Madini

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Mineral)
Nyengwe (Pyrite) ni kampaundi ya chuma na sulfuri yenye fuwele nzuri
Uchimbaji wa madini katika mgodi

Madini (kwa Kiarabu: معدن, ma'adan; kwa Kiingereza: mineral) ni dutu mango inayopatikana duniani kiasili. Madini huwa na tabia maalumu ya kikemia, si mata ogania na mara nyingi huwa na muundo wa fuwele (kristali). Kwa lugha nyingine: madini ni elementi au kampaundi ya kikemia inayoonyesha umbo la fuwele na ambayo imejitokeza katika mchakato wa kijiolojia.

Kuna takriban madini 4,000 yaliyogunduliwa duniani. Miamba yote yanaundwa na madini na kuna hasa madini 30 yanayounda sehemu kubwa ya miamba duniani. Miamba kwa kawaida huwa na madini mbili au zaidi ndani yake.

Madini yapo kila mahali. Katika mazingira yetu kila jiwe limeundwa na madini. Ardhi ya shamba ina kiwango kikubwa cha madini ni punje za mchanga ambao ni mawe yaliyosagwa. Tukiwasha taa kuna madini kwenye uzi ya kuwaka na umeme umefika kwenye taa kupitia shaba ya waya; na shaba hiyo ni madini. Seli za mwili wetu huhitaji madini na hivyo ni muhimu kwamba chakula chetu kina kiasi kidogo cha madini ya lazima kama chuma au kloridi.

Madini kadhaa hupendwa kama vito (johari, mawe ya thamani) au pia dhahabu.

Madini ni kati ya vitu vigumu vilivo vya kawaida katika Dunia. Ni vitu viundanishavo mawe ya Dunia. Kuna baadhi ya madini huundwa na elementi moja tu. Nyinginezo huundwa na zaidi ya elementi mbili au zaidi.

Madini na miamba[hariri | hariri chanzo]

Madini ni tofauti na miamba. Madini ni kampaundi ya kikemia yenye viwango maalumu vya elementi ndani yake na kwa kawaida mfumo maalumu ya fuwele.

Mwamba huwa na madini ndani yake kwa mchanganyiko mbalimbali. Kwa hiyo sampuli mbili kutoka mwamba uleule zinaweza kuonyesha viwango tofauti za minerali husika. Kinyume madini daima huwa na tabia zilezile za kikemia. Kito cha yakuti kitakuwa sawa kama kimepatikana Australia au Asia.

Muonekano na ugumu[hariri | hariri chanzo]

Madini hutambulishwa na sifa kama rangi, ugumu, kiasi cha mwanga yanachoruhusu na mpangilio wa kristali. Almasi ni madini yaliyo magumu kuliko yoyote. Hutumiwa kukatia vitu vingine vigumu.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya kemia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Madini kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.