Robert Mugabe

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Robert Mugabe
Robert Mugabe 2009
Robert Mugabe 2009
Tarehe ya kuzaliwa 21 Februari 1924
Tarehe ya kifo 6 Septemba 2019
Chama ZANU
Kazi Rais


Robert Gabriel Mugabe (21 Februari 1924 - 6 Septemba 2019) alikuwa kiongozi mkuu wa Zimbabwe tangu 1980 hadi 2017. Alikuwa mwenyekiti wa chama tawala cha ZANU.

Mwaka 1980 alikuwa waziri mkuu na mwaka 1987 Rais wa Zimbabwe. Kabla ya wakati ule aliongoza upinzani wa ZANU dhidi ya serikali ya walowezi Waingereza nchini waliofuata siasa ya ubaguzi wa rangi.

Mugabe alirudia kushinda katika uchaguzi mara kadhaa. Tangu mwaka 2000 chaguzi hizo zilitiwa shaka kutokana na matishio na matumizi ya mabavu dhidi ya wapinzani. Utawala wa Mugabe umeitwa wa kidikteta tangu mwaka 2002. Kutokana na mashtaka dhidi ya serikali ya Mugabe ya kudharau haki za binadamu, nchi ya Zimbabwe ilisimamishwa ndani ya Jumuiya ya Madola. Mugabe pamoja na mawaziri wake na viongozi wa chama chake hawakuruhusiwa kusafiri kwenda nchi za Umoja wa Ulaya na Marekani.

Mwanzoni mwa utawala wake Mugabe alisifiwa kujenga uchumi na sera ya elimu nchini. Zimbabwe ilikuwa nchi iliyouza chakula kwa wingi nje. Tangu mwanzo wa milenia mpya pamoja na mashtaka ya udikteta hali ya uchumi ilirudi nyuma. Takriban raia milioni mbili wa Zimbabwe wameondoka nchini wakakaa kama wakimbizi Afrika Kusini.

Tuhuma za mauaji na ukandamizaji

Nchi hiyo ilikuwa tayari imegawanyika kikabila hata katika uchaguzi wa kwanza wa 1980, Mashona wote walimchagua Mugabe na Wandebele na wabunge kutoka chama cha ZANU. Wakati Wandebele walichagua viongozi kutoka chama cha ZAPU kilichoongozwa na Joshua Nkomo.

Baada tu ya kushika madaraka, Mugabe aliamua kukandamiza upinzani dhidi yake aliyoona kati ya wanachama wa ZAPU na wanajeshi wake wa ZIPRA waliowahi kurudi. Alishinda majaribio ya uasi wa askari wa ZIPRA 1980 kwa msaada wa vikosi vya Rhodesian Defence Force. 1981 Mugabe aliunda kikosi kipya cha "Brigedi ya Tano" kilichofanywa na wanamgambo wa ZANLA wa awali (jeshi la chama chake ZANU) na kufundishwa na washauri kutoka Korea Kaskazini. Brigedi hii ilitumwa katika maeneo ya Wandebele katika kusini ya Zimbabwe (mazingira ya Bulawayo) kutafuta askari wa ZIPRA mafichoni; katika mauaji ya Gukurahundi yaliyoendelea hadi 1984 ni Wazimbabwe 20,000 wanakadiriwa waliuawa.

Ingawa mauaji hayo hayakufikia kiwango cha yale ya Rwanda na Burundi, waliuawa wanawake, wanaume, watoto na hata vichanga vilivyokuwa matumboni.

Kuanzia enzi hizo rais Mugabe amejaribu kushinda kila uchaguzi nchini huko kwa kutumia nguvu za kikabila na mabavu.

Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Robert Mugabe kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.