Sisimizi mfumaji

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Sisimizi mfumaji
Sisimizi mfumaji mwekundu
Sisimizi mfumaji mwekundu
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Arthropodi (Wanyama wenye miguu yenye viungo)
Nusufaila: Hexapoda (Wanyama wenye miguu sita)
Ngeli: Insecta (Wadudu)
Nusungeli: Pterygota (Wadudu wenye mabawa)
Oda: Hymenoptera (Wadudu wenye mabavu angavu)
Nusuoda: Apocrita (Hymenoptera wenye kiuno chembamba sana)
Familia ya juu: Formicoidea (Hymenoptera kama siafu)
Familia: Formicidae (Sisimizi)
Nusufamilia: Formicinae
Jenasi: Oecophyllus
F. Smith, 1860
Ngazi za chini

Spishi 2, 1 katika Afrika ya Mashariki:

Sisimizi wafumaji ni spishi kubwa kiasi za jenasi Oecophylla katika familia Formicidae ya oda Hymenoptera ambao hujenga makoloni yao kwenye miti wakiunganisha majani kwa hariri na kufuma nyando kati yao. Kuna spishi moja katika Afrika kusini kwa Sahara (sisimizi mfumaji nyekundu) na spishi moja katika Asia ya Kusini-Mashariki (sisimizi mfiumaji kijani).

Maendelo[hariri | hariri chanzo]

Sisimizi hao ni kubwa kiasi. Malkia wana urefu wa mm 15-25, spishi ya Afrika kwa upande mdogo na spishi ya Asia kwa ukubwa zaidi. Ukubwa wao pia unategemea wingi na ubora wa chakula. Wafanyakazi wakubwa wana urefu wa mm 8-10 na wafanyakazi wadogo takriban nusu ya hii. Vipapasio vina pingili 12 na pingili ya kwanza ni ndefu kuliko zile za pili na tatu pamoja. Wana mandibulo kubwa zenye umbo la pembetatu na kulabu iliyopinduka kuelekea ndani. Toraksi imefunika kwa nywele nyororo na fumbatio kwa nywele wima. Katikati ni kiuno chembamba na kirefu. Kuna pedi ya kufyonza kati ya kulabu za kila tarsi ili kuwawezesha sisimizi kushikamana na nyuso. Tofauti kuu kati ya spishi ni rangi. Sisimizi wafumaji wekundu ni kahawiamachungwa hadi kahawia iliyokolea. Malkia wa sisimizi wafumaji kijani ni kijani na kahawia iliyofifia, lakini wafanyakazi ni kahawianjano hadi kahawiamachungwa, ingawa wale huko Australia wana fumbatio kijani na kichwa vilevile mara nyingi.

==Biolojia na ekolojia

Makazi ya sisimizi wafumaji wekundu

Kama sisimizi wote hao ni wadudu wa kijamii na huishi katika makoloni lakini yale ya sisismizi wafumaji yapo kati ya majani ya miti. Makazi hutengenezwa kwa kuunganisha majani kwa hariri inayokalidiwa na lava. Makazi yanaweza kuwa mengi kwenye miti kadhaa. Kwa kawaida kuna malkia moja tu. Wafanyakazi ni wa ngeli mbili za ukubwa, wakubwa (majors) na wadogo (minors). Wadogo hukaa ndani au karibu na makazi ambapo wanatunza lava na kuchunga wadudu wanaotoa mana. Wakubwa huenda kukamata mbuawa. Hutengeneza makazi pia na kuyalinda.

Sisimizi wafumaji ni wagomvi sana. Hawavumilii viumbehai vingine kwenye mti wao wa makazi. Ikiwa kiumbe hakikimbia, kinauawa na kuletwa kwenye makazi kizima au vipande vipande. Isipokuwa tu ni wadudu fulani ambao hutoa mana, kama vile wadudugamba, vidukari, vidung'ata na viwavi wa spishi kadhaa za vipepeo. Mana hukusanywa na wafanyakazi wadogo. Wakubwa wanalinda makazi na kutoa au kufukuza viumbehai. Ikiwa kuna koloni jingine karibu, wakubwa wa makoloni yote mawili huweka ukanda bila sisimizi. Wakubwa kuwinda ardhini pia na kukamata wadudu, invertebrata wengine na hata vertebrata wadogo.

Makazi hujengwa na wakubwa kwa kuvuta pamoja majani yaliyo karibu na kuyafunga kwa nyuzi za hariri zinazonata ambazo zimefumwa na lava wa hatua ya mwisho. Makazi haya yana umbo la duaradufu na urefu wa kati ya sm 25 na 50, ingawa kiota cha kwanza kabisa cha koloni kinachoanzia kinaweza kuwa jani moja tu lililokunjwa. Katika kipindi cha maendeleo yake sisimizi hukuza koloni kwa kuongeza idadi ya makazi, hata kuhamia miti iliyo karibu. Mwishowe lina maelfu mengi ya sisimizi.

Sisimizi wafumaji na binadamu[hariri | hariri chanzo]

Sisimizi hao wanaweza kuumia sana, kwa sababu waking'ata hutia asidi ya sisimizi (formic acid). Hata hivyo wakuzaji wa miti ya matunda huwatumia kuzuia wadudu wasumbufu fulani. K.m. katika Tanzania wakuzaji wa minazi wanawatumia dhidi ya kunguni wa mnazi. Wanatumika pia dhidi ya nzi-matunda, k.m. huko Benin.

Spishi[hariri | hariri chanzo]

  • Oecophylla longinoda (Sisimizi mfumaji mwekundu)
  • Oecophylla smaragdina (Sisimizi mfumaji kijani)

Picha[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]