Ziwa Van

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Ramani ya Ziwa Van
Ziwa Van pamoja na kanisa kwenye kisiwa cha Akdamar

Ziwa Van (kwa Kituruki: Van Gölü; kwa Kikurdi: Gola Wanêkwa; kwa Kiarmenia: Վանա լիճ, Vana lič̣) ni ziwa kubwa la chumvi na ziwa kubwa zaidi nchini Uturuki, mashariki mwa nchi.

Jiografia[hariri | hariri chanzo]

Ziwa Van iko katika nyanda za juu kwenye kimo cha mita 1,640. Linapokea maji yake kutoka milima jirani lakini hakuna njia ya maji kutoka; mto uliotoka zamani ulifungwa na miamba ya volkeno miaka milioni iliyopita.

Umbali kati ya miji Tatvan upande wa magharibi na Van upande wa mashariki ni kilomita 93, umbali mkubwa wa magharibi hadi mwisho wa hori upande wa mashariki ni km 127. Umbali mkubwa kutoka kaskazini hadi kusini ni km 52.

Kina kirefu ni mita 451.

Kuna feri ya reli inayozunguka baina ya Tatvan na Van. Treni za kimataifa baina ya Uturuki na Iran zinavuka hapa.

Chumvi na ekolojia[hariri | hariri chanzo]

Maji yake ni ya chumvichumvi, takriban nusunusu magadi na NaCl. Maji huwa kwa wastani na thamani pH ya 9.8. [1]

Kiwango cha magadi kwenye ziwa kinabadilika kufuatana na majira, pia ni tofauti kufuatana na kina cha maji. Maji yenye chumvi nyingi ni mazito zaidi, hivyo maji ya usoni hayana magadi mengi sawa na maji ya chini. Pia sehemu karibu na ufuko ambako mito inaingia huwa na maji matamu kuliko eneo la katikati.

Kuna spishi moja ya samaki pekee (alburnus tarichi) inayopatikana katika ziwa; wakati wa kuzaa wanarudi kwenye midomo ya mito ambako kiasi cha maji matamu ni cha juu zaidi, baadaye wanaweza kurudi katika sehemu ambako kiwango cha magadi ni juu kiasi.

Kuna aina nyingi za planktoni.

Ramani inaonyesha lugha za mazingira ya Ziwa Van kabla ya maangamizi ya Waarmenia; kibichi ni wasemaji wa Kiarmenia, njano ni Wakurdi.

Historia na utamaduni[hariri | hariri chanzo]

Katika milenia ya kwanza KK Ziwa Van lilikuwa sehemu ya milki ya Urartu.

Tangu karne ya 3 KK Ziwa Van lilikuwa katikati ya maeneo yaliyokaliwa na Waarmenia. Ushuhuda wake hadi leo ni monasteri ya Kiarmenia kwenye kisiwa cha Akdamar. Tangu maangamizi ya Waarmenia taifa hilo halipo tena hapa lakini watalii wengi Waarmenia wanatembelea Akdamar.

Siki hizi kuna Wakurdi wengi katika mazingira ya ziwa.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Andreas Reimer, Günter Landmann & Stephan Kempe, Lake Van, Eastern Anatolia, hydrochemistry and history. Aquatic Geochemistry 15: 195-222, 2009

Tovuti za Nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu: