Motokaa

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Magari)
Ford Mondeo ni motokaa ndogo ya kubeba abiria wachache, kwa mfano familia ndogo.
Magari kama Toyota Landcruiser hujengwa juu ya fremu ya lori dogo kwa kusudi la kubeba watu kwenye njia mbaya.

Motokaa (kutoka Kiingereza "motor car"[1], mara nyingi huitwa tu gari kutoka neno la Kihindi) ni chombo cha usafiri ambacho kwa kawaida kinakwenda kwenye nchi kavu kikitumia nguvu ya injini au mota yake. Hata hivyo ziko zinazoweza kusafiri pia majini, na kwa sasa kampuni kadhaa duniani zinafanya utafiti wa kutengeneza motokaa ambazo zitakuwa zikiruka angani.

Kuna aina nyingi za motokaa: magari madogo hubeba abiria tu na gari dogo la kawaida hubeba dereva pamoja na abiria hadi wanne. Magari makubwa kidogo hubeba hadi watu 8.

Mengine ya kubeba abiria ni mabasi ambayo ni pia aina ya motokaa lakini mara nyingi hutajwa kama kundi la pekee, sawa na malori ambayo ni motokaa kubwa za kubeba mizigo. Kuna kila aina ya mchanganyiko kati ya aina hizi.

Fremu ya motokaa pamoja na magurudumu, bila injini wala bodi.

Muundo[hariri | hariri chanzo]

Motokaa huwa na injini (mota) inayosukuma magurudumu kupitia giaboksi. Injini pamoja na magurudumu na bodi hushikwa na fremu ya gari. Magari madogo ya kisasa huwa na bodi inayojibeba yenyewe bila fremu ya pekee. Motokaa nyingi huwa na magurudumu manne lakini magari mazito sana kama lori au basi mara nyingi huwa na magurudumu ya ziada.

Dereva hutumia mitambo ya kutawala motokaa ambayo ni hasa:

  • usukani wa kuongoza mwendo na mwelekeo wa gari
  • kichapuzi cha kutawala mbio au kasi yake
  • breki inayosimamisha chombo
  • mara nyingi pia mkono wa kubadilisha gia

Mitambo ya lazima kwa usalama wa gari ni taa zake za nje mbele na nyuma, kiashirio au indiketa ya kuonyesha nia ya kubadilisha mwelekeo, kifuto au waipa inayosafisha kioo cha mbele wakati wa mvua.

Magari ya kisasa huwa na mitambo mengi mengine kama redio, vyombo vya muziki, kiyoyozi, siku hizi pia kompyuta ndogo ya kusimamisha injini au kuonyesha ramani ya njia pamoja na kutoa maelezo kuhusu njia kwa dereva kwa kutumia sauti iliyorekodiwa.

Injini kwa kawaida hupata nguvu yake kwa kuchoma petroli, diseli au gesi. Motokaa za kwanza zilitumia pia nguvu ya mvuke. Motokaa za kisasa kabisa zinatumia pia injini ya umeme.

Historia ya motokaa[hariri | hariri chanzo]

Kwa karne nyingi watu walitumia magari yaliyovutwa na wanyama kwa mfano farasi, punda au maksai. Waroma wa kale walifanya majaribio na magari yaliyosukumwa na watumwa. Maendeleo ya uhandisi yalisababisha majaribio ya kutengeneza magari yaliyosogezwa kwa nguvu ya upepo yakitumia tanga kuanzia mwaka 1600 huko Uholanzi.

Injini za mvuke[hariri | hariri chanzo]

Baada ya kugunduliwa kwa injini ya mvuke nguvu yake ilitumiwa pia kwa vyombo vya usafiri. Kutokana na uzito wa injini pamoja na magari yaliyoweza kuvumilia uzito mkubwa wa injini pamoja na maji na kuni iliyohitajika kuchemsha maji vyombo hivi havikufaa barabara za kawaida vikatumia njia ya reli za chuma. Nusu ya pili ya karne ya 19 iliona maendeleao ya kutengenezwa kwa motokaa za mvuke madogo yaliyotembea barabara za kawaida katika nchi za Ulaya na Marekani.

Injini za umeme[hariri | hariri chanzo]

Sehemu ya pili ya karne ya 19 iliona pia magari yaliyoendeshwa kwa nguvu ya umeme. Magari haya yana faida nyingi; muundo wa gari ni rahisi zaidi kwa sababu haihitaji giaboksi wala gia na gari halina makelele pia hautoi harufu baya ya eksozi. Lakini magari haya yalikuwa na tatizo ya kwamba yalitegemea kupata nishati kwa njia ya beteri nzito zilizochukua muda mrefu kuchajiwa. Hata hivyo hadi mwanzo wa karne ya 20 magari ya umeme yalikuwa mengi katika miji mikubwa.

