Jawaharlal Nehru

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Jawaharlal Nehru (1949)

Jawaharlal Nehru (14 Novemba 1889 - 27 Mei 1964) alikuwa waziri mkuu na kiongozi wa kwanza wa Uhindi ya kisasa. Alitawala miaka 17 tangu uhuru wa mwaka 1947 hadi 1964.

Maisha ya binafsi[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa mjini Allahabad (jimbo la Uttar Pradesh) katika familia ya Brahmin kutoka Kashmir. Baba yake, wakili Motilal Nehru, alikuwa kati ya viongozi wa kwanza wa chama cha Indian National Congress.

Kijana Jawaharlal alipewa elimu kufuatana na mtindo wa magharibi na shule ya sekondari alisoma Uingereza. Akaendelea kusoma biolojia kwenye chuo kikuu cha Cambridge halafu sheria huko London.

Baada ya kurudi Uhindi alimwoa Kamala Kaul aliyemzalia mtoto wake pekee, Indira Priyadarshini. Indira alimfuata baadaye kuwa waziri mkuu wa Uhindi na baada yake mjukuu wake Nehru, Rajiv Gandhi. Katika miaka ya mwisho ya utawala wa Kiingereza Nehru alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Edwina Mountbatten, mke wa mfalme mdogo Louis Mountbatten.

Kazi na siasa[hariri | hariri chanzo]

Baada ya kumaliza masomo yake huko London alikubaliwa kuwa wakili na mwaka 1917 alirudi Uhindi alipokuwa karani yake Mahatma Gandhi. Kwa njia hiyo Motilal Nehru na Gandhi walijuana na Ghandi alijiunga na chama cha Congress.

Mwaka 1922 alikamatwa mara ya kwanza na serikali ya kikoloni ya Kiingereza na katika miaka iliyofuata alirudi gerezani mara nyingi. Tangu mwaka 1929 alikuwa kiongozi wa Congress pamoja na Gandhi akawa mwenyekiti wake kuanzia mwaka 1930.

Katika serikali ya muda iliyoandaa uhuru alihudumia kama makamu wa rais. Siku ya 15 Agosti 1947 ilipoleta uhuru, Nehru akawa waziri mkuu na kiongozi wa kisiasa wa Uhindi wote na muda huohuo waziri wa mambo ya nje. Nehru alishindwa kuzuia ugawaji wa Uhindi ulioleta nchi mbili za pekee za Uhindi na Pakistan.

Waziri Mkuu[hariri | hariri chanzo]

Nehru alirudishwa mwaka 1952 katika uchaguzi huru wa kwanza wa nchi hiyo. Alirudishwa mara mbili, miaka 1957 na 1962 akafariki akiwa madarakani.

Nehru alijenga uhusiano mwema na makoloni mengi ya awali yaliyopata uhuru katika miaka ya 1950 na 1960. Katika mazingira ya vita baridi alianzisha harakati ya kutofungamana na Marekani wala Umoja wa Kisovyeti akakusanya mataifa mapya mengi katika ushirikiano huo.

Ndani ya Uhindi aliunda uchumi wenye tabia za kijamaa kwa sekta ya viwanda. Alimaliza mabaki ya utawala wa kikabaila wa maraja na utawala wa kikoloni katika maeneo madogo ya Goa na Pondicherry yaliyokuwa yamebaki chini ya Ureno na Ufaransa.

Mwishoni mwa utawala wake aliona vita ya China na Uhindi iliyomlazimisha kutumia silaha alizozichukia.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu: