Nicolaus Copernicus

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Taswira ya Nicolaus Copernicus (mwanzo wa karne ya 16).

Nicolaus Copernicus (kwa Kijerumani Nikolas Koppernigk, kwa Kipolandi: Mikołaj Kopernik; 19 Februari 147324 Mei 1543) alikuwa padri wa Kanisa Katoliki na mtaalamu wa astronomia, tiba na hisabati.

Ni maarufu hasa kwa kuwa ndiye aliyeeleza muundo halisi wa ulimwengu kwa kusema dunia inazunguka jua, kinyume cha fundisho lililotawala awali kuwa jua linazunguka dunia. Ndiyo yanayoitwa "Mapinduzi ya Kikoperniki" ambayo ni ya msingi kwa ustawi wa sayansi ya kisasa.

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa Toruń, iliyokuwa mji wa Hanse huko Poland, katika familia yenye damu ya Kijerumani.

Alisoma theolojia, sheria na tiba huko Poland na Italia, akawa padri wa kanisa kuu la Frauenburg-Fromburg, ambapo alifariki mwaka 1543 akazikwa chini ya sakafu yake.

Mchango mkubwa alioutoa na tathmini yake[hariri | hariri chanzo]

Muda mfupi tu kabla hajafa alitoa kitabu chake "De revolutionibus orbium coelestium" (kuhusu mizunguko ya magimba ya angani), ambacho kinatoa mafundisho makuu ya elimu ya nyota ya siku zile, kama vile mpangilio wa sayari zinazolizunguka Jua na mzunguko wa Dunia kwenye mhimili wake kila siku.

Copernicus hakuwa mtu wa kwanza aliyewaza ya kwamba Dunia inazunguka Jua: miaka 2000 kabla yake wanafalsafa kadhaa wa Ugiriki waliwahi kufundisha hivyo. Lakini tangu maandiko ya Ptolemaio wataalamu wa nyota pamoja na walimu wa dini za Ukristo na Uislamu walikubaliana kwamba Dunia ni kitovu cha ulimwengu na Jua pamoja na sayari zote zinaizunguka. Kitabu cha Copernicus kilikuwa cha kwanza kilichoondoa Dunia katika kitovu cha ulimwengu na kwa ujumla alipingwa na wataalamu wengi.

Ingawa hoja zao hazikuwa sahihi, ni kweli kwamba mafundisho yake yalikuwa na kasoro zilizojulikana baadaye kwa maendeleo ya utafiti: kwa mfano, alidhani njia za sayari kuzunguka jua zina umbo la duara kamili. Pia alifikiri ya kwamba jua liko kwenye kitovu cha ulimwengu.

Mafundisho yake yaliathiri wanasayansi wengine kama Galileo Galilei na Kepler, ambao waliyathibitisha na kuyaboresha.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Kuhusu De Revolutionibus
Urithi wake
Ushirikiano wa Poland na Ujerumani kuhusu Copernicus
Makala hii kuhusu mwanasayansi fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Nicolaus Copernicus kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.