Basi ya umeme mjini San Francisco inapokea nishati kupitia waya juu ya barabara inapopita

Mwaka 1900 asilimia 40 za motokaa zote nchini Marekani zilikuwa na injini za mvuke, 38 % za umeme na 22% za petroli. Mjini New York nusu ya motokaa zote zilikuwa na injini ya umeme.

Baadaye magari ya petroli yalisogea mbele kwa sababu yaliweza kutembea mbali kwa kujaza mafuta kuliko magari ya umeme kwa beteri zao. Pia beteri zilichukua masaa mengi hadi kujazwa upya wakati mafuta hujazwa mara moja.

Katika nchi kadhaa mabasi ya umeme yameendelea kutumiwa katika miji mikubwa yakipokea nishati si kwa beteri bali kwa nyaya za umeme zinazopangwa juu ya barabara ambako basi inapita.

Katika karne ya 21 teknolojia ya beteri ilisogea mbele kutokana na upanuzi wa matumzi ya simu za mkononi. Beteri ziliendelea kuwa ndogo zaidi na pia kushika umeme kwa muda mrefu zaidi. Maendeleo haya yametumiwa kwa kubuni motokaa mpya za umeme. (tazama chini)

Injini za mwako ndani (petroli na diseli)[hariri | hariri chanzo]

Injini mwako ndani imekuwa hadi leo njia kuu ya kusogeza magari na kwa kawaida tukiongelea motokaa tunamaanisha gari lenye injini mwako ndani inayochoma petroli au diseli.

Motokaa ya kwanza ya Benz ya 1885

Katika karne ya 19 wahandisi mbalimbali walianza kutengeneza injini za mwako wa ndani zilizochoma gesi au petroli ndani yake. Injini ya kwanza iliyofaulu kuanzia 1876 na kutengenezwa kwa wingi ilikuwa ni ile ya Mjerumani Nikolaus Otto aliyeshirikiana na Gottlieb Daimler na Wilhelm Maybach. Ilikuwa na mapigo manne petroli ikichomwa kwa msaada wa mwasho wa umeme na hadi leo sehemu kubwa ya injini zote inafuata kielelezo wa Otto. 1879 Karl Benz alitengeneza injini ya mapigo mawili kwa mfano wa Otto akaitumia kwa gari lake na tangu 1885 akatoa aina ya kwanza ya motokaa yenye magurudumu matatu iliyoendelea kujengwa mfululizo yaani kibiashara.

Maendeleo ya motokaa zilizotumia injini mwako ndani yalikuwa haraka. Mwanzoni yalikuwa na matatizo mengi hasa uhaba wa petroli. Benz alinunua mafuta kwa gari lake kwenye duka la dawa.

Mwaka 1892 mhandisi Mjerumani Rudolf Diesel alitunga injini inayochoma mafuta kwa kuikandamiza vikali na kutumia joto la hewa ndani ya injini kutokana na mshtuko wa kukandamizwa. Mashine hizi zina uwezo kutumia aina mbalimbali za mafuta na ile ya kawaida ilikuwa nzito kuliko petroli ikaitwa "diseli". Injini za diseli zamani hazikupendwa kwa magari madogo kutokana na sauti kubwa zaidi ya injini lakini zikawa kawaida kwa malori, mabasi na injini za meli kwa sababu zinatumia mafuta kidogo kuliko injini za petroli.

Gari la Ford T ya 1926

Ushindi wa motokaa[hariri | hariri chanzo]

Mwanzoni motokaa zilikuwa ghali sana zikanunuliwa na matajiri pekee. Mwaka 1914 mhandisi wa Marikani Henry Ford alianza kutengeneza gari lake la "Ford Model T" kiwandani akitumia mbinu mpya; aligawa matengenezo ya gari kwa hatua mbalimbali zilizotekelezwa na wafanyakazi walioshughulika hatua moja-moja tu. Mbinu huu ulisababisha utekelezaji wa haraka kwa sababu kila mfanyakazi alikuwa na shughuli chache zu alizojua kwa undani kabisa akiwa na vifaa na vipuri vyote pale alipofanya kazi bila kupotezy muda. Kwa njia hii Ford aliweza kutengeneza magari mengi tena kwa bei nafuu na hata watu wenye mapato ya wastani waliweza kununua gari hili. Mfanyakazi wa Ford aliweza kununua gari kwa mshahara wa miezi minne. Kwa jumla magari milioni 15 ya Ford T yalitengenezwa hadi 1927.

Wengine waliiga mfano wa Ford na motokaa zilizidi kupanua. Baada ya vita kuu ya pili ya dunia polepole katika nchi nyingi za Ulaya, Amerika na Asia motokaa ilikuwa njia ya kawaida ya usafiri kwa watu wengi.

