Msumbiji (kisiwa)

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kanisa la Mt. Antonio
Daraja la Kisiwa cha Msumbiji linalounganisha kisiwa na bara

Kisiwa cha Msumbiji (kwa lugha ya Kireno: "Ilha de Moçambique") ni kisiwa kidogo (na pia mji) kilichopo km 3 mbele ya mwambao wa Msumbiji ya kaskazini. Urefu ni km 3 na upana kati ya m 500 hadi 200. Kisiwa ni sehemu ya mkoa wa Nampula.

Kisiwa kilikuwa chanzo cha koloni la Kireno la Msumbiji na mji ulikuwa mji mkuu wa nchi kwa karne kadhaa hadi mwaka 1898 BK. Leo hii mji umepanuka kote kisiwani. Kuna wakazi 60,000 wanaoishi katika mji wenye sehemu mbili: mji wa mawe upande wa kaskazini na mji wa makuti upande wa kusini.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Habari za kwanza za Kisiwa cha Msubiji zimetokana na Wareno. Alipofika Vasco da Gama mwaka mwaka 1498 BK kisiwa kilikuwa na mji wa Waswahili na Waarabu kikiwa kituo muhimu cha biashara ya kimataifa katika Bahari Hindi.

Mwaka 1507 Wareno walijenga kituo cha kijeshi. Jengo la kale kisiwani ni kanisa dogo la Nossa Senhora de Baluarte lililojengwa mwaka 1522 BK.

Tangu mwaka 1558 hadi 1620 Wareno walijenga boma kubwa la Mtakatifu Sebastiano kwa gharama kubwa. Mawe yote yalichukuliwa kwa meli kutoka Ureno, Goa (Uhindi) na pia pwani ya Msumbiji yenyewe. Umuhimu wa Msumbiji machoni pa Wareno ulikuwa nafasi ya kituo chenye usalama cha safari ndefu kati ya Ureno na Bara Hindi.

Kisiwa kilikua kituo kikuu cha Wareno katika Afrika ya mashariki hasa baada ya kupotea Boma la Yesu huko Mombasa. Waholanzi na Wafaransa walishambulia kisiwa lakini walishindwa kuteka boma lenyewe.

Mwanzoni Msumbiji ilitawaliwa kama sehemu ya Uhindi ya Kireno kutoka mji mkuu wa Goa. Mwaka 1720 Msumbiji ilipata kuwa kama jimbo la pekee na kisiwa cha Msumbiji kikawa mji mkuu. Kisiwa kilikuwa bandari muhimu katika biashara ya watumwa kwa visiwa vya Bahari Hindi na pia hadi Brazil ya Kireno.

Mwaka 1898 mji mkuu ulihamishwa kwenda Lourenco Marques (leo Maputo). Kisiwa kilianza kurudi nyuma.

Katika miaka ya 1960 daraja lilijengwa kati ya kisiwa na bara. Idadi ya watu kisiwani imezidi kukua. Walio wengi wanaishi bila maji wala choo. Nafasi ya kila mtu ni 27,6 pekee.

Urithi wa dunia[hariri | hariri chanzo]

Kabla ya kuhamishwa kwa mji mkuu kisiwa kilikuwa makao ya Gavana Mkuu wa Msumbiji, wa askofu, wa balozi za nchi kadhaa na wafanyabiashara kutoka India, Ujerumani, Uswisi, Ufaransa na Uingereza. Mabaki yao ni majengo ya kihistoria ambayo ni mfano wa pekee wa mji wa kikoloni hasa kwa sababu ujenzi mpya haukutokea baada ya kuondoka kwa makao ya serikali.

UNESCO imeandikisha mji wa mawe katika orodha ya Urithi wa Dunia.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu maeneo ya Msumbiji bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Msumbiji (kisiwa) kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.