Ayubu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Ayubu, mchoro wa Léon Bonnat, 1880.

Ayubu au Yobu ni mhusika mkuu wa Kitabu cha Yobu, anayetajwa kwa heshima katika vitabu vya Ezekieli (14:14-18), Yoshua bin Sira (49:9), Waraka wa Yakobo (5:11) na Kurani (21:83).

Tangu kale anaheshimiwa na Wayahudi, Wakristo na Waislamu kama mtakatifu na pengine kama nabii pia.

Sikukuu yake huadhimishwa tarehe 10 Mei[1] au nyingine.

Ayubu katika Biblia[hariri | hariri chanzo]

Ayubu alikuwa tajiri aliyesoma na kumcha Mungu. Aliishi katika nchi ya Usi iliyokuwa mashariki kwa Palestina. Alipopatwa na mfululizo wa maafa, marafiki zake walikazania kwamba shida zile lazima zilisababishwa na dhambi zake za siri. Ayubu alikataa maneno yao. Alijua kwamba hakuwa mtu mkamilifu, lakini pia alijua kwamba maoni ya kawaida ya desturi za nchi ile, kama yalivyoelezwa na marafiki zake, hayakueleza jambo lolote. Majadiliano marefu yenye uchungu yaliyofuata yalijaza nafasi kubwa ya kitabu chote.

Elifazi (Ayubu 42:7) alikuwa ametoa mashtaka kwa Mungu kwamba watu humtumikia Mungu tu kwa sababu ya vitu wanavyoweza kupata kutoka kwake. Kama wangepata matatizo na shida wangemlaani (1:9-11; 2:4-5). Mungu akaruhusu maafa yaje juu ya Ayubu ili kupima uthabiti wa imani yake, na hivyo kuimarisha imani hiyo na kuongeza uzoefu wa Ayubu na Mungu (taz. Yak 5:11). Mateso ya Ayubu hayakuthibitisha hukumu ya Mungu juu yake, bali yalithibitisha matumaini yake katika Mungu na jinsi alivyomwamini.

Mkazo wa marafiki zake kwamba mateso au shida lazima vitokane na dhambi za mtu binafsi ulimfikisha Ayubu katika hali ambayo nusura ashindwe kuwavumilia zaidi. Lakini pia hali hiyo ilimsababisha amkaribie Mungu zaidi ambaye Ayubu alimwona kuwa tumaini lake pekee. Alipomlalamikia Mungu, inawezekana kuwa alikosa alipotumia lugha isiyostahili, lakini kwa hali yoyote alipeleka malalamiko yake kwa Yule aliyehusika.

Mwisho aliridhishwa, si kwa sababu maswali yake yote yalijibiwa, bali kwa sababu alikutana na Mungu ambaye alimlilia. Inawezekana kwamba Ayubu hakuelewa makusudi ya Mungu, lakini alijifunza kwamba Mungu huyo ambaye hekima yake ni kubwa sana kuliko ufahamu wa wanadamu, alistahili kutegemewa. Mungu hakuhitaji kujitetea kwa wanadamu, bali aliweza kufanya jambo lo lote alilopenda.

Mungu alipomthibitisha Ayubu, aliwaonyesha marafiki kwamba walikosa walipodai kwamba kila shida ni matokeo ya dhambi za mtu binafsi. Pia alionyesha kwamba Elifazi alikosa alipodai kwamba watu wanamwabubu Mungu tu, kwa sababu anawapa mambo mema na fanaka. Ayubu alidumu kuwa mwaminifu kwa Mungu, ingawa alipoteza kila kitu, lakini mwisho Mungu alimbariki kwa mibaraka mikubwa kuliko aliyokuwanayo hapo awali.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Martyrologium Romanum: ex Decreto Sacrosancti oecumenici Concilii Vaticani II instauratum auctoritate Ioannis Pauli P.P. II promulgatum, Romae 2001, ISBN 8820972107

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mtu wa Biblia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Ayubu kama habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.