Glavu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Glavu za kingabaridi katika maonyesho

Glavu au glovu (kwa Kiingereza glove) ni kivazi kinachofunika mkono. Kazi yake ni hasa kukinga mkono dhidi ya athira za kudhuru kama baridi, joto, pembe kali au kemikali. Wakati mwingine kazi ya glavu ni pia kukinga mazingira dhidi ya athira inayotokana na mkono wenyewe.

Kama kila kivazi, glavu zinafuata fesheni na wakati mwingine huvaliwa kwa sababu za fesheni pekee.

Kimsingi glavu inafanana na soksi ya mguu. Hutengenezwa kwa kitambaa, ngozi au mpira na kwa kawaida huwa na nafasi kwa kila kidole.

Hakuna uhakika juu ya asili ya kivazi hiki. Uwezekano mkubwa ni kinga dhidi ya baridi. Mumia ya Otzi aliyekufa mnamo 3300 KK kwenye milima ya Alpi na mwili wake ulihifadhiwa katika barafu ilikuwa na glavu.

Baadaye glavu ziliendelea kupamba watu wa cheo. Katika kaburi la farao Tutankhamun († mnamo 1323 KK) glavu kadhaa zilikutwa.

Leo hii kuna aina nyingi tofauti za glavu

  • glavu za kinga dhidi ya baridi zinavaliwa na watu katika mazingira yenye baridi
  • glavu za kazi zinavaliwa na watu wanaobeba vitu venye nyuso kali na kukinga ngozi dhidi ya kukatwakatwa
  • glavu za raba hutumiwa na wauguzi wanaotaka kijikinga dhidi ya maambukizo
  • glavu za aina hii huvaliwa pia katika maabara kwa kujikinga dhidi ya kemikali, na kinyume kukinga vitu vinavyochunguliwa dhidi ya machafuko kutoka mkono
  • glavu za pekee kwa michezo mbalimbali kama vile glavu ya baseball, glavu ya bondia, glavu za madereva wa gari au baisikeli kwa mashindano