Tofali bichi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Matofali mapya ya udongo, katika Bonde la Yordani, Ukingo wa Magharibi (2011)
Matofali mabichi yalitumika kwa ujenzi wa zigurati za Elamu ambazo ni kati ya majengo makubwa ya dunia ya kale. Choqa Zanbil ilitengenezwa karne ya 13 KK huko Iran kwa kutumia matofali mabichi pamoja na matofali ya kuchomwa. [1]

Tofali bichi ni tofali lililokaushwa hewani bila kulichoma. Matofali ya udongo yanajulikana tangu mwaka 9000 KK hivi [2] ingawa tangu 4000 KK matofali yalichomwa pia kuongeza nguvu na uimara. Ila tu katika mazingira yenye mvua kidogo matofali mabichi hutumiwa hadi leo.

Utengenezaji[hariri | hariri chanzo]

Hutengenezwa kwa kutumia udongo mzito kiasi pamoja na maji; mara nyingi huchanganywa na ubua unaolifanya kuwa imara zaidi.

Matope yanayotokea yanaweza kupewa umbo maalumu kwa mkono. Nyumba ndogo zinaweza kujengwa kwa kuweka udongo uliopewa umbo kwa mkono mahali pake bila kuukausha kwanza. Ukuta wa aina hiyo hujengwa polepole ili sehemu ya chini ya ukuta ipate nafasi ya kukauka kiasi hadi tabaka jipya linaongezwa juu yake.

Vinginevyo vipande vya udongo hupokea maumbo tofauti, mara mviringo, mara silinda, mara kimstatili na kuwekwa chini ili vikauke. [3]

Mbinu inayoruhusu kuharakisha kazi ni matumizi ya kalibu yanayoleta pia matofali ya ukubwa wa pamoja.

Wakati mwingine yametumiwa pamoja na matofali ya kuchomwa kwa shabaha ya kupunguza gharama upande mmoja na kuongeza kinga dhidi ya mvua kwa upande mwingine. Njia nyingine ni kutumia lipu.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Msikiti Mkuu wa Djenné ni msikiti mashuhuri nchini Mali. Inataazamiwa kama jengo kubwa la matofali mabichi duniani.

Matumizi ya matofali mabichi yamepatikana tangu miaka elfu kadhaa. Mifano ya mapema ni nyumba mjini Yeriko zilizojengwa miaka 9,000 iliyopita. Inaonekana kwamba tekinolojia hiyo imetambuliwa katika maeneo mbalimbali ya Dunia kwa kujitegemea, kama vile Mashariki ya Kati, Afrika, Amerika na China.

Pamoja na matofali mabichi kuna pia maeneo ambako nyumba zimetengenezwa kwa kutumia udongo moja kwa moja. Afrika ya Kaskazini ni maarufu kwa nyumba zake za udongo uliokandamizwa tabaka kwa tabaka.

Adobe[hariri | hariri chanzo]

Katika maeneo yaliyoshawishiwa na Hispania, ujenzi wa matofali mabichi huitwa adobe.

Piramidi ya Jua huko Teotihuacan nchini Meksiko na hekalu la Huaca del Sol huko Peru hutajwa kama majengo makubwa za adobe katika mabara ya Amerika.

Nyumba za kisasa zinajengwa Texas, Marekani kwa kutumia matofali mabichi uliosongolewa

Matumizi ya kisasa[hariri | hariri chanzo]

Mahali pengi duniani matofali mabichi yanaendelea kutumiwa, hasa katika tabianchi yabisi (pasipo mvua nyingi) na pale ambako kuni au fueli ya kuchomea ni haba.

Katika miaka ya nyuma nyumba zinajengwa tena pia Marekani na Ulaya kwa kutumia matofali mabichi yasiyochomwa[4]

Wakati mwingine mitambo ya kusongolea udongo hutumiwa, pamoja na kuongeza saruji kidogo kwenye udongo mbichi. (linganisha en:compressed earth block).

Picha[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Roman Ghirshman, La ziggourat de Tchoga-Zanbil (Susiane), Comptes-rendus des séances de l'Académie des Inscriptions et Belles-Lettres, vol. 98 lien Issue 2, pp. 233–238, 1954
  2. Rosenberg, Danny; Love, Serena; Hubbard, Emily; Klimscha, Florian (2020-01-22). "7,200 years old constructions and mudbrick technology: The evidence from Tel Tsaf, Jordan Valley, Israel". PLOS ONE (kwa Kiingereza) 15 (1): e0227288. Bibcode:2020PLoSO..1527288R. ISSN 1932-6203. PMC 6975557 Check |pmc= value (help). PMID 31968007 Check |pmid= value (help). doi:10.1371/journal.pone.0227288. 
  3. Labelle Prussin: Building Technologies in the West African Savannah[dead link], In: 2000 ans d’histoire africaine. Le sol, la parole et l’écrit. Mélanges en hommage à Raymond Mauny. Tome I. Paris : Société française d'histoire d'outre-mer, 1981. pp. 227-245. (Bibliothèque d'histoire d'outre-mer. Études, 5-6-1);
  4. Linganisha kwa mfano Ujerumani

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Possehl, Gregory L. (1996). Mehrgarh katika Oxford Companion to Archaeology, iliyohaririwa na Brian Fagan. Chuo Kikuu cha Oxford Press.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya teknolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hiyo kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.