaowinda wadudu wengine. Hukimbia mbio sana ili kukamata mbuawa wao. Huruka juu pia kwa urahisi na kipindi chao cha mwitikio ni mwepesi sana kama nzi.

Mabuu husubiri ndani ya machimbo yao mpaka mdudu akikaribia. Kisha wanatumia kulabu zao kunyoosha mwili haraka ili kutoka kwa chimbo kwa kiasi na kumkamata mbuawa.

Spishi zilizochaguliwa za Afrika ya Mashariki[hariri | hariri chanzo]

  • Bennigsenium horni
  • Chaetodera regalis
  • Cicindela alboguttata
  • Cicindela fimbriata
  • Cicindela flavosignata
  • Cylindera rectangularis
  • Dromica mauchii
  • Elliptica kolbeana
  • Lophyra neglecta
  • Manticora scabra
  • Megacephala regalis
  • Myriochila melancholica
  • Prothymidia angusticollis
  • Ropaloteres alluaudi

Picha[hariri | hariri chanzo]