Malawi Congress Party

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Nyasaland African Congress)

Malawi Congress Party (MCP) ni chama cha kisiasa nchini Malawi. MCP ilikuwa chama tawala nchini tangu uhuru hadi mwaka 1993.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Chama kitangulizi kilikuwa Nyasaland African Congress (NAC) kilichoundwa mwaka 1944 kwa shabaha ya kupanua haki za Waafrika wazalendo katika koloni la Nyasaland, jinsi Malawi ilivyoitwa kabla ya mwaka 1964.

Mwaka 1958 Hastings Banda alirudi nchini akachaguliwa kuwa mwenyekiti wa chama. Baada ya Banda kuzunguka na kuhutubia wananchi na kupinga Shirikisho la Afrika ya Kati serikali ya kikoloni ilitangaza hali ya dharura na kupiga NAC marufuku.

Badala yake viongozi wa awali wa NAC wasiokuwa gerezani waliunda Malawi Congress Party (MCP) iliyomtambua Hastings Banda kuwa kiongozi wake ilhali amefungwa jela.

Katika uchaguzi kabla ya uhuru mwaka 1961 MCP ilipata kura nyingi kikawa chama cha kuongoza nchi kwenda uhuru. Tangu mwaka 1966 kilikuwa chama pekee kilichoruhusiwa.

Baada ya mwisho wa udikteta wa Banda MCP ilizidi kushindwa katika uchaguzi mkuu lakini inaendelea kuwa chama muhimu katika Malawi.

Wakati wa uchaguzi wa mwaka 2009 ilipata takriban asilimia 30 za kura kitaifa.

Tovuti rasmi[hariri | hariri chanzo]