Pezi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mapezi-tindi kwa samaki wa Teleostei, Samaki-taa wa Hector
(1) peziubavu, (2) pezitumbo, (3) pezimgongo,
(4) pezi-shahamu, (5) pezimkundu, (6) pezimkia

Mapezi ni sifa bainifu sana za mwili wa samaki. Hushirikishwa kwa miiba au tindi za mfupa zinazotokeza katika mwili na kufunikwa na kuunganishwa pamoja na ngozi, ama katika mtindo wa utando, kama inavyoonekana katika samaki wengi wenye mifupa, au sawa na kikono, kama inavyoonekana katika papa. Licha ya mkia au pezimkia, mapezi ya samaki hayana muungano wa moja kwa moja na uti wa mgongo na hutegemewa tu na misuli. Kazi yao kuu ni kusaidia samaki kuogelea. Mapezi yaliyomo katika sehemu tofauti kwenye samaki hutumikia madhumuni tofauti kama kusonga mbele, kugeuka, kukaa wima au kusimama. Takriban samaki wote hutumia mapezi wakati wa kuogelea, panzi-bahari hutumia mapeziubavu kwa kuumbia, na guguye huyatumia kwa kutembea. Mapezi pia yanaweza kutumika kwa madhumuni mengine; papa na msiha-mbu hutumia pezi lililobadilika ili kufikisha shahawa, karage hutumia pezimkia lao ili kuziraisha mawindo, mabocho wana miiba katika mapezimgongo yao yanayoingiza sumu, samaki washawishi hutumia mwiba wa kwanza wa pezimgongo lao kama fimbo ya uvuvi ili kuvutia mawindo, na vikande huepuka mbuai kwa kujifinya ndani ya ufa za miamba ya korali na kutumia miiba katika mapezi yao ili kujifunga kwenye mahali palepale.

Aina za mapezi[hariri | hariri chanzo]

Mapeziubavu[hariri | hariri chanzo]

Kila samaki ana jozi ya mapeziubavu, moja kwa kila ubavu nyuma ya vifuniko vya matamvua. Mapezi haya ni homolojia na miguu ya mbele ya Tetrapoda. Yanatumika kwa kutunza taraju.

  • Kazi ya pekee ya mapeziubavu, iliyoendelea sana katika samaki fulani, ni kuundwa kwa kani ya kuinua yenye msukumo inayosaidia samaki fulani, kama vile papa, ili kudumisha kina na pia inawezesha "kuruka angani" kwa panzi-bahari.
  • Katika samaki wengi, mapeziubavu yanasaidia kutembea, hasa katika mapezi kama ndewe ya samaki washawishi kadhaa na katika warukatope.
  • Tindi fulani ya mapeziubavu zinaweza kubadilishwa katika makadirio yanayofanana na vidole kama katika minuvi.
  • "Pembe" za shepwa na jamii yao huitwa mapezikichwa; kwa ukweli haya ni mabadiliko ya sehemu za mbele za mapeziubavu.



Mapezitumbo[hariri | hariri chanzo]

Mapezitumbo yanapatikana kwa kawaida chini na nyuma ya mapeziubavu, ingawa katika familia nyingine za samaki yanaweza kuwapo mbele ya mapeziubavu (k.m. tondi). Haya ni homolojia na miguu ya nyuma ya Tetrapoda. Mapezitumbo husaidia samaki kwenda juu au chini kupitia maji, kugeuka kwa kasi, na kusimama haraka.

  • Katika samaki wa aina ya goby, mapezitumbo huungana pamoja mara nyingi katika sahani moja la kumung'unyia. Hilo linaweza kutumika kujiambata kwa vitu.
  • Mapezitumbo yanaweza kuwa kwa mahali pengi kwenye tumbo wa samaki. Mahali pa kiasili kwa tumbo huonekana katika (kwa mfano) kasimba; mahali kwa kidari katika mbamba; na mahali kwa mataya, wakati mapezitumbo yapo mbele ya mapeziubavu, kama inavyoonekana katika samaki aina ya burbot.


Pezimgongo[hariri | hariri chanzo]

Pezimgongo lipo mgongoni. Samaki fulani anaweza kuwa na mapezimgongo moja hadi matatu. Mapezimgongo hutumika ili kulinda samaki dhidi ya kuvingirika na kumsaidia kwa kugeuka na kusimama ghafla.

  • Katika samaki washawishi, sehemu ya mbele ya pezimgongo imebadilika katika ilisio (illicium na eska (esca, mfano wa kibiolojia wa fimbo ya uvuvi na chambo.
  • Mifupa inayoegemeza pezimgongo inaitwa Pterygiophore. Kuna miwili au mitatu kati yao: mbele, katikati na nyuma. Katika mapezi ngumu sana yenye miiba ule wa nyuma mara nyingi umeungana na ule wa katikati, au hauko kabisa.

