Leo Africanus

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Picha hii ya mchoraji Mwitalia Sebastiano del Piombo ilitenegenzwa mwaka 1520; kuna uwezekano ya kwamba inamwonyesha Leo Africanus

Leo Africanus (kilatini: "Simba Mwafrika"; pia: Al-Hasan ibn Mohammed al-Wazzan na Ioannes Leo Medici) alikuwa mwandishi Mwarabu kutoka Hispania aliyesafiri katika maeneo ya Sahara na Sudan, kuwa Mkristo baadaye na mwandishi mashuhuri wa Ulaya juu ya habari za Afrika.

Utoto na masomo[hariri | hariri chanzo]

Alizaliwa mnamo mwaka 1490 kwa jina la الحسن بن محمد الوزان (Al-Hasan ibn Mohammed al-Wassan) katika mji wa Granada uliokuwa mji mkuu wa dola la mwisho wa Waislamu katika Hispania. Baada ya kutekwa kwa mji na Wahispania Wakristo 1492 familia yake ilihamia Fes (Moroko). Hapo kijana alisoma kwenye chuo kikuu cha Al-Qairawin.

Safari kwenda Timbuktu[hariri | hariri chanzo]

Baada ya kumaliza masomo yake aliongozana na mjomba katika safari zake wakivuka jangwa la Sahara na kufika mjini Timbuktu katika Dola la Songhai mnamo mwaka 1510. Akaendelea kuvuka kanda la Sahel hadi Sudan na Misri.

Maisha mapya katika Italia[hariri | hariri chanzo]

Katika safari kwenye Mediteranea jahazi yake ilishambuliwa na mashujaa wa msalaba mwezi wa Juni 1518 akakamatwa na kupewa kama zawadi kwa Papa Leo X huko Roma. Papa alivutwa na tabia na elimu yake akampatia mafundisho ya kikristo akabatizwa. Katika ubatizo alipokea jina la Papa mwenyewe "Leo" pamoja na jina la mtume "Yohane" na jina la "Medici" familia ya Papa: Ioannes Leo de Medici.

Leo alijifunza Kiitalia na Kilatini akafundisha lugha ya Kiarabu kwenye chuo kikuu cha Bologna. Amejulikana kama "Leo Africanus" kutokana kitabu chake "De Africae descriptione" (kiit. "Kuhusu aridhio ya Afrika"). Kitabu hiki kilikuwa chanzo cha pekee cha elimu juu ya dunia ya Kiislamu katika Ulaya ya karne ya 16. Ilileta mara kwanza habari za mji wa Timbuktu na utajiri wake wa kiuchumi na kiutamaduni mbele ya macho ya Ulaya. Leo alitunga pia kamusi ya lugha tatu za Kiarabu-Kilatini-Kiebrania.

Kurudi kwake[hariri | hariri chanzo]

Baadaye Leo alirudi Afrika akaishi Tunis. Anasemekana aligeukia tena Uislamu katika kipindi hicho cha mwisho wa maisha yake. Aliaga dunia Tunis mwaka 1554.

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]