George Weah

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
George Weah mwaka 2019.

George Weah (alizaliwa Monrovia, 1 Oktoba 1966) ni rais wa Liberia kuanzia mwaka 2017. Kabla ya kuwa mwanasiasa aliwahi kuwa mwanakandanda mashuhuri duniani.

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Utoto, familia na kabila[hariri | hariri chanzo]

Weah ni wa kabila la Kru ambalo linatoka upande wa kusini-mashariki mwa Liberia kwenye Kaunti ya Grand Kru, ambayo ni moja ya maeneo maskini sana nchini humo.

Wazazi wake walikuwa William T. Weah, Sr. na Anna Quayeweah. Alilelewa zaidi na bibi yake upande wa baba, Emma Klonjlaleh Brown.

Weah alikulia jijini Monrovia katika kitongoji cha maskini cha Clara.

Alihudhuria shule ya msingi katika shule ya Muslim Congress and sekondari katika shule ya Wells Hairston High School.

Weah amemuoa Clar Weah, mwenye asili ya Visiwa vya Karibi. Wana watoto watatu: George Weah Jr, Tita na Timothy. Huyo, baada ya majaribio na timu ya Chelsea mwaka 2013, alijiunga na timu ya Paris Saint-Germain mwaka 2015. Timothy anaichezea pia timu ya taifa ya Marekani ya chini ya umri wa miaka 18. Binamu yake Weah, Christopher Wreh aliwahi pia kucheza soka la kulipwa kwenye timu ya Arsenal.

Weah aliwahi kubadili dini toka Ukristo kwenda Uislamu na baadaye akarudi tena kwenye Ukristo. Hivi sasa ni muumini wa Ukristo wa Kiprotestanti.

Elimu[hariri | hariri chanzo]

Kielimu, Weah ana Shahada ya Kwanza ya Uendeshaji Michezo toka Chuo Kikuu cha Parkwood, London, Uingereza. Hata hivyo baadhi ya watu wanatilia shaka shahada hii kwakuwa chuo hiki kinajulikana kwa kutoka shahada bila kusoma hapo. baadaye alipata shahada ya Usimamizi wa Biashara toa Chuo Kikuu cha DeVry, Miami nchini Marekani. Mwaka 1999 alipata shahada ya Udakitari ya Heshima toka Chuo Kikuu cha A.M.E Zion nchini Liberia.

Katika soka[hariri | hariri chanzo]

Kabla ya kujiunga na soka la kulipwa, Weah alikuwa akifanya kazi katika Shirika la Mawasiliano la Liberia kama fundi simu.

Mwaka 1995 Weah alipewa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) tuzo ya kuwa Mwanasoka Bora Duniani. Yeye ni mwanasoka pekee toka Afrika aliyewahi kupewa tuzo hiyo. Mwaka huohuo alichaguliwa pia kuwa Mwanasoka Bora Ulaya na Mwanasoka Bora Afrika. Miaka 1989, 1994 na 1995 alichaguliwa kuwa Mwanasoka Bora wa Mwaka Afrika na mwaka 1996 alichaguliwa kuwa Mwanasoka Bora wa Karne wa Afrika. Mwaka 2004, Pelé alimchagua kwenye orodha ya FIFA ya wachezaji bora ambao wako hai.

Weah alianza safari yake ya soka katika timu Incincible Eleven ya Liberia na Tonnerre Yaounde ya Cameroon. Baada ya hapo alikwenda kucheza soka la kulipwa Ulaya mwaka 1988. Alijiunga na timu ya Monaco ambayo ilikuwa ikifundishwa na Arsène Wenger ambapo aliiongoza kushinda kombe la Ufaransa mwaka 1991. Baadaye alijiunga na Paris Saint Germain mwaka 1992-95. Aliiongoza timu hii kuchukua kombe la ligi ya Ufaransa mwaka 1994. Akiwa hapo aliweza kuwa mfungaji bora wa Ligi ya Mabingwa wa Ulaya (UEFA Champions League) mwaka 1994–95. Mwaka 1995-2000 alikuwa akiichezea timu ya AC Milan ambayo ilishinda ligi ya Italia mwaka 1996 na 1999. Mwaka 2000 aliondoka AC Milan na kujiunga na Chelsea, baada ya muda mfupi alijiunga na Manchester City na baadaye Marseille mwaka 2001. Alimaliza soka la kulipwa akiwa na timu ya Al JAzira ya Falme ya Nchi za Kiarabu. Kwa ujumla alicheza soka la kulipwa kwa miaka 14.

Weah aliichezea pia timu ya taifa ya Liberia na aliiwakilisha nchi yake katika Kombe la Mataifa ya Afrika mara mbili.

Weah amekuwa akitoa misaada kwa wananchi wa Liberia. Mwaka 2004 alipewa Tuzo ya Ujasiri ya Arthur Ashe kwa juhudi zake za kusaidia kujenga nchi yake.

Katika siasa[hariri | hariri chanzo]

Kwenye uchaguzi wa urais mwaka 2005, Weah alishindwa kwenye raundi ya pili na rais wa kwanza mwanamke Afrika, Ellen Johnson Sirleaf. Uchaguzi uliofuata mwa mwaka 2011, Weah alipigania kiti cha umakamu wa rais kama mgombea mwenza wa Winston Tubman. Mwaka 2014, Weah alishinda kiti cha useneti kupitia chama cha Congress for Democratic Change kwenye Kaunti ya Montserrado.

Mwaka 2017 alishinda uchaguzi wa urais wa Liberia. Aliongoza kwa kura nyingi katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 10 2017. Hata hivyo, alishindwa kupata asilimia zaidi ya asilimia 50. Kwenye raundi ya pili ya uchaguzi hapo 25 Desemba 2017 alimshinda Joseph Boakai aliyekuwa makamu wa rais aliyetangulia Ellen Johnson Sirleaf. Weah alipata asilimia 61.5 za kura.[1].

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Ex-soccer star 'King George' Weah wins Liberia's presidency, tovuti ya uk.reuters.com ya tar 28 Desemba 2017, iliangaliwa 5 Januari 2018

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu George Weah kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.