William Booth

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

William Booth (10 Aprili 1829 – 20 Agosti 1912) ni Mkristo aliyeanzisha Jeshi la Wokovu na kuwa mkurugenzi wake wa kwanza (1878 – 1912).

William Booth.

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Utoto na Ujana[hariri | hariri chanzo]

Booth alizaliwa katika kijiji cha Sneiton, wilaya ya Nottingham, nchi ya Uingereza. Alikuwa mmoja wa watoto wanne, lakini mwana wa kiume wa pekee, wa Samuel Booth na Mary Moss. Baba yake alikuwa tajiri, lakini wakati wa utoto wa William, familia ilianza kuwa maskini.

Mwaka 1842 Samuel, ambaye wakati huo alikuwa amefilisika, hakuweza kulipa ada za shule kwa William aliyekuwa na umri wa miaka 13. Hivyo William alianza kuwa mwanagenzi wa mweka rahani. Kabla mwaka huo haujaisha, baba yake alifariki.

Wakati wa uanagenzi wake William aliingia Ukristo. Alianza kusoma vitabu vingi, kujifundisha kuandika na kutoa hotuba, na kuwa mhubiri mlei wa Kanisa la Metodisti.

Alipomaliza uanagenzi wake mwaka 1848, alijaribu kupata kazi nyingine kwa vile hakupenda kazi ya mweka rahani. Mwaka 1849 aliacha familia yake na kuhamia jiji la London ambapo alipata kazi katika duka la mweka rahani tena. Pia aliendelea na huduma ya mhubiri mlei lakini hakuridhika na nafasi alizozipata. Kwa hiyo aliacha kazi ya mhubiri mlei na kuanza huduma ya uinjilisti mitaani.

Mwaka 1851 alijiunga na Kanisa la Wesley, na tarehe 10 Aprili 1852, sikukuu yake ya kuzaliwa ya 23, aliacha kazi ya mweka rahani na kuwa mhubiri kwenye makao makuu yao kule Clapham. Baada ya wiki tano tu, alimchumbia Catherine Mumford.

Mwezi wa Novemba 1852, Booth alialikwa kuwa mchungaji wa kanisa kule Spalding, wilaya ya Lincolnshire.

Ndoa na watoto[hariri | hariri chanzo]

William Booth na Catherine Mumford walifunga ndoa tarehe 16 Juni 1855 katika kanisa la Stockwell Green kule London. Walikuwa na watoto wanane wafuatao:

Huduma yake ya kwanza[hariri | hariri chanzo]

Ingawa Booth alikuwa mwinjilisti hodari, hakufurahia uchungaji. Mkutano wa kila mwaka wa kanisa lake walipoendelea kumpa majukumu ya uchungaji na kumkatalia ombi lake la kufanya uinjilisti tu, alijiuzulu uchungaji wake mwaka 1861.

Kwa vile madhehebu yake hayakumruhusu kufanya uinjilisti ndani ya makanisa baada ya kujiuzulu kwake, akawa mwinjilisti aliyejitegemea. Hata hivyo, teolojia yake haikubadilika. Aliendelea kuhubiri kwamba wasiookoka watateswa milele, kwamba kila mtu anahitaji kutubu, na kwamba Mungu anatuwezesha kuwa watakatifu, yaani tukiishi maisha ya upendo kwa Mungu na wenzetu. Hatimaye, hata watoto wa Booth walishirikisha katika huduma yake.

Misheni ya Kikristo (‘’The Christian Mission’’)[hariri | hariri chanzo]

Mwaka wa 1865, Booth pamoja na mke wake walianzisha Shirika la Uamshaji la Kikristo (‘’Christian Revival Society’’)) katika eneo la East End la London. Waliendesha mikutano kila jioni na siku nzima ya Jumapili wakitoa huduma za toba, wokovu na maadili ya kikristo kwa fukara, pamoja na walevi, wahalifu na malaya. Jina la shirika lilibadilishwa baadaye kuwa Misheni ya Kikristo (‘’Christian Mission’’).

Booth na wanashirika wake walitenda walichohubiri, yaani waliishi maisha ya kikristo wakijitolea mhanga katika huduma kwa wengine. Kwa mfano, waligawa chakula kwa maskini bila kujali wakidharauliwa kwa ajili ya huduma zao za kikristo.

Jeshi la Wokovu[hariri | hariri chanzo]

Mwaka wa 1878, jina la shirika lilibadilishwa tena kuwa Jeshi la Wokovu. Kama majeshi mengine, lilipata bendera yake na nyimbo zake ambazo hufuata sauti za watu wa kawaida zikiunganishwa na maneno ya kikristo. Booth na wanajeshi wengine huvaa sare za jeshi la Mungu kwenye mikutano. Booth alianza kuitwa Jenerali, na watumishi wengine walipewa vyeo vya afisa vilivyofaa.

Ingawa walibanwa kifedha, Jeshi la Wokovu na huduma zake zilienea haraka na kuzalia matawi katika nchi nyingine, baadhi yao Marekani, Ufaransa, Uswisi, Sweden, Australia, Kanada, Uhindi, Afrika ya Kusini, New Zealand, Jamaika, na kadhalika.

Wakati wa maisha yake, William Booth alianzisha huduma za Jeshi la Wokovu katika nchi 58 akisafiri sana na kuendesha mikutano. Booth alitoa jarida na kuandika vitabu kadhaa. Pia alitunga nyimbo nyingi. Kitabu chake maarufu kabisa ni In Darkest England and the Way Out kilichotolewa mwaka wa 1890.

Miaka ya mwisho[hariri | hariri chanzo]

Hatimaye huduma za Jeshi la Wokovu na za William Booth ziliheshimiwa hadharani.

Mwishoni mwa maisha yake, Booth alipokewa na wafalme na marais.

Hata vyombo vya habari walimwita Jenerali kwa kumheshimu.

William Booth aliaga dunia akiwa amefikisha umri wa miaka 83.

Alizikwa kwenye Abney Park Cemetery ambapo na mke wake alikuwa amezikwa.

Ili kumheshimu Booth, mshairi Vachel Lindsay aliandika shairi liitwalo General William Booth Enters Into Heaven, na Charles Ives aliyekuwa jirani wa Booth alitunga sauti kwa shairi hilo.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]