Amerika

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Pitio kulingana na tarehe 19:25, 21 Desemba 2016 na Baba Tabita (majadiliano | michango) (→‎Historia: rekebisha kiungo cha picha)
Amerika duniani


Amerika ni jina la mabara mawili makubwa upande wa magharibi ya Afrika na Ulaya. Amerika iko kati ya Bahari ya Atlantiki na Bahari ya Pasifiki kwa urefu wa kilomita 15,000 kutoka kaskazini (rasi Columbia) hadi kusini (rasi Hoorn). Eeno lote ni 42,000,000 km² na jumla ya wakazi ni milioni 800.

Ramani ya Amerika yote

Eneo hugawiwa katika sehemu tatu au mbili, ama

au sehemu mbili za Amerika Kaskazini na Amerika Kusini pekee,

Hesabu ya pande tatu inalingana na jiografia inayotambua hasa mabamba matatu yanayobeba sehemu hizi tatu: Amerika ya Kaskazini hulala hasa juu ya Bamba la Amerika ya Kaskazini, Amerika ya Kati juu ya Bamba la Karibi na Amerika ya Kusini hasa juu ya Bamba la Amerika ya Kusini.

Katika hesabu ya mabara kwa kawaida Amerika ya Kati huhesabiwa kuwa sehemu ya bara la Amerika Kaskazini. Kiutamaduni Amerika ya Kati na ya Kusini kwa pamoja huitwa "Amerika ya Kilatini" kutokana na lugha na utamaduni wa Kihispania zilizofinyanga tabia za mataifa yake.


Jina la "Amerika"

Neno "Amerika" limetokana na jina la kwanza la Mwitalia Amerigo Vespucci (1451-1512). Vespucci alikuwa mbaharia na mfanyabiashara katika utumishi wa familia ya Medici kutoka Firenze (Italia). Tangu 1499 alisafiri kwenye pwani za Amerika ya Kusini na Amerika ya Kati akaandika kitabu juu ya safari zake. Hapa aliandika ya kwamba hakukubaliana na Kristoforo Kolumbus ya kwamba visiwa na nchi zilizofikiwa na Kolumbus zilikuwa sehemu ya Uhindi. Amerigo alipendekeza ya kwamba zilikuwa sehemu za "dunia mpya" au bara jipya akiwa mtu wa kwanza kuandika hivyo. Mjiografia Mjerumani Martin Waldseemüller alitumia jina la "Amerika" kwa heshima ya Amerigo alipochora ramani yake ya dunia ya mwaka 1507.

Historia

Wenyeji asilia kutoka Asia Kaskazini

Inaaminiwa leo ya kwamba hadi miaka 20,000 hadi 16,000 iliyopita hapakuwa na binadamu Amerika. Wakazi asilia walianza kuingia wakati ule kutoka Siberia (Asia ya Kaskazini) kupitia nchi kavu iliyopatikana wakati ule katika eneo la mlango wa bahari wa Bering kutokana na kipindi cha baridi.

Waindio wa Brazil

Hakuna uhakika jinsi gani uhamiaji huu ulitokea. Lakini wataalamu wote wakubaliana ya kwamba karibu wakazi asilia wote walitokea kutoka vikundi vya wavindaji walioingia Amerika kutoka Siberia na kusambaa hadi kusini kabisa. Kutoka vikundi hivi vilijitokeza mataifa na makabila mengi ya wenyeji asilia jinsi walivyoonekana wakati wa kuja kwa Wahispania wakati wa Kolumbus ambayo ni wakati ambako habari za maandishi zinaanza kupatikana.

Kuna dalili ya kwamba labda vikundi vidogo vilivuka bahari hata baadaye kutoka Ulaya, Afrika au Asia / Pasifiki na kuingia katika tamaduni za wenyeji. Ila tu haya yote hayana uhakika isipokuwa kufika kwa Wanorway mnamo mwaka 1000 waliounda vituo katika sehemu za Labrador (Kanada) zisizodumu muda mrefu.

Kuja kwa Wazungu

Kuja kwa Wahispania na Wazungu wengine kuanzia Kolumbus (1492) kulibadilisha historia na uso wa Amerika. Kolumbus aliamini ya kwamba aligundua njia ya kufika Uhindi akaita nchi mpya "Uhindi wa Magharibi" na wenyeji wake "Wahindi" - jina hili limebaki kwao katika lugha mbalimbali kama "Indio" (kihisp.) au "Red Indians" (kiing.). Tamaduni zote za Amerika hazikuanza bado kutumia chuma - silaha zao za mawe na ubao hazikuweza kushindana na silaha za watu wa Ulaya.

Wenyeji asilia walikufa kwa mamilioni hasa kutokana na magonjwa kutoka "dunia ya kale" ambayo hawakuzoea. Vita na utumwa vilichangia katika kupungukiwa kwa wenyeji asilia. Idadi kubwa za wenyeji asilia walibaki tu katika nchi za milima ya Andes.

Mazao za Amerika

Ulaya na mabara mengine ya dunia yalifaidika sana na maendeleo ya utaalamu wa kilimo yaliyopatikana katika Amerika: mazao kama mahindi, viazi, nyanya, maboga, kokoa na mengine yalipelekwa kutoka Amerika katika mabara yote na kuboresha malisho ya watu.

Amerika yote ilifanywa kuwa koloni ya nchi za Ulaya; Wahispania na Wareno walitawala sehemu za kusini; Waingereza na Wafaransa walishindana juu ya kaskazini ikiwa Waingereza walishinda. Mataifa madogo ya Ulaya kma Uholanzi na Denmark yalipata nafasi katika visiwa vya Karibi na katika Guyana.