Anwar Sadat

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Anwar Sadat

Muhammad Anwar el-Sadat (kwa Kiarabu: محمد أنور السادات‎ muhammad anwar as-sadat25 Desemba 19186 Oktoba 1981) alikuwa Rais wa tatu wa Misri akihudumia kuanzia 15 Oktoba 1970 hadi kuuawa kwake na maafisa wa jeshi.

Sadat alikuwa mwanachama mwandamizi wa Harakati ya Maafisa Huru iliyompindua Mfalme Farouk wa Misri katika mapinduzi ya mwaka 1952. Baadaye alikuwa mshauri wa karibu wa Rais Gamal Abdel Nasser akihudumu mara mbili kama makamu wake, halafu baada ya kifo cha Nasser alichukua nafasi yake mwaka 1970.

Katika kipindi cha miaka 11 alipotawala alibadilisha mwelekeo wa taifa. Aliachana na misingi mingi ya kisiasa na ya kiuchumi ya mfumo wa Nasser. Alianzisha mfumo wa vyama vingi na kufungua uchumi kwa makampuni ya binafsi. Aliondoa Misri katika ushirikiano na Umoja wa Kisovyeti na kurudisha wasaidizi Warusi kwao.

Mwaka 1973 aliongoza Misri katika Vita ya Yom Kippur dhidi ya Israeli akafaulu kurudisha rasi ya Sinai kutoka utawala wa Israeli. Kufaulu hapo kulimfanya shujaa wa taifa akatumia heshima hii kwa majadiliano na Israeli na mkataba wa amani wa mwaka kati ya Misri na Israel. Mwaka 1977 Sadat alikuwa rais wa kwanza wa nchi ya Kiarabu aliyefika mwenyewe nchini Israel na kuhutubia bunge la Knesset.

Mwaka 1979 alifikia mkataba wa amani na Israeli. Mkataba huu ulimletea tuzo ya Nobel ya Amani pamoja na Menachim Begin wa Israel. Hapo Sadat alikuwa Mwislamu wa kwanza kupokea tuzo ya Nobel yoyote.

Ingawa Wamisri wengi walikubali mkataba wa amani, hasa kwa sababu ulirudisha Sinai kwa Misri, wengine walisikitika, hasa Jumuiya ya Ikhwan Muslimin waliokataa kabisa. Pia nchi nyingine za Kiarabu zinazounganishwa katika Jumuiya ya Nchi za Kiarabu -isipokuwa Sudan- zilikataa mkataba huo wa amani zikatenga Misri katika jumuiya hii hadi 1989. Sababu ilikuwa ya kwamba mkataba huo haukutaja suala la dola au nchi kwa Wapalestina waliokuwa wakimbizi tangu kufukuzwa kwao wakati wa kuundwa kwa Israel mwaka 1948.

Mkataba wa amani ulikuwa pia sababu ya kwamba kundi la wanajeshi wenye uhusiano na Ikhwan Muslimin walimwua Sadat tarehe 6 Oktoba 1981.

Aliyemfuata madarakani alikuwa makamu wake, Hosni Mubarak.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Kujisomea[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Wikiquote ina mkusanyiko wa dondoo kuhusu: