Uenezi wa Kiswahili

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Waluguru ni jamii ya wazungumzaji wazuri wa Kiswahili nchini Tanzania pamoja na lugha yao asili, Kiluguru.

Kiswahili ni lugha ambayo ilikuwa ikitumiwa na wakazi wa maeneo ya pwani ya Afrika Mashariki hata kabla ya ukoloni. Lugha hii ilitumika katika kufanyia mawasiliano na ilitumika kuwaunganisha watu kwa kuwa waliweza kuelewana na kuongea kwa mshikamano wa watu wengi.

Uenezi wa Kiswahili nchini Tanzania[hariri | hariri chanzo]

Lugha ya Kiswahili iliweza kukua sana na kuenea katika nchi ya Tanzania kuliko Kenya na Uganda kutokana na sababu zifuatazo.

Kuteuliwa kwa lugha ya Kiswahili kuwa lugha ya taifa: baada ya kupata uhuru mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliteua lugha ya Kiswahili itumike kama lugha kuu.

Hii ilipelekea sana kuenea kwa lugha ya Kiswahili Tanzania kuliko nchi za Kenya na Uganda pamoja na kuanzisha vyama mbalimbali kama BAKITA, BAMITA na vingine ambavyo vilisaidia kukua kwa lugha ya Kiswahili kwa kuongeza misamiati ambayo ilifanya lugha ya Kiswahili kuendelea kukua.

Vyombo vya habari kama vile televisheni, redio na hata magazeti ambavyo vilizungumza na kuchapisha majalada mbalimbali kwa kutumia lugha ya Kiswahili.

Kutumika kwa Kiswahili kama lugha ya kufundishia: lugha ya Kiswahili ilitumika kufundishia katika shule za msingi mpaka vyuoni kwa hiyo hili lilipelekea kuelea na kuenea kwa lugha ya Kiswahili Tanzania kuliko Kenya na Uganda.

Kukua na kuenea kwa lugha ya Kiswahili Tanzania kinaganaga zaidi[hariri | hariri chanzo]

Baada ya uhuru kuna mambo mengi yaliyosaidia kukua na kuenea kwa lugha ya Kiswahili Tanzania; miongoni mwa mambo hayo ni:

Kuteuliwa kwa lugha ya Kiswahili kuwa lugha ya taifa[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1967 serikali iliteua Kiswahili. Hatua hii imesaidia kukua kwa Kiswahili kwa njia mbalimbali kama vile:

  • kutumika katika shughuli zote za kiofisi
  • kuundwa kwa vyombo mbalimbali vya ukuzaji wa Kiswahili
  • kutumika katika shughuli zote za mawasiliano
  • kutumika katika kutolewa kwa elimu

Kuundwa kwa vyombo mbalimbali vya kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili[hariri | hariri chanzo]

Baada ya uhuru serikali iliunda vyombo katika kukuza na kuenea kwa lugha ya Kiswahili: vyombo hivyo ni TUKI, BAKITA, TAKILUKI na kadhalika.

Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI); taasisi hii ilianzishwa tangu wakati wa mkoloni mnamo mwaka 1954. Kamati hii ikabadilishwa jina ikawa inajulikana kama Kamati ya Kiswahili ya Afrika Mashariki. Ulipofika mwaka 1964 kamati ikaingizwa katika chuo kikuu kishiriki cha Dar es Salaam chini ya chuo kikuu cha Afrika Mashariki ikawa inajulikana kama chuo cha uchunguzi wa lugha ya Kiswahili.

Aidha mnamo mwaka 1970 kilipoanzishwa chuo kikuu cha Dar es Salaam kwa sheria ya bunge chuo hiki kilikuwa mojawapo ya asasi ya utafiti ya chuo hicho kikajulikana kama Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.

Mnamo mwaka 2009 taasisi hiyo ilibadilishiwa jina baada ya kuungana na idara ya Kiswahili chuo kikuu cha Dar es Salaam na kujulikana kwa jina la Taasisi za Taaluma za Kiswahili (TATAKI) ikawa imejiongezea dhima nyingine ya kufundisha taaluma mbalimbali za Kiswahili.

