Al-Ghazali

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Abu Hamid Muhamad ibn Muhamad al Ghazali
Al Ghazali
Alizaliwa mnamo 1058 BK (450 AH)
Alikufa mnamo 1111 BK (505 AH)
Nchi Uajemi (Milki ya Waselchuki)
Kazi yake Mwanafalsafa, mwanatheolojia, mwanasheria wa Kiislamu

Abū Ḥāmid Muḥammad ibn Muḥammad al-Ghazālī (kwa Kiarabu:ابو حامد محمد ابن محمد الغزالی; kwa kifupi Al Ghazali, 1058-1111), alikuwa mwalimu mashuhuri wa dini, falsafa na sheria ya Kiislamu. Anahesabiwa kati ya walimu wa dini muhimu zaidi katika historia ya Uislamu.

Maisha yake[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa mjini Tus katika jimbo la Khorasan la Uajemi. Pamoja na mdogo wake Ahmad alilelewa kama mtoto yatima.

Akiwa kijana alifundishwa sharia ya Kiislamu akaendelea kuwa mwanafunzi wa mwanasheria wa Shafii ʿAbd-al-Malek Jovayni mjini Nishapur aliposoma pamoja na mwalimu Msufi.

Baada ya kifo cha walimu wake alipata ajira kwenye ikulu ya waziri Nezam-al-Molk aliyewahudumia watawala Waselchuki. Waziri alimfanya profesa wa sharia huko Baghdad alipofundisha kufuatana na madhhab ya Shafii.

Mnamo mwaka 1095 Al Ghazali alishambuliwa na mashaka makali kutokana na masomo yake katika falsafa ya Kiislamu akaacha nafasi yake ya ualimu. Alikatishwa tamaa pia kutokana na rushwa kati ya walimu wa chuo chake. Wakati ule ilikuwa vigumu kutoka katika utumishi wa mtawala, kwa hiyo aliomba rukhsa kuhiji Makka.

Miaka 11 iliyofuata hadi mwaka 1106 hakuna habari za hakika kuhusu shughuli zake. Katika kitabu alichoandika juu ya maisha yake mwenyewe Al Ghazali anasimulia jinsi alivyoguswa na nuru kutoka Allah iliyomrudishia hakika ya imani. Katika kitabu hiki anataja kipindi cha kufundisha kwenye madrasa huko Dameski, baadaye safari ya kutembelea kaburi la Abrahamu huko Hebron mnamo 1096. Hapa alitoa kiapo cha kutopokea pesa ya serikali tena, cha kutomhudumia kamwe mtawala yeyote na cha kutoshiriki katika mabishano ya kitaalamu tena.

Baada ya miaka hiyo ya kuzunguka kwa namna ya Wasufi alianza kufundisha tena kama profesa wa sharia huko Nishapur kwa miaka kadhaa. Baadaye alirudi kwake nyumbani mjini Tus alipokuwa na maisha ya kimya na kufundisha kibinafsi kama walimu Wasufi.

Mafundisho[hariri | hariri chanzo]

Al Ghazali alifahamu vizuri sana mapokeo ya falsafa kuanzia Wagiriki wa Kale na ya teolojia ya Kiislamu.

Kujisomea falsafa ilikuwa imemleta katika kipindi cha mashaka. Katika kipindi cha maisha yake kama Msufi alirudi kwa imani akaandika kitabu cha kueleza mipaka ya falsafa. Alikataza falsafa kama njia ya kufikia ukweli. Akapinga watangulizi wake kama Avicenna na Alfarabi akisema hao waliharibu imani ya Kiislamu kwa kutumia mno matokeo ya Aristoteli na Plato. Alisisitiza ya kwamba mantiki haiwezi kumweleza Mungu aliye mkuu kuliko akili ya binadamu.

Alipinga pia wenzake waliofundisha ulimwengu kuwa wa milele akitetea dhana ya uumbaji.

Maandiko yake kuhusu Usufi yalikuwa muhimu kwa kuleta kiwango cha upatanisho kati ya teolojia ya Kiislamu na harakati ya Wasufi. Alionyesha jinsi gani mazoezi ya Wasufi yanaweza kulinganishwa na kanuni za sharia akieleza desturi zao kwa undani. Kwa njia hii aliweza kupunguza uadui ya ulema dhidi ya Wasufi.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu mtu huyo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Al-Ghazali kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.