Maria kupalizwa mbinguni
Maria kupalizwa mbinguni ni sikukuu ya Kanisa Katoliki inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 15 Agosti. Inatokana na dogma iliyotangazwa na Papa Pius XII kwa hati Munificentissimus Deus ya tarehe 1 Novemba 1950 baada ya kusikiliza maoni ya maaskofu wote.
Fundisho hilo la imani ni kwamba Bikira Maria, mama wa Yesu, alipomaliza maisha yake duniani alichukuliwa mwili na roho mbinguni, ashiriki mapema utukufu wa Mwanae mfufuka kama alivyoshirikiana naye toka mwanzo hata mwisho wa maisha yake.
Fundisho hilo linalingana na lile la Waorthodoksi, ingawa hao hawajalitangaza kuwa dogma. Tarehe hiyo wao wanaadhimisha ya Kulala kwa Bikira Maria.
Umoja wa msimamo huo upande wa mashariki na wa magharibi wa Kanisa unatokana na mapokeo ya karne za kwanza za Ukristo, yanayoshuhudiwa na mababu wa Kanisa kama vile Efrem wa Syria, Timoteo wa Yerusalemu, Epifanio wa Salamina, Yohane wa Damasko.