Dhima hizo ni:

  • kufanya utafiti wa kuiendeleza na kuikuza lugha ya Kiswahili
  • kuendeleza uchapishaji wa jarida la Kiswahili
  • kutoa machapisho mengine yatakayoonekana kuwa na manufaa
  • kukusanya taarifa zote za sasa zilizopo ulimwenguni
  • kufanya miradi ya utafiti ya muda mrefu
  • kutafsiri maandishi yafanyayo katika Kiswahili

Vyombo vya habari[hariri | hariri chanzo]

Tangu kupata uhuru hadi hivi sasa kumekuwepo na ongezeko kubwa la vyombo vya habari nchini. Vyombo hivi ni kama:

  • magazeti: kuna magazeti mengi yanayochapishwa kwa lugha ya Kiswahili; mfano wa magazeti hayo ni Uhuru, Mzalendo, Mwananchi, Nipashe, Mtanzania na kadhalika. Magazeti yanayochapishwa kwa lugha ya Kiswahili yamekuza Kiswahili kwa njia kuu mbili:
    • mfumo wake wa kuchapisha habari kwa kutumia Kiswahili
    • kuwa na safu maalumu zinazohusiana na taaluma ya Kiswahili, mathalani uhakiki wa vitabu, mashairi na hadithi. Kutokana na kusoma magazeti hayo watu wengi wameweza kukijua Kiswahili kuliko hapo awali
  • redio na televisheni; kumekuwa na ongezeko kubwa la vituo vya redio na televisheni baada ya uhuru. Kwa upande wa redio baadhi ya vituo hivyo ni TBC taifa, Redio one, Redio Free Afrika, Sauti ya Tanzania Zanzibari na kwa televisheni kuna ITV na vinginevyo.

Uenezi wa Kiswahili na magazeti[hariri | hariri chanzo]

  • Daima - Tanzania, Zanzibar
  • Taifa Leo
  • Un Nuur
  • Jamvi ya Habari
  • Mwananchi
  • Habari Leo
  • Majira
  • Nipashe
  • Raia
  • Moja
  • Mwanahalisi
  • Upendo
  • Uhuru
  • Michezo
  • Maendeleo

Katika nchi nyingine[hariri | hariri chanzo]

Kenya imetangaza Kiswahili kuwa lugha ya taifa lakini inaendelea kutumia Kiingereza katika shughuli za serikali. Watu wa matabaka ya juu mara nyingi hupendelea kutumia Kiingereza wakiona ni lugha bora. Lakini tangu 1986 wanafunzi wote wanatakiwa kujifunza Kiswahili katika shule za sekondari. Tatizo mojawapo ni kuwepo wa makabila makubwa kama Wakikuyu au Waluo wenye wasemaji wengi sana katika eneo moja, hali isiyosaidia kujifunza lugha tofauti. Pia kaskazini na magharibi mwa Kenya wenyeji wengi si wasemaji wa lugha za Kibantu nao hawaoni Kiswahili ni lugha rahisi.

Uganda inatumia Kiswahili kama lugha ya polisi na jeshi, hali ambayo haikuongeza upendo wa Waganda kwa lugha kutokana na historia ya Uganda ya kuwa na vita na serikali za kijeshi. Lakini kinasikika pia kama lugha ya biashara masokoni. Pamoja na kwamba Waganda walikichukulia Kiswahili kama lugha ya kitumwa lakini pia lugha hii ilionekana kuwa na ustaarabu wa Kiarabu zaidi, yaani Uislamu. Lugha ya Kiswahili ilitumika katika kueneza dini hiyo.

Mashariki mwa Kongo Kiswahili kimeenea sana: ni moja kati ya lugha nne za kitaifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Kwenye visiwa vya Ngazija (Comoros) kuna lahaja mbalimbali za Kiswahili zinazotumika na wananchi.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya lugha bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Uenezi wa Kiswahili kama historia yake, uenezi au maendeleo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.