Maktaba ya Aleksandria

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Maktaba jinsi ilivyokuwa zamani, kulingana na baadhi ya ushahidi wa kiakiolojia.

Maktaba ya Aleksandria ilikuwa maktaba kubwa na mashuhuri ya zama za kale. Ilianzishwa mjini Aleksandria katika Misri wakati wa utawala wa mfalme Ptolemaio I (305283/282 KK). Ptolemaio alikuwa jenerali Mgiriki chini ya Aleksanda Mkuu aliyeendelea kutawala Misri na kujitangaza kama mfalme. Alichagua Aleksandria kama mji mkuu mpya na kuupamba kwa majengo na taasisi nyingi.

Wakuu wa maktaba walikuwa wataalamu mashuhuri kama Eratosthenes ambao mara nyingi walikuwa pia walimu wa wana wa mfalme.

Maktaba ililenga kukusanya vitabu vyote vilivyopatikana. Serikali ya Misri iliagiza ya kwamba kila mgeni alipaswa kuonyesha vitabu na miandiko yake yote vichunguzwe na maafisa wa maktaba na kama havikuwemo bado vilinakiliwa haraka. Hata jahazi zilizoingia katika bandari zilitembelewa na maafisa wa maktaba na vitabu vyote kuchunguzwa kama lazima kukamatwa na kunakiliwa.

Mwanahistoria Mroma Aulus Gellius aliandika ya kwamba maktaba ilikuwa na vitabu 700,000 wakati wa Julius Caesar.

Vitabu vingi viliharibiwa wakati wa vita kati ya Caesar na Kleopatra.

Hakuna uhakika maktaba iliendelea kwa muda gani baada ya uharibifu huo.

Leo[hariri | hariri chanzo]

Bibliotheca Aleksandrina (maktaba) iliyoko Alexandria, Misri.
Picha ya nje ya Bibliotheca Aleksandrina.
Maktaba hiyohiyo.

Bibliotheca Alexandrina ni maktaba kuu na kituo cha kitamaduni kwenye mwambao wa Bahari ya Mediterania katika jiji la Aleksandria. Ni ukumbusho wa hiyo Maktaba ya Aleksandria, ambayo ilikuwa moja ya maktaba kubwa zaidi ulimwenguni ikapotea zamani.

Wazo la kufufua maktaba ya zamani lilianzia mwaka 1974, wakati kamati iliyoundwa na Chuo Kikuu cha Aleksandria ilichagua shamba kwa maktaba yake mpya. Kazi ya ujenzi ilianza mnamo 1995 na, baada ya dola milioni 220 kuwa zimetumika, jengo hilo lilizinduliwa rasmi tarehe 16 Oktoba 2002.

Mnamo 2010, maktaba ilipokea mchango wa vitabu 500,000 kutoka Bibliotheque nationale de France (BnF). Zawadi hiyo inafanya Bibliotheca Alexandrina kuwa maktaba ya sita kwa ukubwa duniani ya lugha ya Kifaransa.

Picha[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]