Atacama

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Jangwa la Atacama, huko Chile.
Atacama ni eneo lenye rangi ya njano.

Jangwa la Atacama ni jangwa lililoko kaskazini mwa Chile. Linaenea kwenye kanda yenye urefu wa kilomita 1,000 kwenye pwani ya Chile, upande wa magharibi wa milima ya Andes. Eneo lake ni kilomita za mraba 105,000.

Atacama hutazamwa kuwa kati ya maeneo yabisi yaani makavu zaidi duniani.[1] Kuna sehemu zinazopokea chini ya milimita 25 za mvua kila baada ya miaka 10. Katika maeneo mengine, chini ya inchi (25 mm) ya mvua inanyesha kila miaka kumi. Moja tu ya mito inayotelemka kutoka milima ya Andes hufikia baharini kupitia jangwa. Mingine hupotea ndani ya ardhi kavu.

Sababu ya ukame wa Atacama ni mkondo baridi wa bahari unaotoka kwenye Bahari ya Kusini ukipita kwenye pwani ya Chile. Baridi ya maji hairuhusu hewa juu yake kushika unyevu, kwa hiyo mvua kidogo sana unafika barani, lakini kuna ukungu.[1] Wakazi wa pwani ya Chile wamejifunza kuvuna maji kutoka ukungu. Katika sehemu za jangwa hili haijanyesha kwa zaidi ya miaka 400. Ingawa Atacama ndio mahali pakavu zaidi ulimwenguni hiyo haimaanishi ndio mahali pa joto zaidi. Jangwa la Atacama kweli ni mahali pa baridi sana na hali ya joto kuanzia nyuzi 0 hadi 30.

Katika karne ya 19 chumvi ya nitrati mbalimbali ilichimbwa kwenye jangwa na utajiri huo ulisababisha vita ya shura baina ya Bolivia, Peru na Chile kati ya miaka 1879 - 1884. Chile ilishinda.

Ukavu wa hewa pamoja na uhaba wa makazi ya binadamu na wa mianga yao unarahisisha utazamaji wa nyota. Nchi za Ulaya zimejenga paoneanga patatu katika Atacama, na kituo kikubwa ni Atacama Large Millimeter Array inayounganisha viakisi parabola 66.

Picha za Atacama[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. 1.0 1.1 K. Buskey, Theresa. LIFEPAC, History and Geography. Alpha Omega Publications. p. 34. ISBN 978-1-58095-155-5. 

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu maeneo ya Chile bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Atacama kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.