Bustani ya Edeni

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Bustani ya Edeni na Anguko la Binadamu, taswira ya Jan Brueghel Mzee na Pieter Paul Rubens, c. 1615

Bustani ya Edeni (kwa Kiebrania: גַּן־עֵדֶן gan-'Ēḏen) inatajwa katika Kitabu cha Mwanzo cha Biblia kama bustani nzuri iliyopandwa na Mungu alimoweka Adamu na Hawa baada ya uumbaji wa hao watu wa kwanza.

Katika tafsiri ya Kigiriki ya Biblia jina hili lilitajwa kama "Paradiso" (παράδεισος paradeisos) kutoka neno la Kiajemi ya Kale parādaiĵah) lililomaanisha eneo lililozungushwa kwa ukuta[1].

Inaelezwa katika Biblia kwenye vitabu vya Mwanzo 2-3 na Ezekieli 28 na 31. [2]

Mahali[hariri | hariri chanzo]

Mahali pa Edeni panaelezewa katika Kitabu cha Mwanzo kama chanzo cha mito minne.

Maelezo ya Mwa. 2, 10-13 yanasema: 10 Ukatoka mto katika Edeni wa kuitilia bustani maji, na kutokea hapo ukagawanyika kuwa vichwa vinne. 11 Jina la wa kwanza ni Pishoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Havila, ambako kuna dhahabu; 12na dhahabu ya nchi ile ni njema; huko kuna bedola, na vito shoham. 13 Na jina la mto wa pili ni Gihoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Kushi. 14 Na jina la mto wa tatu ni Hidekeli; ndio unaopita mbele ya Ashuru. Na mto wa nne ni Frati.

Lakini haiwezekani kutaja mahali maalum kwa maana, mbali na mito ya Frati na Hidekeli, mingine haijulikani, ila Gihoni inahisiwa kuwa Naili kwa kuwa inasemwa kwamba inazunguka nchi yote ya Kushi. Majaribio mbalimbali yamefanywa na wataalamu mbalimbali ila bila mapatano[3].

Makazi ya Adamu na Hawa[hariri | hariri chanzo]

Biblia ya Kiebrania inawaonyesha Adamu na Hawa wakitembea kuzunguka bustani ya Edeni uchi kwa sababu ya kutokuwa na ubaya wa dhambi.

Edeni inatajwa pia katika sehemu nyingine za Biblia kama vile Mwanzo, [4] katika Isaya 51:3, [5] Ezekieli 36:35, [6] na Yoeli 2:3; [7] Zekaria 14 na Ezekieli 47 hutumia taswira ya paradiso bila kulitaja jina la Edeni.

Sehemu ya pili ya simulizi la uumbaji kwenye Biblia inaanza katika mlango wa pili Mwanzo 2: 4-3: 24. Hapa YHWH - Elohim (inayotafsiriwa hapa "BWANA Mungu") anamwumba mtu wa kwanza (Adamu) na kumweka katika bustani aliyoipanda “mashariki mwa Edeni”. "BWANA Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa; na mti wa uzima katikati ya bustani, na mti wa ujuzi wa mema na mabaya." [8]

Mtu alikuwa huru kula matunda ya mti wowote wa bustani isipokuwa mti wa uzima na mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Mwisho wa yote, Mungu alimuumba mwanamke (Hawa) kutoka kwa ubavu wa mwanamume ili awe mwandamani wa mwanamume. Katika sura ya tatu, mwanamume na mwanamke walishawishiwa na nyoka kula matunda yaliyokatazwa, na walifukuzwa kutoka bustani ili kuwazuia kula matunda ya mti wa uzima, na hivyo kuishi milele. Makerubi waliwekwa mashariki mwa bustani, "na upanga wa moto uliogeuka huku na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima." [9]

Mtazamo wa Kiislamu[hariri | hariri chanzo]

Katika Kurani, mahali wanapokwenda hao watakaokubaliwa na Allah huitwa "jannat" (جنات) yaani bustani. "Bustani" (jannat) inatajwa mara kadhaa katika Kurani [10]. Katika mawazo ya Kiislamu hiyo bustani huwa na matabaka saba. Hapa majina ya Kiblia hutumiwa kwa namna tofauti kidogo.

Tabaka la saba na la juu ni "Firdausi" (فردوس) ambayo ni matamshi ya Kiarabu ya neno Paradiso[11]. Jina la Edeni linatumiwa kwa ajili ya "jannat adni" (جنات عدن)[12] ambayo ni tabaka la nne tu[13]. [14]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Katika nchi yabisi za Mashariki ya Kati, hadi leo bustani ni eneo lililoviringishwa na ukuta kwa kusudi la kulinda mimea, matunda na maji dhidi ya wanyama wa pori na wizi. Linganisha Moynihan, Elizabeth; Paradise as a garden: in Persia and Mughal India, uk. 1; New York 1979 ISBN 9780807609316
  2. Metzger, Bruce Manning; Coogan, Michael D (2004). The Oxford Guide To People And Places Of The Bible. Oxford University Press. p. 62. ISBN 978-0-19-517610-0. Retrieved 22 December 2012. 
  3. Wilensky-Lanford, Brook (2012). Paradise Lust: Searching for the Garden of Eden. Grove Press. ISBN 9780802145840. paradise lust.  Unknown parameter |url-access= ignored (help)
  4. Genesis 13:10 HE
  5. Isaiah 51:3 HE
  6. Ezekiel 36:35 HE
  7. Joel 2:3 HE
  8. Bible, Genesis 2:9 HE
  9. Bible Genesis 3:24 {{{3}}}
  10. Qur'an, 2:35, 7:19, 20:117, 61:12
  11. Kurani 23:11: " Ambao watairithi Pepo ya Firdausi, wadumu humo"
  12. Tafsiri ya Kurani kwa Kiswahili ya Sheikh Ali Muhsin Al Barwani haitumii neno "adn"; anatafsiri mara nyingi "bustani za milele" (Kurani 13:23, 18:31, 19:61 ) au "bustani za kudumu" (9:72), bustani za daima (98:8); Tarjuma ya "Al Muntakhab" katika tafsiri ya QUR'ANI TUKUFU imetafsiriwa Kiswahili na Sheikh Ali Muhsin Al-Barwani]
  13. Jannat al-ʿadn
  14. Wheeler, Brannon Mecca and Eden: ritual, relics, and territory in Islam k. 16, 2006

Kujisomea[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]