Pezimkundu[hariri | hariri chanzo]

Pezimkundu liko kwenye upande wa chini nyuma ya mkundu. Pezi hili hutumika kuweka samaki wima wakati wa kuogelea.








Pezi-shahamu[hariri | hariri chanzo]

Pezi-shahamu ni pezi nyororo lenye nyama linalopatikana mgongoni nyuma ya pezimgongo na mbele kidogo ya pezimkia. Halipo katika familia nyingi za samaki, lakini hupatikana katika tisa za oda 31 za Euteleostea (Percopsiformes, Myctophiformes, Aulopiformes, Stomiiformes, Salmoniformes, Osmeriformes, Characiformes, Siluriformes na Argentiniformes). Samaki maarufu wa oda hizi ni samoni, Characiformes (kama vile kasa, bembe, kachinge n.k.) na kambale.

Kazi ya pezi-shahamu ni kitu kama fumbo, ingawa taarifa kutoka mwaka wa 2005 zilionyesha kuwa trauti ambao pezi-shahamu lao limeondolewa wana ongezo la marudio ya kupiga mkia la 8%. Mara nyingi hutolewa kwa kualamisha samaki inayofugwa katika madimbwi. Taarifa za ziada zilizotolewa mwaka 2011 zimependekeza kama pezi hili linaweza kuwa muhimu kwa kutambua, na kuitika, michocheo kama vile mguso, sauti na mabadiliko katika shinikizo. Watafiti wa Kanada walitambua mtandao wa neva katika pezi hili, inayoonyesha kwamba inawezekana lina kazi ya hisia, lakini bado hawajui hasa matokeo ya kuliondoa.

Uchunguzi wa kulinganisha mwaka 2013 unaonyesha kuwa pezi-shahamu linaweza kuendelea kwa njia mbili tofauti. Moja ni njia ya aina ya Salmoniformes, ambapo pezi-shahamu hutoka kwenye kunyanzi la mapezi ya lava kwa wakati mmoja na kwa namna sawa moja kwa moja kama mapezi mengine ya kati. Njia nyingine ni aina ya Characiformes, ambapo pezi-shahamu hukawia kuendelea baada ya kupungua kwa kunyanzi la mapezi ya lava na maendeleo ya mapezi mengine. Inasemwa kwamba kuwepo kwa aina ya maendeleo ya Characiformes hupendekeza kwamba pezi-shahamu silo "tu asiya ya kunyanzi ya mapezi ya lava" na hakuendani na maoni kwamba pezi-shahamu halina kazi.

Pezimkia[hariri | hariri chanzo]

Pezimkia lipo mwishoni kwa shina la mkia na hutumika kwa kuendesha. Pezi hili linaweza kuwa na maumbo mbalimbali:

  • “Heterocercal (A)” inamaanisha kwamba mifupa ya uti wa mgongo inaingia kwenye ndewe ya juu ya mkia inayoifanyia kuwa ndefu zaidi (kama katika papa). Hiki ni kinyume cha “hypocercal”.
  • “Hypocercal”, pia inajulikana kama “heterocercal” kinyume, inamaanisha kwamba mifupa ya uti wa mgongo inaingia kwenye ndewe ya chini ya mkia inayoifanyia kuwa ndefu zaidi (kama katika Anaspida). Hiki ni kinyume cha “heterocercal”.
  • “Protocercal (B)” inamaanisha kwamba mifupa ya uti wa mgongo inaendelea mpaka mwisho wa mkia, ulio ni mlinganifu lakini kutokuwa na ndewe mbili.
  • “Homocercal (C)” inamaanisha kwamba mkia ni mlinganifu wenye ndewe mbili lakin mifupa ya uti wa mgongo inaingia kidogo katika ndewe ya juu.
  • “Diphycercal (D)” inamaanisha kwamba mifupa ya uti wa mgongo inaendelea mpaka mwisho wa mkia, ulio ni mlinganifu na kuwa na ndewe moja tu. Takriban samaki wote wa Paleozoiki walikuwa na mkia aina ya “diphycercal”.

Takriban samaki wote wa kisasa huwa na mikia aina ya “homocercal”. Hio inaonekana katika maumbo mbalimbali kama vile:

  • Mviringo
  • Katwa
  • Panda
  • Ukingo ndani
  • Mwezi

Mkuku wa mkia na vipezi[hariri | hariri chanzo]

Aina kadhaa za samaki wanaoogelea mbio zina mkuku wa mlalo mbele kidogo ya pezimkia. Kama mkuku wa meli hasa huu ni mwiniko kwa mbavu juu ya shina la mkia ulioundwa kwa skuto. Unampatia pezimkia uimara na egemeo. Inaweza kuwa na jozi moja ya mikuku, moja kwa kila upande, au jozi mbili juu na chini.

Vipezi ni mapezi madogo nyuma ya pezimgongo na pezimkundu (kambare wana vipezi upande wa juu tu).





Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya biolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Pezi kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.