Mdudu Mdomo-ndani

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mdudu mdomo-ndani
Mdudu mkia-fyatuo wa jenasi Isotoma
Mdudu mkia-fyatuo wa jenasi Isotoma
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Arthropoda (Wanyama wenye mwili wa pingili na miguu ya kuunga wasio na ugwe wa mgongo)
Nusufaila: Hexapoda (Arithropodi wenye miguu sita)
Ngeli: Entognatha (Hexapoda bila mabawa)
Ngazi za chini

Nusungeli 3:

Wadudu mdomo-ndani ni arithropodi wadogo walio na mnasaba na wadudu wa kweli. Ngeli hii ina oda tatu: wadudu mkia-fyatuo (Collembola), wadudu mikia-miwili (Diplura) na wadudu mkia-sahili (Protura). Kama wadudu wa kweli wadudu hawa wana miguu sita lakini hawana mabawa na vipande vya mdomo viko ndani ya mfuko maalum katika kichwa. Kila pingili ya vipapasio ina misuli (kwa wadudu wa kweli pingili mbili za kwanza tu zina misuli). Madume hawaweki shahawa yao katika jike lakini huiweka katika kibumba juu ya aina ya kikonyo (spermatofori) ambacho jike hukiingiza katika ufunguzi wa uzazi wake akikubali. Majike wana kiungo cha kutaga mayai. Spishi nyingi hazina macho, lakini kuna spishi za Collembola ambazo zina macho madogo yasiyo na zaidi ya omatidio nane.

Uainishaji[hariri | hariri chanzo]

Tangu mwaka 2005 wanasayansi wameanza kushuku usahihi wa ngeli hii. Malinganisho ya ADN yanadokeza kwamba Collembola (wadudu mkia-fyatuo), Diplura (wadudu mikia-miwili) na Protura (wadudu mkia-sahili) hawana mnasaba karibu. Wataalamu wanafikiri sasa kwamba kila kundi ni ngeli tofauti na kwa hivyo ngeli Entognatha imekwisha kukiriwa.

Picha[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu "Mdudu Mdomo-ndani" inatumia neno (au maneno) ambalo si kawaida na matumizi yake ni jaribio la kutafsiri neno (au maneno) la asili Entognatha kutoka lugha ya Kilatini. Neno (au maneno) la jaribio ni mdudu mdomo-ndani.
Wasomaji wanaombwa kuchangia mawazo yao kwenye ukurasa wa majadiliano ya makala.

Kamusi za Kiswahili ama zinatofautiana kuhusu matumizi ya neno hili au hazieleweki au hazina neno kwa jambo linalojadiliwa.