Antara

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Antara (Antares) katika kundinyota lake la Akarabu (pia: Nge) – Scorpius jinsi inavyoonekana kwa mtazamaji wa Afrika ya Mashariki
Ulinganifu wa ukubwa baina ya Antares (Antara), Simaki (Arcturus9 na Jua

Antara (kwa Kiingereza na Kilatini Antares; pia α Alpha Scorpii, kifupi Alpha Sco, α Sco) ni nyota angavu zaidi katika kundinyota la Nge (pia: Akarabu) (Scorpius). Ni pia nyota angavu ya 15 kwenye anga la usiku. Mwangaza unaoonekana unacheza kati ya mag 0.75 na 0.95.

Jina[hariri | hariri chanzo]

Antara ilijulikana kwa mabaharia Waswahili tangu miaka mingi wakifuata njia yao baharini wakati wa usiku kwa msaada wa nyota. [1]. Walipokea jina hili kutoka kwa Waarabu waliosema عنترة antarah, ingawa leo wanatumia zaidi قلب العقرب qalb al-aqrab (moyo wa akarabu - nge). Hii „Antara“ ilikuwa namna ya kutamka jina la Ἄντάρης an-ta-res walilokuta kwa Klaudio Ptolemaio katika kitabu cha Almagesti[2]. Lakini Waarabu walichukua maana yake kwa kumtaja Antara ibn Shaddad (ar. عنترة بن شداد ) aliyejulikana kwao kama mshairi na shujaa wa Uarabuni wa Kale kabla ya Uislamu. Ἄντάρης - Antares iliyotumiwa na Ptolemaio inamaanisha "sawa na Ares", ilhali "Ares" ni jina la Kigiriki kwa mungu wa vita (kama Kiroma Mars) na pia jina la sayari ya nne katika mfumo wa Jua yaani Mirihi. Sawa na Mirihi pia Antara inaonekana kuwa na rangi nyekundu kwa macho matupu; mwangaza unafanana pia hivyo si vigumu kuchanganya nyota na sayari hii..

Kwa matumizi ya kimataifa Umoja wa Kimataifa wa Astronomia ulifuata mapokeo ya Kigiriki na kuorodhesha nyota hii kwa jina la "Antares" [3].

Alfa Scorpii (au α Scorpii) ni jina la Bayer kufuatana na utaratibu ulioanzishwa na Mjerumani Johann Bayer katika karne ya 17. Inamaanisha ni nyota angavu zaidi (hivyo inatajwa kwa herufi ya kwanza kwenye alafabeti ya Kigiriki) katika kundinyota la "Scorpius" (kwa Kiswahili Akarabu au Nge).

Tabia[hariri | hariri chanzo]

Antara - Antares ni nyota badilifu na mwangaza unaoonekana wake unabadilika kati ya Vmag +0.6 na +1.6. Mwangaza halisi ni -5.3. Hivyo no nyota angavu ya 15 kwenye anga ya usiku.

Antara iko katika umbali na Dunia wa miaka nuru 550 – 600. Masi yake ni takriban M☉ 15 na nusukipenyo chake R☉ 680 (vizio vya kulinganisha na Jua letu). [4][5]).

Ni nyota jitu kuu jekundu katika kundi la spektra M1.5 Iab-b. Inaitwa jitu kuu kwa sababu masi yake ni kubwa vile, mara 15 ya Jua. Ikiwa nyota jitu kuu jekundu ni nyota iliyopanuka baada ya kuishiwa hidrojeni katika kitovu chake; katika hali hii kitovu cha nyota kinajikaza na myeyungano wa hidrojeni unahamia kwenye tabaka za nje za nyota. Hii inasababisha kupanuka kwa nyota na kuongezeka kwa mwangaza wake. Kama Antara ingechukua nafasi ya Jua letu, sayari za Utaridi, Zuhura, Dunia na Mirihi zingemezwa nayo maana kipenyo chake kinazidi obiti ya Mirihi.

Antara ina nyota msindikizaji kwa hiyo iki katika mfumo wa nyota maradufu. Nyota hii ya pili huitwa α Scorpii B. Ni ndogo kuliko α Scorpii A yaani Antara ikiwa na masi ya M☉ 7 na nusukipenyo cha R☉ 5[6] . Ni nyota ya safu kuu ikiwa katika kundi la spektra B2. Kutokana na mwangaza mkubwa wa Antara yenyewe si rahisi kuiona iligunduliwa wakati Mwezi ulipita mbele ya nyota kuu na kuifunika.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. ling. Knappert 1993
  2. Toomer, Ptolemy’s Almagest, p. 372
  3. Naming Stars, tovuti ya Umoja wa Kimataifa wa Astronomia (Ukia), iliangaliwa Novemba 2017
  4. Schröder, K.-P.; Cuntz, M. (April 2007)
  5. Ohnaka, K; Hofmann, K.-H; Schertl, D; Weigelt, G; Baffa, C; Chelli, A; Petrov, R; Robbe-Dubois, S (2013
  6. Kudritzki, R. P.; Reimers, D. (1978)

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Allen, Richard Hinckley: Star-Names and their Meanings; kwa G. E. Stechert New York, Leipzig, London, Paris 1899, ukurasa 59 (online kwenye archive.org)
  • Knappert, Jan: The Swahili Names of Stars, Planets and Constellations; The Indian Ocean Review September 1993 Volume 6 No. 3 September 1993, kurasa 6-7, ISSN 1031-2331
  • Ptolemy's Almagest, translated and annotated by G.J. Toomer, London 1984, ISBN 0-7156-1588-2 online hapa
  • Ohnaka, K; Hofmann, K.-H; Schertl, D; Weigelt, G; Baffa, C; Chelli, A; Petrov, R; Robbe-Dubois, S (2013). "High spectral resolution imaging of the dynamical atmosphere of the red supergiant Antares in the CO first overtone lines with VLTI/AMBER". Astronomy & Astrophysics. 555: A24 online hapa
  • Kudritzki, R. P.; Reimers, D. (1978). "On the absolute scale of mass-loss in red giants. II. Circumstellar absorption lines in the spectrum of alpha Sco B and mass-loss of alpha Sco A". Astronomy and Astrophysics. 70: 227 online hapa
  • Pugh, T.; Gray, D.F. (2013). "On the Six-year Period in the Radial Velocity of Antares A". The Astronomical Journal. 145 (2): 4. online hapa
  • A. Richichi (April 1990). "A new accurate determination of the angular diameter of Antares". Astronomy and Astrophysics. 230 (2): 355–362. online hapa.
  • Reimers, D.; Hagen, H. -J.; Baade, R.; Braun, K. (2008). "The Antares emission nebula and mass loss of α Scorpii A". Astronomy and Astrophysics. 491: 229–238. online hapa
  • Schröder, K.-P.; Cuntz, M. (April 2007), "A critical test of empirical mass loss formulas applied to individual giants and supergiants", Astronomy and Astrophysics, 465 (2): 593–601 online hapa

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]