Aljeri

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Algiers)








Jiji la Aljeri

Nembo
Nchi Aljeria
Jimbo Jimbo la Aljeri

Aljeri (Kiarabu: مدينة الجزائر, madīnat al-djazā'ir, "mji wa visiwa"; Kifaransa: Alger) ni mji mkuu pia mji mkubwa kabisa wa nchi ya Aljeria ikiwa na wakazi milioni 2 (mwaka 2005), pamoja na mitaa ya nje takriban milioni 5. Iko mwambaoni mwa bahari ya Mediteranea.

Aljeri ni makao ya serikali na kitovu cha uchumi, biashara, utamaduni na mawasiliano nchini.

Kasbah yake imeorodheshwa na UNESCO kama Urithi wa Dunia.

Waingereza walivamia meli za maharamia Aljeri mnamo Agosti 1816.
Majengo ya nyakati za ukoloni.
Mtaa wa Aljeri mwambaoni.
Uwanja wa "Mashahidi wa Uhuru".
Algiers inavyoonekana kutoka angani.
Aljeri inavyoonekana kutoka angani.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Mji ulianzishwa kama koloni la Wafinisia katika karne ya 4 KK. Mahali palifaa kutokana na visiwa vinne vidogo vilivyokuwepo karibu na mwambao (lakini katika karne ya 17 BK viliunganishwa na bara).

Baada ya kuenea kwa Dola la Roma ikawa mji wa Icosium na kuvamiwa na Waarabu Waislamu mwaka 702. Waberber wa kabila la Beni Mezghenna walikaa katika eneo hili. Mwaka 960 kiongozi wa Kiberber Buluggin ibn Ziri aliyekuwa gavana wa makhalifa wa Fatimiya wa Misri aliteua mahali pa Icosium na kujenga boma hapa. Mji uliitwa sasa "Al-djazair-Mezghenna" yaani "visiwa vya Beni Mezghenna". Ndiyo asili ya jina la leo "Al djaza'ir (الجزائر)" yaani "visiwa".

Katika karne zilizofuata mji ulivamiwa na watawala Wamurabitun na Wamuwahidun kutoka Moroko. Baadaye ukawa chini ya masultani wa Aljeria ya Kaskazini.

Mnamo mwaka 1302 Uhispania ilifaulu kushika visiwa vidogo mwambaoni kwa miaka kadhaa hadi kufukuzwa tena na mharamia Barbarossa aliyeteka mji kwa niaba ya Sultani wa Uturuki.

Tangu karne ya 16 BK Aljeri ikawa mji wa kujitawala ndani ya Dola la Uturuki. Imekuwa mara kwa mara makao makuu ya maharamia wa Mediteranea ya magharibi. Maharamia hao walishambulia jahazi za Wakristo kama Waitalia, Wafaransa, Wahispania na kadhalika na kuteka abiria pamoja na mabaharia. Waliuzwa kama watumwa au kurudishwa kwao baada ya kulipiwa pesa. Maharamia waliweza pia kushambulia miji ya Wakristo mwambaoni mwa Mediteranea na kutwaa wakazi kama watumwa. Hali hiyo ilisababisha tena na tena majaribio ya nchi za Ulaya kuvamia Aljeri lakini bila kufaulu hadi karne ya 19.

Mwaka 1815 Marekani ilishambulia Aljeri baada ya kupotea meli na raia kwa maharamia wa mji; mwaka 1816 Waingereza pamoja na Waholanzi walishambulia tena kwa kusudi la kulinda meli na raia zao. Walifaulu kumlazimisha mtawala wa Aljeri atie sahihi mkataba wa kutochukua tena watumwa kutoka nchi za Ulaya ingawa biashara hii iliendelea kwa siri hata baadaye.

Mwaka 1830 Wafaransa walivamia mji na kuanzisha utawala uliokuwa mwanzo wa ukoloni wa Kifaransa katika Aljeria.

Wafaransa walipanua na kubadilisha mji wa Kiarabu na Kiberber. Katika karne ya 19 Wafaransa wengi walihamia Aljeria hadi Aljeri ilikuwa mji mwenye wakazi wengi Wafaransa kuliko wenyeji waliokaa hasa katika mji wa kale ulioitwa "Kasbah". Wafaransa waliozaliwa Aljeria walijiita "pieds noir" (miguu myeusi).

Wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia Aljeria ilikuwa chini ya serikali ya Kifaransa katika maeneo yasiyovamiwa na Ujerumani hadi kuingiliwa na wanajeshi Wamarekani na Waingereza mwaka 1942. Baadaye ikawa mji mkuu wa "Ufaransa Huru" hadi mwisho wa vita.

Tangu uhuru wa Aljeria (1962) Aljeri imekuwa mji mkuu wa Aljeria. Akina pieds noir walio wengi waliondoka wakihofia uchungu baada ya vita vya ukombozi.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu maeneo ya Algeria bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Aljeri kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.