Kutubu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kutubu (Alfa Ursae Minoris, Polaris)
Picha iliyounganishwa na picha 20 zilizopigwa kwa muda wa dakika 1.5 kutoka mahali palepale inaonyesha mwendo wa nyota angani zinazochora mistari kwenye picha. Nyota ya katikati haibadiliki ni Kutubu.
Kundinyota Dubu Mdogo (Ursa Minor)
Mwangaza unaonekana 1.98
Kundi la spektra Aa: F7 I Ab: F6 V B: F3 V
Paralaksi (mas) 7.54
Umbali (miakanuru) 323–433[1]
Mwangaza halisi Aa:: -3.6 Ab: 3.6 B: 3.1
Masi M☉ Aa:: 5.4 Ab: 1.26 B: 1.39
Nusukipenyo R☉ Aa:: 37.5 Ab: 1.04 B: 1.38
Mng’aro L☉ Aa:: 1260 Ab: 3 B: 3.9
Jotoridi usoni wa nyota (K) Aa:: 6015 Ab: ? B: 6900
Majina mbadala 1 Ursae Minoris, HR 424, BD +88° 8, HD 8890, SAO 308, FK5 907, GC 2243, ADS 1477, CCDM J02319+8915, HIP 11767

Kutubu (lat. & ing. Polaris au Pole Star, pia α Alfa Ursae Minoris, kifupi Alfa Umi, α Umi) ni nyota angavu zaidi katika kundinyota la Dubu Mdogo (Ursa Minor). Nyota hii iko karibu sana na nukta ya ncha ya kaskazini ya angani na kabla ya kupatikana kwa teknolojia ya kisasa ilikuwa nyota muhimu kwa ajili ya mabaharia waliotazama angakaskazi. Haionekani kwenye nusutufe ya kusini ya Dunia.

Jina[hariri | hariri chanzo]

Kutubu haionekani na watu wanoishi upande wa kusini wa ikweta inayokata pwani ya Uswahilini kati ya Lamu na Mogadishu. Hata hivyo, ilijulikana na mabaharia Waswahili tangu miaka mingi wakifuata njia yao baharini upande wa kaskazini wa ikweta wakati wa usiku kwa msaada wa nyota. [2]. Walipokea jina hilo kutoka kwa Waarabu wanaosema القطب al-qutub inayomaanisha „nyota ya ncha ya kaskazini".

Jina badala lilikuwa "nyota ya jaa" kwa maana ya "nyota ya kaskazini", ilhali "jaa" ilitaja pia mwelekeo wa kibla ya Waislamu[3].

Kwa matumizi ya kimataifa Umoja wa Kimataifa wa Astronomia ulikubali jina la Kilatini na kuorodhesha nyota hii kwa jina la "Polaris" [4].

Alfa Ursae Minoris ni jina la Bayer ikiwa ni nyota angavu zaidi katika Dubu Mdogo na Alfa ni herufi ya kwanza katika Alfabeti ya Kigiriki.

Tabia[hariri | hariri chanzo]

Kutubu iko kwa umbali wa miaka nuru takriban 323 - 433 kutoka Jua letu, tofauti ya namba inatokana na vipimo vinavyoofautiana hadi sasa bila kupata usuluhisho[5]. Mwangaza unaoonekana ni mag 1.98.

Kutubu ni nyota maradufu yenye sehemu tatu : nyota kuu inayojulikana kama α Umi Aa (au A1) inayozungukwa na msindikaji mdogo α Umi Ab (au A2) na hizi mbili zinazungukana na nyota ya tatu α Umi B kitovu cha graviti cha pamoja.

Kutubu ilitambuliwa kwenye mwaka 1780 na William Herschel kwa darubini kuwa nyota maradufu yaani mfumo wa nyota mbili za α Umi A na α Umi B. Wakati ule darubini ya Herschel ilikuwa kati ya vifaa bora duniani. Kwa kutumia Darubini ya Angani ya Hubble ilitambuliwa kwenye mwaka 2006 ya kwamba pia nyota ya A yenyewe ni nyota maradufu na sasa Polaris yote inajulikana kama mfumo wa nyota tatu zinazoitwa α Umi A1, α Umi A2 na α Umi B.

