Jumba la Maajabu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Jumba la Maajabu.

Jumba la Maajabu (kwa Kiarabu : Beit-al-Ajaib, بيت العجايب) ni jengo la kihistoria katika Mji Mkongwe, Zanzibar. Ni jengo kubwa na refu zaidi la Mji Mkongwe lililojengwa mnamo mwaka 1883 kwa amri ya Sultani Sayyid Bargash. Linatazama Bustani ya Forodhani kwenye ukingo wa bahari, karibu na boma la Wareno na ikulu ya zamani ya Sultani. [1] Jumba la Maajabu lilikuwa na Makumbusho ya Historia na Utamaduni wa Zanzibar hadi kufungwa kwa shughuli za matengenezo yaliyoanza mwaka 2019 kwa msaada kutoka Oman[2]. Tarehe 25 Desemba 2020 sehemu kubwa ya jengo iliporomoka.[3]

Historia[hariri | hariri chanzo]

Jumba la Maajabu mwanzoni mwa karne ya 20.

Jumba hilo lilijengwa mnamo mwaka 1883 kwa amri ya Barghash bin Said, Sultani wa pili wa Zanzibar. [4] [5] Ilikusudiwa kuwa jumba la sherehe na ukumbi rasmi wa mapokezi. Likapokea jina la "Nyumba ya Maajabu" kwa sababu ya kuwa jengo la kwanza huko Zanzibar kuwa na umeme na eleveta. [6] Ubunifu wa jumba hilo umetokana na mhandisi Mwingereza aliyeingiza staili mpya kama roshani pana zinazozunguka jengo lote na nguzo za chuma. Vinginevyo ujenzi ulitumia vifaa vya kawaida katika ujenzi wa Waswahili kama mawe ya matumbawe na boriti za mikoko.

Jumba liliathiriwa na kufyatuliwa na manowari za Waingereza tarehe 27 Agosti 1896 wakati wa Vita ya Uingereza dhidi Zanzibar. Lilikarabatiwa mwaka uliofuata na wakati ule lilipokea nyongeza ya mnara wenye saa kubwa. Wakati ule sultani alihamia hapa pamoja na maharimu wake.

Baada ya mapinduzi jengo hilo lilikuwa makao makuu ya Chama cha Afro-Shirazi na baadaye makumbusho. Lilipokelewa katika orodha ya Urithi wa Dunia ya UNESCOna kuwa kivutio cha watalii.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. "Independent Travel Guide to Zanzibar". www.zanzibar.org. Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2005-07-06. 
  2. https://www.omanobserver.om/oman-to-renovate-zanzibars-house-of-wonders/
  3. https://www.mwananchi.co.tz/mw/habari/kitaifa/jengo-la-kihistoria-beit-al-ajaib-laanguka-zanzibar-3239382
  4. "House of Wonders Museum". Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2012-11-16. 
  5. "The Zanzibar Stone Town Tour". Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 17 March 2018. Iliwekwa mnamo 22 November 2010.  Check date values in: |archivedate=, |accessdate= (help)
  6. "House of Wonders". Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2005-02-05. 

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]