Muhamad VI

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Mohammed VI (kwa Kiarabu: الملك محمد السادس للمغرب al-malik muhamad as-saadis lil-maghrib yaani "mfalme Muhamad wa sita kwa Moroko") ni mfalme wa Moroko. Anaitwa pia "Muhamad Ben Al-Hassan".

Amepokea cheo cha mfalme tarehe 23 Julai 1999 masaa machache baada ya kifo cha baba yake, mfalme Hassan II. Yeye ni mfalme wa 18 katika familia ya Waalawi anayetawala nchi hii.

Utoto na masomo[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa mjini Rabat tarehe 21 Agosti 1963 kama mtoto wa pili na mwana wa kwanza wa mfalme Hassan II na mke wake wa pili Latifa Hammou. Alisoma sheria kwenye chuo kikuu cha Rabat akachukua digrii ya kwanza mwaka 1985. Akaongeza masomo huko Ufaransa na kupokea shahada la daktari tarehe 29 Oktoba 1993 kwenye chuo kikuu cha Nizza kwa utafiti kuhusu „Ushirikiano kati ya Umoja wa Ulaya na nchi za Maghreb".

Siasa mpya[hariri | hariri chanzo]

Mohammed VI wa Moroko akikutana na rais wa Marekani George W. Bush huko ofisini mwake katika Nyumba Nyeupe ya Washington DC tarehe 23 Aprili 2002.

Mohammed VI ameanza siasa ya mageuzi. Mara baada ya kupokea cheo alihutubia wananchi akaahidi kupambana na rushwa na umaskini, kujenga uchumi wa kisasa na kuimarisha haki za wananchi.

Anapingwa na Waislamu wenye mwelekeo wa kidesturi hasa kwa sababu ya sheria mpya ya familia iliyopanua haki za wakinamama tangu mwaka 2004.

Ndoa yake[hariri | hariri chanzo]

Tarehe 21 Machi 2002 alimwoa mtaalamu wa kompyuta Salma Bennani aliyezaa mtoto wa kwanza Mulai Hassan ambaye ni mfalme mteule wa Moroko.