Upanuzi wa usafiri wa motokaa ulibadilisha tabia nyingi za nchi zilizoathiriwa nao. Miji ilibadilika kwa kutengeneza barabara pana za kupokea magari mengi. Watu walianza kuishi mbali na mahali pa kazi kwa sababu usafiri ulikuwa rahisi na haraka. Njaa ya petroli na diseli iliendelea kuzidi na nchi zenye akiba za mafuta ya petroli zilitajirika kwa mfano nchi za Uarabuni, Norwei au Venezuela.

Mielekeo mipya[hariri | hariri chanzo]

Tangu miaka ya 1970 kuzidi kwa motokaa kulileta pia matizo mapya:

  • machafuko kwa mazingira kwa kelele na hewa chafu ya eksozi. Machafuko haya yalionekana kusababisha magonjwa kama kansa pia kuleta uharibifu kwa machafuko kwa hewa. Matokeo yake yalikuwa mvua asidi inayohatarisha mimea pamoja na misitu, wanyama ndani ya maziwa na pia kuharibu majengo hasa majengo ya kihistoria.
  • kupanda kwa bei ya petroli tangu vita ya Oktoba 1973 kati ya Waarabu na Israeli. Ilionekana mara ya kwanza ya kwamba nchi zenye mafuta zina uwezo wa kusumbua uchumi wa nchi wateja kwa kusimamisha utengenezaji.
  • hofu ya kuishi kwa mafuta ya petroli baada ya Klabu ya Roma kutoa taarifa yake ya kwanza iliyoeleza ya kwamba malighafi yote duniani yana mwisho na yatakwisha siku moja.

Jibu la wahandisi lilikuwa majaribio ya kuboresha injini zisizotumia mafuta. Ni hasa teknolojia mbili zilizoendelea kushughulikiwa:

  • injini ya gesi
  • injini ya umeme

Kwa jumla magari ya umeme bado hutegemea mbinu za kubeba nishati njiani kwa beteri. Siku hizi ni hasa injini za umeme zinazopokea jitihada nyingi. Tatizo hadi leo ni uzito, uwezo na gharama za beteri. Hata kama zimeshaboreka sana bado chaji ya beteri inaruhusu safari ya kilomita 50-100 tu. Kuchajiwa upya kunachukua masaa. Kuna mawazo ya kuunda mfumo wa vituo vya beteri ambako beteri zingebadilishwa sawa na vituo vya mafuta vya leo.

Mwelekeo tofauti ni majaribio ya kutengeneza umeme njiani. Hapa kuna njia mbili hasa:

  • Daimler-Benz na makampuni mengine yametengeneza magari yenye teknolojia mpya ya seli ya fueli inayotumia haidrojeni. Lakini hadi sasa nguvu yake haitoshi kwa magari ya kawaida. Utafiti unaendelea.
  • hasa makampuni ya Japani yameshafaulu kutoa na kuuza magari chotara yanaounganisha injini ya umeme na injini ya petroli. Gari linaanza safari kwa nguvu ya beteri; beteri ikikwisha injini ya mafuta inawaka na kujaza betri.

Ya kuangazia unaponunua motokaa[hariri | hariri chanzo]

Haya ndiyo mambo ya kuangazi kabla ya kununua gari lako likiwa jipya au hata la zamani.

Usiwe na pupa[hariri | hariri chanzo]

Usiwe mwenye pupa wa kununua gari kabla ya kufanya utafiti ili ulijue gari lile zuri kabisa na ambalo litadumu kwa muda mrefu. Ukifanya utafiti wako kwa mitandao, kwa vitabu au marafiki walio na lile gari, basi utafanya uamuzi mwema wenye busara.

Jaribu kuliendesha gari[hariri | hariri chanzo]

Ni vizuri uliendeshe gari kabla ya kulinunua. Hili huitwa kwa Kiingereza "test drive" na muuzaji atakuruhusu kufanya hivi

Kuwa na makanika wako[hariri | hariri chanzo]

Huenda ukalinunua gari lililozeeka na kwa maana wewe ni mgeni katika kununua magari, ni vizuri uliangalie na makanika ambaye atakupa mashauri.

Nunua gari utakalomudu[hariri | hariri chanzo]

Ni vizuri uangalie gari ambalo wewe mwenyewe utalimudu, isiwe kwamba ni gari linalohitaji mambo mengi yatakayokushinda.

Angalia bima ya gari[hariri | hariri chanzo]

Gharama ya bima ni jambo lingine la kuangazia unaponunua gari.

Nambari ya usajili[hariri | hariri chanzo]

Serikali zahitaji kwamba kila gari liwe na nambari ya usajili. Nambari hii pia yaweza kukusaidia kujua umri wa gari.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Maneno hayo yana asili katika lugha ya Kilatini; "car" kutoka Kilat. carrus = gari na "motor" kutoka Kilat. movere = sogeza, hamisha yaani "mhamishaji, msukumaji"

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mambo ya teknolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hiyo kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.