Rasi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Rasi ndogo.

Rasi (pia: peninsula, neno la Kiingereza lenye asili ya Kilatini na maana ya nusukisiwa) ni sehemu ya nchi inayoelekea katika maji ya bahari au ziwa na kuzungukwa na maji pande tatu. Ni kama kisiwa kinachounganishwa na bara upande mmoja tu.

Rasi inaweza kuwa ndogo au kubwa. Mifano ya rasi kubwa ni nchi za Italia na Korea au Bara Hindi.

Rasi kubwa barani Afrika ni Pembe ya Afrika.

Rasi ndogo zaidi mara nyingi zina umaarufu fulani kwa sababu zilikuwa alama muhimu kwa kutambua njia ya baharini zamani za usafiri kwa jahazi (meli za tanga). Mifano mashuhuri ni Rasi ya Tumaini Jema na Rasi Agulhas kwenye ncha ya kusini ya Afrika, Rasi Delgado iliyokuwa alama ya mpaka kati ya utawala wa kikoloni wa Wareno na Wajerumani katika Afrika ya Mashariki na hivyo hadi leo mwisho wa mpaka kati ya Msumbiji na Tanzania.

Rasi hizo ndogo ziliweza kuhofiwa na mabaharia wa jahazi kwa sababu mara nyingi mikondo ya maji ndani ya bahari iliathirika ghafla na rasi hizo na jahazi zilizosafiri karibu na pwani ziliweza kusukumwa kwenye miamba.