Mubashara

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
kipindi cha mubashara kwenye TV ya Ujerumani

Mubashara (kutoka kitenzi ku-bashiri, kwa Kiarabu بشير; kwa Kiingereza live) ni istilahi inayotumiwa katika teknolojia ya redio, runinga na matangazo kwa njia ya intaneti. Kipindi mubashara hakiandaliwi kwenye studio bali kinarekodiwa papohapo na kurushwa moja kwa moja kutoka kamera (TV) au kinasasauti (redio na TV) hadi studio ambako picha au sauti husambazwa kwa wapokeaji. Kuna pia vipindi vinavyorekodiwa katika studio na kurushwa mara moja.

Vipindi mubashara vilianza kwenye michezo hasa wakati wa mashindano[1] na mechi za kandanda.

Picha na sauti hutokea kwenye runinga au redio kwa kuchelewa kidogo, kutegemeana na mbinu mbalimbali za kurusha. Kama mawimbi hupita kwenye satelaiti yanachukua muda mrefu zaidi. Hapa inaweza kutokea kwamba majirani wa uwanja wanasikia tayari kelele ya watazamaji baada ya goli, lakini picha na sauti za runinga zinafuata sekunde kadhaa baadaye.

Katika nchi kadhaa vipindi vya mubashara hucheleweshwa sekunde chache kwa makusudi; hii inampa mhariri nafasi ya kukata picha kama jambo linatokea lisilotakiwa kuonekana; mfano kama wakati wa uwindaji wa wahalifu na polisi (inayoonyesha kule mara nyingi kutoka helikopta ya shirika la TV) mtu anauawa. Mfumo huo ulianzishwa Marekani baada ya tukio la kuonyeshwa kwa titi la mwanaigizo Janet Jackson wakati wa mechi ya mpira mnamo mwaka 2004[2].

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Berlin 1936, Michezo ya Olimpiki ya Berlin 1936 ilikuwa tukio la kwanza la michezo iliyorushwa kwenye TV
  2. Oscar head angry at TV show delay, BBC 11.02.2004, iliangaliwa Desemba 2020