Waanglia-Saksoni

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Waanglia-Saksoni (kwa Kiingereza: Anglo-Saxons) walikuwa Wagermanik wenye asili katika Ujerumani ya Kaskazini ya leo waliohamia Uingereza wakati wa karne ya 5 na 6 BK na kuwa wenyeji hata wakahesabiwa kama mababu wa Waingereza wa leo.

Jina linaonyesha kwamba walianza kama mchanganyiko wa makabila mbalimbali, maana "Anglia" ni sehemu ya jimbo la Schleswig-Holstein ya leo na Wasaksoni walikalia maeneo upande wa kusini-magharibi kutoka kule (kuanzia Saksonia Chini, Westfalia hadi Uholanzi na pwani ta kaskazini ya Ufaransa ya leo).

Historia yao katika Britania[hariri | hariri chanzo]

Hadi mwaka 400 kisiwa kikubwa cha Britania (Great Britain) kilikaliwa na makabila yenye lugha za Kikelti. Kusini mwa Britania (Uingereza na Welisi ya leo) kulikuwa sehemu ya Dola la Roma; Waroma walitawala juu ya wenyeji Wakelti waliojulikana kama Wabritania na wengi wao walizoea utamaduni wenye mchanganyiko kati ya ule wa Kiroma na ule wa Kikelti.

Mwaka 401 serikali ya Roma iliondoa jeshi lake Britania kwa sababu lilihitajika Italia. Sasa Wabritania wa Kiroma walishambuliwa kutoka Uskoti (kaskazini mwa Britania). Hivyo waliwakaribisha Wasaksoni kutoka ng'ambo ya bahari kuja Britania wakawaahidi eneo la kukalia na chakula kama shukrani kwa msaada wa kutetea wananchi dhidi ya Waskoti[1]. Baada ya muda mfupi Wasaksoni hawakuridhika tena na malipo yao na vita ilitokea ambako Wasaksoni walipanua eneo waliloshika. Vikundi vingine vya Wagermanik walifuata wakivuka Bahari ya Kaskazini na kuvamia Britania. Uvamizi huo uliendelea katika karne ya 5 na ya 6.

Mnamo mwaka 600 sehemu kubwa ya Uingereza ya leo ilishikwa na makabila ya Wagermanik, hasa Waanglia na Wasaksoni. Katika mikoa kadhaa kwenye pwani ya mashariki walifika pia watu kutoka Denmark na Norwei waliounda madola yao.

Wakazi asilia walianza kutumia lugha ya mabwana wao wapya, wengine walihamia maeneo ya mashariki ya Welisi, Cornwall yaliyotawaliwa bado na Wakelti na Gallia (Ufaransa leo).

Kutokana na mchanganyiko huo ulitokea utamaduni wa Kianglia-Kisaksoni. Lugha yao inayoitwa "Kisaksoni cha kale" imekuwa msingi wa lugha ya Kiingereza cha baadaye. Waanglia-Saksoni walifika Britania wakiwa na dini yao asilia lakini kisiwani waligeukia Ukristo.

Waanglia-Saksoni walishambuliwa tena na tena na Waviking wa Skandinavia walioanza kushika maeneo kwenye pwani ya mashariki. Katika mapigano hayo wafalme wao walitafuta usaidizi wa Wanormandi katika kaskazini ya Ufaransa.

Mwaka 1066 mtemi William Mshindi (William the Conqueror) wa Normandi alivamia Britania na kushinda jeshi la Waanglia-Saksoni akawa mfalme William I wa Uingereza. Wavamizi Wanormandi walikuwa mabwana wapya wa Britania ya kusini wakaendelea kushika maeneo yote ya Waanglia-Saksoni na kutawala kama tabaka la makabaila.

Kwa karne za kwanza baada ya uvamizi Kifaransa cha mabwana wapya kilikuwa lugha ya milki lakini polepole Wanormandi walizoea lugha ya watawaliwa waliopokea pia maneno mengi kutoka Kifaransa chao. Toleo la mchanganyiko huo ni lugha ya Kiingereza ambayo ni lugha ya Kigermanik yenye maneno mengi ya asili ya Kilatini-Kifaransa.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Gildas: On The Ruin of Britain (De Excidio Britanniae), §23 online hapa
Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Waanglia-Saksoni kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.