Mtaguso wa pili wa Laterano

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Basilika la Mtakatifu Yohane huko Laterano ambamo mtaguso ulifanyika.

Mtaguso wa pili wa Laterano, uliofanyika kuanzia tarehe 4 hadi 11 Aprili 1139 chini ya Papa Inosenti II (1130-1143), unahesabiwa na Kanisa Katoliki kuwa mtaguso mkuu wa kumi.

Ni wa pili kufanyika Magharibi, kwenye Kanisa kuu la Roma (Italia).

Historia[hariri | hariri chanzo]

Mtaguso ulihitajika kutokana na farakano lililotokea mwaka 1130 alipofariki Papa Honori II (1124-1130): hapo makardinali waligawanyika kuhusu Mapatano ya Worms, ambayo mwaka 1122 yalikuwa yamekomesha Mashindano kuhusu uteuzi wa maaskofu.

Isitoshe, kulikuwa na ushindani kati ya koo mbili za Roma, yaani Frangipane na Pierleoni.

Tarehe 14 Februari 1130, makardinali 16 waliosimama upande wa familia ya Frangipane walimchagua Gregorio Papareschi, aliyejiita Papa Inosenti II.

Saa chache baadaye, Pietro Pierleoni alichaguliwa na makardinali wengine na kujiita papa Anakleti II.

Hatimaye, kwa msaada wa Bernardo wa Clairvaux, Inosenti II alishinda na kukubaliwa na wengi, ingawa hakuweza kuhamia Roma mpaka baada ya mpinzani wake kufa (1138).

Mtaguso ulipaswa kurekebisha matokeo ya farakano hilo. Basi Inosenti II alifungua kikao na kuondoa madarakani maaskofu waliomfuata mpinzani wake.

Halafu papa alikusudia kuendeleza juhudi za urekebisho za Mtaguso wa kwanza wa Laterano. Hivyo zikapitishwa kanuni 30, ambazo nyingi kati yake zilikuwa za kurudia zile za zamani kuhusu usimoni, mapadri wenye wake n.k.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mtaguso wa pili wa Laterano kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.