Filamu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mcheza filamu za kuchekesha Chaplin
Alama mojawapo ya Filamu
Mwandaaji wa filamu nchini Tanzania

Filamu (kutoka Kiingereza film, pia movie au motion pictures) ni mfululizo wa picha zinazoonyesha mwendo wa watu au vitu na kuonekana na watazamaji kwenye skrini.

Ni aina ya mawasiliano yanayotumiwa kutolea hadithi au kuwaelezea watu kuhusiana na kujifunza fikra au mitazamo mipya katika jamii.

Watu katika kila pembe ya dunia huwa wanaangalia filamu ambazo zinaelezea hadithi fulani ikiwa kama kiburudisho, au njia ya mojawapo ya upenzi.

Filamu nyingi zinatengenezwa ili kuonyeshwa katika makumbi makubwa ya video au sinema.

Historia

Misingi ya kuona mwendo kwa njia ya filamu

Msingi wa filamu ni mbinu wa kushika mwendo fulani kwa picha nyingi. Kila picha peke yake inaonyesha tu hali fulani bila mwendo. Lakini jicho la binadamu likiona picha zaidi ya 15 kwa sekunde haliwezi kuona tofauti kati ya picha hizo mojamoja, hivyo linaanza kuona mwendo mfululizo. Kwa hiyo lazima kuwa na kamera inayopiga angalau picha 15 au zaidi kwa sekunde ili kupata filamu itakayoonekana kama mwendo halisi. Idadi ya picha 24 kwa sekunde ilikuwa wastani wa kawaida kwa muda mrefu.

Filamu za kwanza zilikuwa bila sauti lakini kuanzia miaka ya 1920 teknolojia ya kutoa sauti pamoja na picha ilianza kupatikana.

Filamu za kuchorwa zilitumia misingi ileile yaani wachoraji walipaswa kugawa mwendo katika picha zilizopigwa mojamoja na kuonyeshwa mfululizo.

Siku hizi sehemu kubwa za filamu hutengenezwa kwa kompyuta.

Filamu namna inavyotengenezwa

Mwandikaji muswada (screenwriter), anaandika muswada huo utakaotumika katika filamu na waigizaji watafuata muswada andishi huo. Kisha mtayarishaji anakodi watu watakaoshiriki na kuandaa pesa zote zitakazohitajika kuwalipa waigizaji na vyombo vya utenegezaji wa filamu. Mara nyingi atamtafuta pia mwongozaji lakini wakati mwingine mtayarishaji na mwongozaji ni mtu yeye yule.

Mtayarishaji mara nyingi hupata hela za kufanyia kazi hiyo kwa kupitia mikopo ya benki au wawekezaji watakaomsaidia kumkopesha fedha kwa ajili ya matayarisho ya filamu hiyo. Kuna baadhi ya watayarishaji wanaofanya kazi katika studio za utengenezaji wa filamu, na kuna wengine hujitegemea (hawafanyi kazi katika studio za utayarishaji wa filamu).

Mwongozaji na waigizaji husoma muswada andishi ili kufahamu ni nini cha kusema na ni nini cha kufanya. Waigizaji wanahifadhi maneno watakayosema wakati wa kuigiza filamu, na kujifunza matendo ambayo muswada andishi ulivyowaeleza vya kufanya. Kisha mwongozaji anaanza kuwaambia waigizaji nini cha kufanya na kumruhusu mpiga picha aanze kufanya vitu vyake kwa kutumia kamera ya kutengenezea filamu.

Mhariri wa filamu anaviunganisha vipande vya picha pamoja, na kuanza kuchagua vipande vitakavyofaa kwa wapenzi wa filamu. Mhandisi wa sauti na wataalamu wa kutengeneza vibwagizo vya filamu, hukusanyika pamoja na kuanza kuweka milio maalumu katika filamu hiyo.

Pindi filamu inapokamilika, nakala nyingi hutengenezwa na kusambazwa kupitia mikanda maalum kuhifadhia filamu na kuanza kuisambaza katika majumba ya sinema kwa ajili ya kuizindua na baadaye kuipeleka mauzoni.

Baadhi ya waigizaji maarufu

Wanaume

Wanawake

Waongozaji filamu maarufu

Viungo vya nje