Futa Djalon

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Futa Djallon)

Fouta Djalon (pia: Futa Jalon, Futa Djallon) ni eneo la milima nchini Guinea (Afrika ya Magharibi). Huitwa pia "Guinea ya Kati" (kwa Kifaransa: Moyenne Guinée, zone du Fouta Djalon). Makao makuu ya eneo hilo ni mji wa Labé.

Sehemu kubwa ya nyanda hizi za juu ni nchi ya nyasi na misitu kwenye vilima vinavyofuatana kwa kimo cha wastani cha mita 900 UB. Sehemu ya juu ni mlima Joura wenye kimo cha mita 1,515 (futi 4,970). Mmomonyoko wa maji umekata mabonde marefu katika mwamba wa juu.

Fouta Djalon hupokea mvua nyingi na hivyo mito mitatu mikubwa ya Afrika ya Magharibi ina chanzo hapo: ni Mto Niger, Mto Gambia na mto Senegal. Kwa hiyo huitwa tangi la maji kwa sehemu hii ya Afrika.

Wakazi asilia ni wakulima Wafulbe; lahaja yao ya Futa Djalon huhesabiwa kama lugha ya taifa ya Guinea.

Tangu karne ya 18 milima hiyo ilikuwa kitovu cha ufalme au usultani wa Kiislamu. Waislamu walianzisha vita ya jihadi dhidi ya wafuasi wa dini asilia za Kiafrika wakaanzisha dola la kidini. Mtawala aliitwa "Almami" (kutoka Kiarabu Al Imami). Almami wa mwisho, Bubakar Biro, alishindwa na Wafaransa mnamo 1896 kwenye mapigano ya Poredaka nchi ikawa sehemu ya koloni la Kifaransa.

Makala hii kuhusu maeneo ya Afrika bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Futa Djalon kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.