Nusura

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Nusura Masharubu
muhusika wa Siri ya Mtungi

Taswira ya Nusura (uhusika umechezwa na Hidaya Maeda
Mwonekano wa kwanza Msimu wa kwanza sehemu zote
Imebuniwa na MFDI Tanzania
Imechezwa na Hidaya Maeda
Maelezo
Jinsia Kike
Kazi yake Mama wa nyumbani
Ndoa Mzee Kizito
Dini Mwislamu
Utaifa Mtanzania

Nusura Masharubu ni jina la uhusika kutoka katika tamthilia ya Kitanzania maarufu kama Siri ya Mtungi. Uhusika umechezwa na Hidaya Maeda. Muhusika pekee aliye na huzuni tangu msimu wa kwanza hadi wa pili. Awali katika mahusiano yake na mpenzi wake machepele Duma. Duma ana mnyororo wa wanawake licha ya kukataa mara kwa mara akiulizwa. Nusura ni msichana mwenye roho ya upendo kwa kila mtu aliye karibu nae. Nusura alipata malezi ya baba tu, bila mama, ijapokuwa ameonekana kumtembelea mama yake Bi. Sophia. Baba yake ni Mzee wa mjini anayejihusisha na vitendo mbalimbali vya kitapeli na udhulumati.


Mipango yake mingi hupanga na Duma anayeonekana kutoridhika na matendo ya Mzee Masharubu baba wa Nusura. Nusura ni muhusika asiyeyumbishwa na mtu yeyote yule. Si baba yake, mumewe wala marafiki zake. Ana misimamo, lakini vilevile mwepesi kuomba ushauri kwa marafiki zake wa karibu au mama yake. Nusura ni msichana jasiri na mwenye uvumilivu na asiyependa matatizo kwa wengine. Licha ya mateso na manyanyaso anayopata kutoka kwa mke mwenzie Bi. Farida bado hakudiriki kusema yale yote mabaya kwa mumewe Mzee Kizito. Nusura si machapele, lakini hapendi mwanaume asiye na msimamo na uaminifu katika mapenzi. Suala la usaliti wa kimapenzi uliofanywa na Duma ulipelekea kukubali wazo la kuolewa na Mzee Kizito ili kuepuka madhila na maisha ya anasa anayoishi mpenzi wake Duma. Misimamo ya Nusura ni mizito, Mzee Masharubu alichukua milioni 2 kutoka kwa Mzee Kizito kama mahari ya Nusura, lakini Masharubu aliisunda. Nusura alianzisha mbilinge hadi Masharubu kachojoa kiasi chote halali cha mahari yake. Tena alimsimamia kidete na kumweleza hii ni mahari yangu na huna ruhusa ya kuila.


Nusura anakubali kuolewa na Mzee Kizito baada ya safari nyingi za majaribio alizofanya Mzee Kizito kwa msaada wa Mjomba (Seif Mbembe) ili kufanikisha harusi. Kizito anamfananisha Nusura kama Vingawaje mke wake wa tatu aliyefariki ambaye alikuwa mama mzazi wa Sabrina Kizito. Sabrina na Nusura ni mtu na mama yake lakini wanaishi maisha mazuri na maelewano makubwa kama mtu na shogake. Maisha ya Nusura yanakuwa tatizoni na dimbwi kubwa la mawazo baada ya kupata ujauzito na kwenda hospitali na kuambiwa ameathirika na ugonjwa wa UKIMWI. Hali hii ilimhuzunisha sana na kupelekea kujiuliza maswali mengi sana. Huenda UKIMWI kaupata kwa kukubali kuwa mke wa tatu au kaupata kwa Duma hasa kwa kufuatia tabia yake kuwa na rundo la wasichana akiwa klabu ya muziki.


Isitoshe; hana uhakika kama mimba ya Mzee Kizito au ya Duma. Bado kuishi Maisha ya kuwa na mtoto mwenye virusi vya UKIMWI. Hii kabla hajapata ushauri kutoka kwa mama yake mzazi Bi. Sophia. Nusura ni msichana mwenye Bahati ya kupendwa na kila aliyekutana nae, hii ilithibitika alivyoenda kwa Bertha aliyekuwa anaishi na virusi vya UKIMWI akiwa mjamzito lakini alijifungua salama bila kumuambukiza mtoto kwa kushiriki programu maalumu inayotolewa na vituo vya afya ya uzazi wanaoishi na virusi vya UKIMWI. Binti yake alimpenda sana Nusura. Mama huyu alimwondoa hofu kabisa Nusura. Nusura ana urafiki wa karibu sana Julietta, Sabrina na mama yake mzazi. Ana muhushimu sana Mzee Kizito na hamuheshimu kabisa baba yake mzazi hasa kwa tabia zake za kibazazi. Nusura anaheshimu watu wazima wote isipokuwa wale wasiomuheshimu yeye mfano Bi. Farida.


Anampenda sana Bi. Mwanaidi japo hawaongei mara kwa mara. Nusura ni mke wa tatu baada ya Bi. Farida, Bi. Mwanaidi halafu yeye aliyekuja kuziba pengo la Vingawaje aliyekuwa mwimbaji wa taarab na inasemekana alikufa kwa kurogwa na Bi. Farida.[1][2]

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]