Mkoa wa Ujiji

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Mkoa wa Ujiji (DOA))
Mkoa wa Ujiji (XIII) katika Afrika ya Mashariki ya Kijerumani

Mkoa wa Ujiji (tahajia rasmi hadi mwaka 1918: Udjidji) ulikuwa mkoa mmojawapo kati ya mikoa 21 ya koloni la Afrika ya Mashariki ya Kijerumani (DOA, Deutsch Ostafrika) iliyokuwa mtangulizi wa nchi za Tanzania bara, Rwanda na Burundi za leo.

Eneo na mipaka[hariri | hariri chanzo]

Mkoa huo ulikuwa na eneo la kilomita za mraba 37,200. Eneo lake lililingana kimsingi na Mkoa wa Kigoma wa leo.

Makao makuu (kwa Kijerumani Bezirksamt) yalikuwepo pale Ujiji (Wajerumani waliandika "Udjidji") iliyokuwa kituo muhimu cha biashara kwenye Ziwa Tanganyika na mwisho wa njia ya misafara kuanzia bandari kama Bagamoyo, Pangani na Saadani zilizotazama Zanzibar hadi hapa.

Mkoa huu (XIII kwenye ramani) ulipakana na

Mawasiliano[hariri | hariri chanzo]

Ujiji ilikuwa na kituo cha posta kilichounganishwa na simu ya telegrafu kwenda Cape Town; hivyo iliwezekana kuwasiliana na Dar es Salaam kupitia Afrika Kusini na Zanzibar. Boma la Ujiji lilikuwa kambi ya kombania 6 ya jeshi la Schutztruppe.

Ilhali bandari ya Ujiji haikuwa nzuri, Wajerumani walianzisha bandari mpya kwenye hori ya Kigoma kilomita 8 upande wa kaskazini. Bandari hiyo ilikuwa kituo cha mwisho cha reli ya kati kutoka Dar es Salaam iliyofika hapa mwaka 1913.

Wakazi[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1913 kulikuwa na wakazi Waafrika 240,800 pamoja na Wazungu 172 na Wahindi au Waarabu 294.

Uchumi[hariri | hariri chanzo]

Takwimu ya Wajerumani ya mwaka 1913 ilihesabu walowezi Wazungu 4. Mjini Ujiji kulikuwa na kampuni 9 za Waarabu, 7 za Wahindi na 2 za Wazungu.

Wenyeji Waafrika walikuwa na ng'ombe 95,700 na mifugo wadogo kama mbuzi na kondoo waliokadiriwa kuwa milioni 1.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]