Lugha ya kidini

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Maandishi ya Kisanskrit yaliyo ya zamani kuliko yote yaliyobaki hadi leo: Devi Māhātmya, juu ya jani la mtende, Bihar au Nepal, karne ya 11.

Lugha ya kidini ni lugha inayotumiwa pekee katika maisha ya kidini kama vile kwa shughuli za liturujia, sala au maandiko matakatifu, wakati wasemaji au wasomaji wa lugha hii ya kidini hutumia lugha nyingine katika maisha ya kawaida.

Lugha za kale kama lugha za kidini[hariri | hariri chanzo]

Mara nyingi lugha za kidini ni lugha za kale zinazohifadhiwa katika maisha ya kidini lakini katika maisha ya kawaida zimeshabadilika sana.

Kilatini[hariri | hariri chanzo]

Hadi mwaka 1964 ibada karibu zote za Kanisa Katoliki duniani kote ziliendesha kwa lugha ya Kilatini. Mtaguso wa Pili wa Vatikani ulibadilisha utaratibu huo na kupendelea lugha za watu wenyewe zitumike katika ibada. Hata hivyo hadi leo kuna misa na ibada za Kilatini katika makanisa machachechache na monasteri za nchi mbalimbali.

Kislavoni cha Kanisani[hariri | hariri chanzo]

Katika Makanisa ya Kiorthodoksi ya Bulgaria, Poland, Serbia na Urusi liturujia za ibada ni kwa lugha ya Kislavoni cha Kanisani. Lugha hiyo inatunza hali ya Kislavoni ya miaka 1000 iliyopita kilichogeuka baadaye kuwa lugha mbalimbali za kisasa.

Asili ni kazi ya watakatifu Methodio na Kyrilo wa Saloniki waliotafsiri vitabu vya Ukristo kwa ajili ya misheni kati ya Waslavoni. Walitumia lugha ya kawaida ya wakati ule mnamo mwaka 800 BK lakini lahaja mbalimbali za Kislavoni zimeendelea kubadilika hadi lugha mpya za Kislavoni zimetokea kama vile Kirusi, Kibulgaria n.k.

Tangu karne nyingi hakuna mtu anayetumia tena kile Kislavoni cha kale kwa maisha ya kila siku, lakini inaendelea kuwa lugha ya ibada na liturujia katika Makanisa ya Kiorthodoksi ya mataifa ya Kislavoni kama vile Warusi, Wabulgaria, au Waserbia.

Kisanskrit[hariri | hariri chanzo]

Kisanskrit kilikuwa lugha ya Waaria walioingia Uhindi takriban miaka 1,500 KK kikawa pia lugha ya kuandika maandiko matakatifu ya Ubanyani. Kisanskrit hufundishwa hadi leo lakini lugha za leo zimekuwa tofauti kabisa.

Lugha za kidini zisizotumiwa tena katika maisha ya kila siku[hariri | hariri chanzo]

Lugha za kidini zinazoendelea kuzungumzwa au zilizo karibu na lugha hai[hariri | hariri chanzo]

Kuna pia lugha hai zinazotumiwa kama lugha za kidini nje ya eneo wanapokaa wasemaji wao. Mara nyingi hata katika lugha hizi za kidini maneno na matamshi yasiyo ya kawaida tena hutunzwa.

Kiarabu na Uislamu[hariri | hariri chanzo]

Mfano wake mkuu ni Kiarabu kama lugha ya kidini kati ya Waislamu. Waislamu walio wengi kabisa hawajui Kiarabu. Wasemaji wa Kiarabu ni takriban 20% za Waislamu wote. Kuna Waislamu wengi kidogo waliojifunza viwango mbalimbali vya Kiarabu, kwanza kwa kurudia maneno ya sala na kutaka kujua zaidi. Hata hivyo idadi kubwa ya Waislamu duniani hawajui Kiarabu ila maneno yanayorudiwa mara kwa mara.

Pamoja na hayo Kiarabu cha Qurani na cha sala ni lugha isiyotumiwa tena na watu katika maisha ya kila siku. Hata sehemu kubwa ya Waarabu wanaelewa kisehemu tu. Sarufi ya Kiarabu sanifu cha kimaandishi cha leo ni bado kilekile kama lugha ya Qurani, lakini msamiati umebadilika mno na pia sarufi ya lugha inayozungumzwa.

Mifano ya Kiingereza na Kijerumani[hariri | hariri chanzo]

Kwa lugha za Ulaya kama Kiingereza na Kijerumani kuna tafsiri za Biblia zilizoandikwa takriban miaka 400 - 500 iliyopita. Makanisa mengine yanatunza hali hii ya lugha kwa masomo ya Biblia au pia sala kanisani. Hapa maneno ya karne zilizopita yasiyo ya kawaida tena katika maisha ya kila siku bado yanatunzwa. Kwa Kiingereza ni hasa tafsiri ya Mfalme Yakobo (King James) na kwa Kijerumani ni tafsiri ya Martin Luther.

Tabia hizi zinaonekana katika lugha na tamaduni nyingi.