Mnuvi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Plectrogeniidae)
Mnuvi
Mnuvi wa Selebes (Thysanophrys celebica)
Mnuvi wa Selebes (Thysanophrys celebica)
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Chordata (Wanyama wenye ugwe wa neva mgongoni)
Nusufaila: Vertebrata (Wanyama wenye uti wa mgongo)
Ngeli: Actinopterygii (Samaki walio na mapezi yenye tindi)
Oda: Scorpaeniformes (Samaki kama mabocho)
Nusuoda: Platycephaloidei (Minuvi)
Ngazi za chini

Familia 6 na spishi 169, 29 katika Afrika:

Minuvi, songwe au vumbana ni spishi za samaki za baharini za nusuoda Platycephaloidei katika oda Scorpaeniformes walio na kichwa bapa na kipana. Spishi za familia Triglidae huitwa mnuvi pia lakini ni wana wa nusuoda Scorpaenoidei.

Anatomia na morfolojia[hariri | hariri chanzo]

Minuvi wanajulikana kwa umbo la mwili lisilo kwa kawaida, ambalo ni msingi wa mkakati wao wa uwindaji. Minuvi wametanuka juu-chini, maana mwili wao ni mpana lakini umekuwa bapa wenye kimo kidogo sana. Macho yote mawili ni juu ya kichwa kilichotanuka, na kupea uwezo bora wa kuona kama darubini ili kushambulia mbuawa wanaopita juu. Athari hiyo ni sawa na ile ya wayo. Lakini kinyume na wayo, minuvi wamerefuka zaidi, mkia unabaki wima na domo ni kubwa, pana na linganifu. Wana mapezimgongo mawili ambayo lile la kwanza linategemewa na miiba imara sita hadi tisa. Mapeziubavu ni makubwa kama yale ya ndugu wao mabocho.

Minuvi ni samaki wadogo hadi wakubwa kiasi. Spishi nyingi ni ndogo, kufikia urefu wastani wa sm 10, baadhi hukua hadi makumi kadhaa ya sm na spishi chache katika jenasi ya Platycephalus hujulikana kukua hadi urefu wa mita moja.

Minuvi wengi wana miiba miwili mifupi kwenye pande zote za kichwa chao na juu ya kichwa chao iliyo na sumu. Sumu hiyo, wakati haileti kifo, inaweza kusababisha maumivu na maambukizi siyo zaidi ya siku 2. Baadhi ya wavuvi wanaamini kuwa maumivu ya kuumwa na mvuvi yanaweza kupunguzwa kwa kusinga ute wa tumbo la samaki huyu huyu aliyeuma katika jeraha iliyotokana, kwa sababu ya tezi fulani katika tumbo lake.

Makazi[hariri | hariri chanzo]

Takriban minuvi wote ni samaki wa chini ya bahari ambao mara nyingi hupumzika moja kwa moja kwenye sakafu ya bahari. Kwa kawaida hawaogelei sana. Wanaweza kupatikana katika vina mbalimbali, kuanzia mita 10 hadi mita 1000 kando ya tako la bara.

Mwenendo[hariri | hariri chanzo]

Minuvi ni wagwizi na hujilisha kwa samaki na gegereka wadogo. Huotea, mara nyingi wakifukiwa katika mchanga au matope. Macho yao tu yanaonekana juu ya kimeng'enywa. Katika spishi nyingi rangi ya mwili wao inabadilika ili kulingana na mandharinyuma. Mbuawa wa kutumainiwa akitembea au kuogelea karibu na kichwa cha mnuvi, huyu anaruka mara juu na mbele akimeza mbuawa katika domo lake kubwa akitumia mchanganyiko wa upondaji na mfyonzo ili kuboresha nasibu ya kumkamata.

Kwa kuwa minuvi ni mbuai waoteao walikuwa wakitarajiwa kutulia kiasi na kutokutembea umbali mkubwa wakiwa wapevu. Hata hivyo, uchunguzi wa hivi karibuni umeonyesha kwamba sehemu ya wakazi wa spishi kadhaa za minuvi huenda mbali sana ili kutaga mayai.

Minuvi na binadamu[hariri | hariri chanzo]

Wavuvi huvua minuvi kwa vyambo mbalimbali vya asili na bandia kwa mwaka mzima, lakini ni kawaida zaidi kuwakamata wakati wa majira ya joto. Ni chache tu za spishi nyingi za minuvi ambazo hukamatwa na wavuvi mara nyingi. Spishi za minuvi zilizopatikana katika maeneo ya latitudo za juu zinapendwa zaidi kwenye meza. Jimbo la Australia la New South Wales lina uvuvi mkubwa wa kibiashara wa minuvi.

Nchini Japani spishi kadhaa huingizwa kwenye miradi ya majaribio ya ufugaji majini.

Spishi za Afrika[hariri | hariri chanzo]

Picha[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Rashid Anam & Edoardo Mostarda (2012) Field identification guide for the living marine resources of Kenya. FAO, Rome.
  • Gabriella Bianchi (1985) Field guide to the commercial marine brackish-water species of Tanzania. FAO, Rome.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mnyama fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mnuvi kama uainishaji wake wa kibiolojia, maisha au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.