Dayosisi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Dayosisi (kwa Kilatini dioecesis, kutokana na Kigiriki διοίκησις, dioikesis, yaani "utawala") ni jina linalotumika katika madhehebu mbalimbali ya Ukristo (kwa mfano Walutheri na Waanglikana kumaanisha kitengo kilichopo chini ya usimamizi wa askofu katika eneo fulani.

Wakatoliki wanaoongea Kiswahili wanaiita jimbo, lakini kwa lugha nyingine wanatumia neno kama hilo bila ya kulitafsiri; kwa mfano "diocese" (Kiingereza), "diocesi" (Kiitalia) au "diocèse" (Kifaransa).

Historia[hariri | hariri chanzo]

Mwanzoni "dayosisi" ilikuwa kitengo cha utawala wa serikali katika Dola la Roma; dayosisi moja ilijumlisha majimbo kadhaa. Baada ya uenezaji wa Ukristo katika Dola la Roma Kanisa lilianza kutumia mipaka ya utawala wa serikali kwa ajili ya vitengo vyake na kwa njia hiyo muundo wa dayosisi ulikuwa pia muundo wa utawala ndani ya Kanisa. Baada ya kuporomoka kwa Dola la Roma jina hilo halikutumiwa tena upande wa serikali lakini likaendelea ndani ya Kanisa kwa ajili ya eneo lililo chini ya askofu.

Katika Kanisa Katoliki[hariri | hariri chanzo]

Mtaguso wa pili wa Vatikano uliweka mbele waamini kuliko eneo, hivi kwamba yanaweza kuwepo majimbo yasiyo na eneo maalumu, hasa kutokana na wingi wa uhamiaji uliopo siku hizi: "Jimbo ni sehemu ya Taifa la Mungu iliyokabidhiwa kichungaji kwa Askofu, akisaidiwa na mapadri wake, hivi kwamba kwa kuambatana na Mchungaji wake, na kuungana ndani ya Roho Mtakatifu kwa njia ya Injili na ya Ekaristi takatifu, iunde Kanisa maalumu, ambamo linakuwemo na kutenda Kanisa la Yesu Kristo, lililo Moja, Takatifu, Katoliki na la Mitume" (Christus Dominus) 11.

Kwa kawaida majimbo ya jirani yanaunda kanda ya Kanisa ("metropolitani"), mojawapo likiwa jimbo kuu (askofu wake ni askofu mkuu na anaitwa "metropoliti"). Majimbo yaliyo chini yake yanaitwa "sufragani".

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Dayosisi kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.