Nyota kuu ni Kutubu A1 (Polaris Aa) ambayo ni nyota badilifu yenye masi ya Jua mara 5 iking’ara mara 1200 kuliko Jua letu. Kutokana na mng’aro mkubwa inapangwa katika kundi la nyota jitu kuu . Mwangaza wa α Umi Aa ulibadilikabadilika kati ya mag 1.86 hadi 2.13 wakati wa kurekodiwa kama miaka 100 iliyopita. Baadaye kiwango hiki kilipungua kwa muda mrefu lakini kwa miaka ya nyuma kimeanza kuongezeka tena[6]

Kutubu kama Nyota ya Ncha ya Kaskazini[hariri | hariri chanzo]

Mtazamaji kwenye nusutufe ya kaskazini ya Dunia anaona nyota ya Kutubu inakaa mahali pake ilhali nyota zote zingine zinazunguka wakati wa usiku. Hali halisi inazunguka pia kidogo lakini haitambuliki na mtazamaji maana haiko kikamilifu kwenye ncha ya anga bali kwa umbali wa nyuzi 0,7°.

Katika kumbukumbu za kale si Kutubu iliyoangaliwa kuwa nyota ya kuonyesha mwelekeo wa kaskazini. Ptolemaio aliitaja kama « kwenye mkia wa Dubu Mdogo » [7] Miaka 2000 iliyopita nyota iliyokuwa karibu zaidi na ncha ya kaskazini ya anga ilikuwa Kochab (β Ursae Minoris ). Kutokana na kusogea kwa mhimili wa mzunguko (ing. en:precession) pia Kutubu imefika katika nafasi hii takriban miaka 400 iliyopita na bado inaendelea kukaribia hadi mwaka 2100; baadaye itaendelea polepole kusogea tena mbali na ncha ya kaskazini ya anga. Baada ya miaka 12,000, nyota ya Vega katika Kinubi itakuwa nyota ya ncha ya kaskazini jinsi ilivyowahi kuwa miaka 14,000 iliyopita.

Nyota za Ncha ya Kaskazini
mwaka Nyota kwenye nafasi ya „Nyota ya Ncha“
12000–11500 KK Vega (Alfa Lyrae)
7500 KK Tau Herculis
2900–2795 KK Thuban (Alfa Draconis)
ca. 1500 BK Yildun (Delta UMi)
2000 Kutubu (Alfa UMi)
4000 Errai (Gamma Cephei)
6800 Zeta Cephei
7500 Alderamin (Alfa Cephei)
10000–11000 takriban Dhanabu ya Dajaja (Alfa Cygni)
11400 Delta Cygni
14000 Vega
30000 takriban Dabarani
50000 Mizari (Dubu Mkubwa)

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Turner & alii (2013)
  2. ling. Knappert 1993
  3. linganisha kamusi ya Sacleux uk 178, "Dyaa, Dyaha, Dyahi"
  4. Naming Stars, tovuti ya Umoja wa Kimataifa wa Astronomia (Ukia), iliangaliwa Novemba 2017
  5. Turner & alii (2013)
  6. Lee & alii (2008)
  7. Toomer (1984), uk. 341

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Allen, Richard Hinckley: Star-Names and their Meanings; kwa G. E. Stechert New York, Leipzig, London, Paris 1899, ukurasa 437 (online kwenye archive.org)
  • Knappert, Jan: The Swahili Names of Stars, Planets and Constellations; The Indian Ocean Review September 1993 Volume 6 No. 3 September 1993, kurasa 6-7, ISSN 1031-2331
  • Lee, B. C.; Mkrtichian, D. E.; Han, I.; Park, M. G.; Kim, K. M. (2008). "Precise Radial Velocities of Polaris: Detection of Amplitude Growth". The Astronomical Journal. 135 (6): 2240 online hapa
  • Turner, D. G.; Kovtyukh, V. V.; Usenko, I. A.; Gorlova, N. I. (2013). "The Pulsation Mode of the Cepheid Polaris". The Astrophysical Journal Letters. 762: L8 online hapa
  • Ptolemy's Almagest, translated and annotated by G.J. Toomer, London 1984, ISBN 0-7156-1588-2 online hapa