Gandunia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Tectonic plates (surfaces are preserved)

Gandunia (kutoka maneno "ganda" na "dunia"; en:plate tectonics) ni mafundisho ya sayansi za jiolojia na jiofizikia kuhusu tabia za ganda la dunia na miendo ya sehemu zake.

Muundo wa dunia[hariri | hariri chanzo]

Inaanza na hoja ya kuwa muundo wa dunia ni wa tabaka mbalimbali. Tabaka imara ni ganda la nje la dunia pamoja na sehemu ya juu ya koti ya dunia chini ya ganda hilo. Tabaka hiyo -inayoitwa "tabakamwamba"- inakaa juu ya tabaka moto na laini.

Ndani ya tabaka hilo laini kuna mwamba katika hali ya geli yaani ni kati ya hali imara na hali kiowevu. Kwa hiyo vipande vyake havikai mahali pamoja lakini vina mikondo ndani yake kufuatana na mikondo ya joto kali inayopanda juu kutoka kiini cha dunia ambacho ni chuma cha moto katika hali kiowevu.

Mikondo hii inasukuma tabakamwamba ya nje na kuivunjavunja katika vipande au mabamba mbalimbali.

Mikondo ya joto ndani ya dunia husababisha kutokea kwa miamba mipya kwenye migongo ya sakafu ya bahari na kuzama kwa kando ya mabamba ya kibahari chini ya mabamba ya kibara

Mwendo wa mabamba[hariri | hariri chanzo]

Kufuatana na nadharia ya gandunia, ganda la nje limevunjika na vipande vya ganda vyaitwa mabamba. Mabamba hayo yakaa juu ya koti moto kama majani yanayofunika maji katika sufuria inayopashwa moto. Maji ya moto huzunguka ndani ya sufuria na kusababisha majani usoni kutembea. Hivyo mabamba ya gandunia yana mwendo wakati wote.

Mwendo huo husababishwa na kupaa juu kwa magma (yaani mwamba moto wa kiowevu) inayotoka nje kwenye migongo iliyoko katikati ya sakafu ya bahari. Migongo hii ni safu ya milima ya kivolkeno chini ya maji, kwa mfano mgongo kati wa Atlantiki.

Magma hii inapoa kuwa mwamba mpya na kusukuma nusu mbili za bamba la kibahari kwenda nje. Pale ambapo bamba la kibahari linakutana na bamba la kibara linajisukuma chini yake kwa sababu miamba ya mabara ni myepesi na miamba ya bamba la kibahari ni zito zaidi. Hivyo pembizo la bamba la kibahari linazama chini na kuyeyuka katika joto la koti ya dunia. Eneo la kuzama chini linanonekana mara nyingi kama mfereji chini ya bahari.

Shindikizo hilo la sakafu ya bahari linasababisha pia mwendo wa bamba la kibara pamoja na kuvunjika kwa mabamba ya kibara.

Gandunia na uso wa dunia[hariri | hariri chanzo]

Miendo ya gandunia imeunda uso wa dunia jinsi ulivyo na jinsi unavyoendelea kutokea na kubadilika.

  • kugongana kwa mabamba husababisha kukunja kwa ganda la dunia na kutokea kwa safu za milima.
  • kuzama kwa pembizo la bamba moja chini ya bamba lingine husababisha kutokea kwa mifereji chini ya bahari na volkeno kwenye bamba la juu - au kutokea kwa nyororo ya visiwa vya kivolkeno kwenye mstari wa kuzama. Maeneo haya kuna mitetemeko ya ardhi mara kwa mara.
  • shindikizo ya gandunia husababisha pia kuvunjika kwa mabamba. Hali hii inaonekana kwa kutokea kwa mabonde ya ufa.
Makala hiyo kuhusu "Gandunia" inatumia neno ambalo si kawaida na matumizi yake ni jaribio kwa jambo linalotajwa.
Wasomaji wanaombwa kuchangia mawazo yao.

Kamusi za Kiswahili ama zinatofautiana kuhusu matumizi ya neno hili au hazieleweki au hazina neno kwa jambo linalojadiliwa.

Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Gandunia kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.