Mussa Azzan Zungu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Mussa Azan Zungu)

Mussa Azzan Zungu (alizaliwa 25 Mei 1952) ni mwanasiasa wa chama cha CCM nchini Tanzania na ni mbunge wa jimbo la Ilala tangu mwaka 2005.[1]

Tarehe 23 Januari 2020 aliteuliwa na rais John Magufuli kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira).

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Alipata elimu ya msingi katika Shule ya St. Joseph’s (sasa Forodhani) mjini Dar es Salaam kwenye miaka 1958 hadi 1965.

Kuanzia mwaka 1966 hadi 1967 alisoma Shule ya Sekondari ya Kinondoni akaendelea katika Shule ya Sekondari ya Tambaza mwaka 1968 hadi 1969.

Mwaka 1969 alijiunga na chama cha TANU akawa kiongozi kwenye tawi la chama shuleni.

Baadaye alihamia Toronto nchini Kanada aliposomea stashahada ya ufundi wa vyombo vya anga pamoja na urubani. Baada ya masomo alifanya kazi ya uhandisi wa ndege hukohuko Kanada hadi 1982. Mwaka 1983 alipata nafasi ya kazi katika Falme za Kiarabu hadi 1993 aliporudi Tanzania.

Mwaka 2000 alirudia siasa akachaguliwa kuwa diwani wa CCM kwenye Kata ya Mchikichini na kuingia katika Halmashauri ya Ilala, Dar es Salaam. Mwaka 2003 alikuwa Naibu Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala. Mwaka 2005 aliendelea kuchaguliwa mbunge wa CCM katika jimbo la Ilala akarudishwa mwaka 2010 na 2015[2].

Bungeni alichaguliwa kuwa naibu mwenyekiti wa kamati ya mambo ya nje 2007-2011, mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge wa Jumuiya ya Madola Tanzania na naibu mwenyekiti wa kamati wa Huduma za Jamii 2015 - 2018. 2012 na 2016 alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa bunge.[3]

Mnamo 2020 aliteuliwa kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) akahudumia hadi mwisho wa bunge na uchaguzi mpya. [4] Tangu kujiuzulu wa spika wa awali Job Ndugai na kuchaguliwa kwa uongozi mpya wa bunge, Zungu amekuwa naibu wa spika wa Bunge la Tanzania.[5]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Member of Parliament CV. Bunge la Tanzania (2010). Jalada kutoka ya awali juu ya 2013-11-03. Iliwekwa mnamo 2017-05-06.
  2. CV YA MBUNGE WA ILALA MH. MUSSA AZZAN ZUNGU, tovuti ya mussaazzanzungu.blogspot.com, iliangaliwa Januari 2020
  3. Mbunge wa Ilala Mussa Azzan Zungu achaguliwa tena kuwa mwenyekiti, tovuti ya Swahilitimes / Facebook
  4. Mussa Azzan Zungu Archived 25 Januari 2020 at the Wayback Machine., tovuti la Bunge la Tanzania, iliangaliwa januari 2020
  5. https://www.parliament.go.tz/leaders-list, iliangaliwa Fenruari 2023